Sunday, July 24, 2011

Umeme: Jamii na watu binafsi waaminiwe katika kutafuta ufumbuzi

Nchi zetu za Kiafrika zimejenga utaratibu unaowafanya wananchi waamini kwamba bila serikali matatizo yao hayawezi kutatuliwa. Serikali inaonekana kujua kila kitu,kuwa na fedha zote duniani na kuwa bila mkono au mguu wa serikali hakuna anayeweza kusogea kwenda popote. Na serikali kwa upande wake inaelekea kuamini na kudhani ndiyo peke yake yenye majibu ya matatizo yote ya kiuchumi, kijamii, kisiasa, kiutamaduni na kiteknolojia. Kitu ambacho si kweli.

Guru wa Menejimenti, Profesa Peter Drucker anasema meneja mzuri na anayefanya kazi kwelikweli, hafanyi kazi yoyote. Ndivyo ilivyo pia kwa serikali nzuri na inayofanya kazi kwelikweli. Haifanyi kazi. Tunaposema haifanyi kazi hatuna maana haifanyi chochote au inategea tu. La hasha. Meneja na serikali bora na mfano wa kuigwa hufnaya kazi kwa kupitia watu, idara na taasisi nyingine. Unapoingilia kufanya kazi za watu wengine, idara na taasisi nyingine badla aya wao kuzifanya wenyewe kuna uwezekano mkubwa wa wewe kuvuruga kazi hizo au kutokuwa na tija linganifu wala ufanifu na ufanisi. Ni vizuri viongozi na mameneja wetu walielewe hili na wajipime na kuona kama kweli wanafanya kile ambacho kiongozi au meneja anachotakiwa kukifanya na sio kufanya anayoweza kufanya karani au tarishi. Kama sio waziri au mbunge au mkuu wa mkoa kama sio mkuu wa wilaya.

Tujiulize ni nini nafasi ya jamii katika ufumbuzi wa tatizo la umeme nchini Tanzania. Hivi leo, Benki ya dunia inamwaga misaada kwa ajili ya uanzishwaji wa miradi mbalimbali ya kijamii, jambo linaloashiria uwezekano wa kushirikiana na benki hiyo kuziwezesha jamii mbalimbali kuja na mawazo na mapendekezo kuhusiana na jinsi wanajamii wenyewe wanavyoweza kuchangia katika uzalishaji umeme nchini bila ya kutegemea sana wawekezaji toka nje. Maana wawekezaji hawaji kujenga miundombinu bali kuwekeza katika biashara au uzalishaji mali kwenye eneo walilojikita. Mjenzi wa miundombinu yetu ni lazima awe Mtanzania mwenyewe, mwanajamii katika jamii husika.


Wanajamii wa maeneo mbalimbali nchini hivi leo wanasita kujiunga na shughuli yoyote inayonukia ujamaaujamaa au ushirka ushrika kwani dhana hizo zilichakachuliwa vibaya mno na viongozi waliokuwa chini ya Mwalimu Nyerere. Ni yeye tu inaelekea alikuwa na nia safi na nzuri ya kubadili maisha ya Watanzania na sio wengine, na kama walikuwepo walikuwa wachache sana na walisakamwa kupita kiasi na mafisadi na walilia ubepari wa wakati huo.

Ni vyema pia kuzijua njia mbalimbali za kuzalisha umeme. Kisha kuainisha ni ipi au zipi ambazo zinaweza katika muda mfupi kutupa nafuu katika tatizo hili na zile ambazo zinahitaji muda na uwekezaji mkubwa zaidi.

Ziko njia mbalimbali za kuzalsha umeme zinazojulikana kufikia sasa. Njia hizo ni pamoja na mchakato wa nyuklia; samadi na takataka mbalimbali; mvuke; mashamba ya umeme wa solar; mashamba ya umeme wa upepo; mafuta ya petroli au dizeli na maji.

Tanzania inasemekana haijafikia hali ya kujitosheleza kiuwezo na kiusalama kuzalisha umeme kwa mchakato wa uranium ijapo tumejaliwa madini hayo. Kwa hiyo, hii sio njia ya kutusaidia katika siku za karibu.

Umeme kwa maji ndio huo ambao unatuongezea umaskini, maafa na dhiki zisizokweisha.
Nao huu unaweza kurudia hali yake ya kawaida endapo mipango yetu ya uoteshai miti, utunzaji mazingira na vilivyomo na hususan kwenye maeneo ya vyanzo vya maji milimani au chini ardhini itafanikishwa.

Uzalishaji umeme kwa kutumia samadi na takataka mbalimbali; upepo; mafuta ya petroli au dizeli ndio njia zinazoweza kuchangia haraka zaidi kumaliza tatizo hili.

Kwa jiji kama Dar es salaam uzalishaji umeme kwa kutumia takataka ni kitu kinachowezekana. Na njia hii itaua ndege wawili kwa jiwe moja. Kwanza, utaongeza megawati za umeme kwenye mtandoa wa umeme na pili utafanya jiji hili kuwa safi daima.

Mashamba ya umeme wa solar na upepo kwenye mikoa yenye jua na upepo wa kutosha yanaweza kuchangia gridi ya taifa kwa megawati kadhaa.

Kwenye miji na wilaya ambazo zina upepo wa kutosha ni dhahiri tukishirikiana na nchi kama Denmark na Netherlands tunaweza kupata 'shortcut' za kupata mitambo na vifaa vinavyohitaji na kuzalisha umeme chini ya mwaka mmoja.

Umeme wa jenereta zinazotuchafulia hali ya hewa, mazingira na kutupigia makelele unastahili kudhibitiwa na kuvumuliwa tu kutokana na ukweli kuwa hakuna ujanja mwingine.

Mitaani ili tusichafue zaidi hali ya hewa ni vyema maduka au makampuni kadhaa yakaungana na kununua jenereta kubwa zinazoweza kutosheleza maduka au makampuni yote yaliyo sehemu hiyo badala ya kila mmoja kuwa na kijenereta chake na hivyo kusababisha uchafuzi mkubwa wa mazingira kwa moshi, kelele na hewa ya carbon monoxide.

Inafaa pia kuuliza kama nchi zilizotuzunguka, yaani, Msumbiji, Malawi, Zambia, Kongo Kinshasa, Rwanda (ambayo imefanya kazi nzuri sana katika upatikanaji umeme kwa watu wake), Burundi, Uganda na Kenya zina hali gani kiumeme na tunaweza kushirikiana nazo vipi ili tuzalishe umeme kwa pamoja utakaotusaidia sote kupunguza au kumaliza kabisa tatizo letu la umeme.


Maendeleo ni vigumu kupatikana bila kuwa na mipango mizuri inayotekelezeka. Ni heri nchi kupiga maktaimu kwa mwaka mmoja hata zaidi ili kwanza ihakikishe imejipanga vizuri kabla ya kuwa na mpango wowote wa maendeleo usiotekelezeka.

Katika hili ni muhimu kuona kwamba viongozi mbalimbali wa nchi hii wanawekwa kwa misingi ya kujenga na kuendeleza sehemu husika. Hii ina maana kazi ya mkuu wa shrika fulani, mathalani, TANESCO, lazima iwe ni kulitoa shirika hilo kwenye ngazi ya chini kwenda ngazi ya juu kiutendaji na kiufanisi.

Ndivyo ilivyo pia kwa mwenyekiti wa kijiji, katibu kata, kiongozi wa tarafa, mkuu wa wilaya, mkuu wa mkoa wanavyotakiwa kuwa. Baadhi ya matatizo yetu kama hili la umeme kama watu hawa wangeliachiwa kufanya kazi kama watu huru labda linaweza kumalizwa huko huko kwani wao wanajua eneo lao vyema zaidi kuliko viongozi wa kitaifa na mbunge asiyewatembelea hadi uchaguzi mkuu ujao.

Nilishawahi kuzungumzia kwamba ukiwa na kiongozi halafu kiongozi huyo hana tatizo analolitatua, wala haichangamkii fursa yoyote ili kuongeza kipato au kuyafanya maisha ya walio chini yake kuwa bora zaidi-ni sawa na kuwa na watu bila kiongozi.

Kadhalika, kama una shirika, wilaya, mkoa au wizara ambayo haijulikani inashughulikia tatizo gani au kuchangamkia fursa gani za kimaendeleo katika eneo husika, basi mahala hapo hakuna kiongozi. Kuna mtawala. Na kwa bahati mbaya viongozi wengi tuliokuwa nao hawastahili kuitwa viongzi bali watawala au magavana.

Tofauti ya kiongozi na mtawala ni kwamba, mtawala kazi yake ni kusimamia tu kile kilichopto, yaani, kile ambacho kimeshaanzishwa na wengine. Na sio jukumu lake kubadili chochote au kufanya kazi zaidi ya usimamizi na kutoa taarifa kwa wakubwa wake. Wakati kiongozi, ni mtu mwenye dhamana za kuleta mabadiliko toka hali duni kwenda hali bora zaidi. Kiongozi huonyesha kwa vitendo, hushauri, huelekeza, huelimisha, huwezesha na hutoa motisha ili walioko chini yake walete mabadiliko tarajiwa katika eneo husika.

Kiongozi tofauti na mtawala, huona mbali na mbele zaidi. Ni mtabiri wa namna fulani. Hufahamu fika kwamba haya ya kawaida watu walio chini yake wanayajua na wanaweza kuyashughulikia. Lakini yale ya mbele na yajayo na yasiyo tabirika ndio eneo la kuonesha uongozi wake.

Mathalani, mtawala huwaza jinsi ya kuwalisha watu wake leo leo. Wakati kiongozi anatakiwa kuwaza, kupanga na kuweka mikakati ya watu wake kupata chakula bila tatizo miaka mitano au kumi ijayo.

Mtawala huwaza kutatua tatizo la umeme leo leo, lakini kiongozi hutafakari, hupanga na kuweka mikakati inayouliza maswali ya msingi na yasiyo na majibu ya haraka. Kwa mfano, kama tutakuwa na ukame, yaani, mvua hazitanywesha na umeme wetu unategemea maji, ni njia gani mbadala tutakuwa nazo ili ukame na kukosa mvua kuisisababishe matatizo ya upatikanaji umeme.

Kiongozi mzuri huwatumia walio chini yake kutokana na uwezo na utalaamu walio nao bila kujali watokako wala udhaifu wao. Ubora na kile mtu anachoweza kukifanya katika kutimiza lengo lililoko mbele yake ndio kitu muhimu kuliko vyote. Na kiongozi bora, hatokei hata mara moja, kuwalaumu walio chini yake kwamba wameshindwa kazi fulani. Wakishindwa ina maana ni yeye ameshindwa na sio walio chini yake. Aghalabu, kiongozi mzuri na bora, huwaongoza watu kwa namna ambayo watu wao wanapofanikisha malengo fulani basi watu hao kwa pamoja husema, 'tumeweza, tumeshinda!' na sio kiongozi wetu ameweza, ameshinda!

Kiongozi bora na hususan akiwa wa wilaya au mkoa au nchi hupaswa kujua mambo ambayo mkoa wenyewe unastahili kutengeneza au kuzalisha na yale ambayo kwa muda fulani yapasa kuyapata toka kwa wengine.

Ni kichekesho kwa nchi kuwa na mpango unaotaka kuongeza asilimia ya nyumba zinazopata umeme toka asilimia 5 hadi asilimia ishirini na tano au hamsini, bila ya kuwa na mpango wa uzalishaji mashine, vifua umeme, mitambo na zanatepe mbalimbali zinazohitajika ili nchi yenyewe ijitegemee angalau kwa asilimia 80 kwa vitu vinavyohitajika kuzalisha, kusambaza na kuunganisha umeme nchini.

Kama nilivyodokeza huko nyuma, jambo hili sasa ni rahisi na jepesi kuliko wakati wowote katika historia ya nchi yetu na maendeleo yetu. Maana, hakuna sheria inayosema ili tuendelee lazima tuwatumie tu Watanzania au raia wetu hata kama hawajui na hawajasomea kazi inayotaka kufanyika. Na eti, hata kama kuna wahandisi au mafundi wa umeme,, maprofesa wa umeme, washauri, wanafunzi na watafiti wa masuala ya uzalishaji umeme wasio na kazi wala mafunzo kwa vitendo nchini na nchi za nje lazima tutegemee shirika moja tu nchini kutunusuru na balaa na maafa yanayoikumba nchi na watu wetu leo.

Kutokuona na kutozithamini na kutozitumia rasilimali watu zilizotapakaa huko Marekani, Ulaya Magharibi, Ulaya Mashariki, Russia ya zamani na kwingineko kutafuta ufumbuzi wa matatizo yetu mbalimbali ya kijamii, kiuchumi na kiteknolojia
ni jambo ambalo tutakaa na kuja kulijutia baada ya muda si mrefu kutoka sasa.

Miaka mingi iliyopita kulikuwa na Baba Baa na Baba Waa. Wote wawili walikuwa na mashamba makubwa yenye mimea ya kila aina pamoja na maeneo wazi, yaani, yasiyopandwa chochote. Msimu wa kilimo ulivyofika, Baba Baa alikuwa akiwatafuta vibarua wa kikwao tu, hakutaka wageni walime shamba lake. Aliamini hawajui kulima.Lakini mwenziwe Baba Waa aliwamwagia ajira Warundi, wamakonde, wasafwa, Wanyarandwa bila kubagua. Katika mchanganyiko huu wa watu wenye asili mbalimbali shamba la Baba Waa sio tu lililimwa vizuri bali lilinufaika na mimea mipya, njia mpya za kilimo, kama vile kupiga matuta na kadhalika. Hivi leo wajukuu wa Baba Baa hawana lolote maana shamba lilimshinda na hatimaye akaliuza. Wajukuu wa Baba Baa wangali na shamba la babu yao, na Mungu kawaongezea zaidi kwa kuwa na viwanda, maduka na mahoteli ya kitalii! Tafakari! Akili kichwani mwako!

Monday, July 11, 2011

M a l e z i y a w a t o t o h a y a e n d a n i n a t u n a k o t a k a k w e n d a

BILA shaka toka nchi hii ianze kuukumbatia ubepari, soko huria na utandawazi tumeanza kuona mabadiliko makubwa sana katika tabia za watoto na vijana wa KItanzania.

Taifa la watu waliokuwa wema, wapole, wenye huruma, heshima na adabu limeanza kuwa kitu tofauti kabisa. Na hakuna anayeonekana kutaka kukemea huku kukengeuka. Sio vyombo vyetu vya habari au dini zetu wala sio serikali isiyokuwa na dini.

Aghalabu wengi hushtuka kutokana na utovu wa adabu, ukosefu wa heshima na hulka za kiajabuajabu ambazo inadaiwa ni kwenda na wakati.

Kwa namna fulani hali hii inatokana na kukua kwa kasi kwa ubinafsi na watu kujiamini kuwa wanaweza wakajitosheleza kwa kila kitu na wakawalea watoto wao bila msaada wa mtu mwingine.

Matokeo yake hivi leo sio tu kwamba watoto hao wanakuwa kero na maudhi kwa watu wengine lakini hata kwa wazazi wao wenyewe.

Pengine huu ni wakati muafaka wa kuvuta hatua moja nyuma na kujiuliza kama malezi haya ya leo kweli ndiyo yatakayolifikisha taifa letu pale tunapotaka liende ?

Nina wasiwasi mkubwa kama malezi haya kweli ndiyo yanayowafaa watoto wetu. Na kamwe waoto hawawezi kulaumiwa bali ni wazazi wao, viongozi wao wa dini, jamii yao, wanasiasa wao, na taifa lao.

Wazazi ndio wanaoshika usukani hata kama sio moja kwa moja. Na wao wanapochelea kuikosoa serikali na viongozi wao kwamba wanapeleka upogo kizazi kijacho hawatakuwa na kuwamlaumu ila kujilaumu wenyewe.

Pengine upofu huu unatokana na uchu wa viongozi wa dini kupata waumini ndivyo sivyo ili mradi sadaka inayopatikana ni kubwa na wao wanaishi maisha ya kifahari? Au pengine upofu huu unatokana na kukosa chama huru cha wazazi na viongozi wa wazazi wasio wanasiasa. Au pengine upofu huu unatokana na ubinafsi na tamaa ya kuonekana tofauti na watu wengine.

Potelea mbali sababu iwayo, lakini ukweli unabakia palepale kwamba kauli na vitendo vyetu leo ndivyo vinavyosaidia kurithisha tabia, hulka na mienendo ambayo sisi wazazi tulio wengi tunaonekana kuirithia.

Kauli na vitendo vya mzazi wa Kitanzania leo vimetawaliwa na vinatafiriwa na umimi na ubinafsi wa hali ya juu iwe nyumbani, kazini, njiani au michezoni. Na kiongozi mmoja alilipalilia hili kwa kiasi kikubwa pale alipowaambia Watanzania kuwa: ' Kila mtu atabeba msalaba wake mwenyewe!'

Lakini tunachoshindwa kujua sisi wazazi ni kuwa mtoto huzaliwa hana tabia yenye uhakika. Na tabia ni matokeo ya kuzungukwa na wazazi wake na jamii yake na yale yanayomtokea katika maisha yake. Na kama shamba lako halina magugu (kwa maana huna watoto wenye tabia mbaya) lakini aghalabu utakuwa umezungukwa na mashamba yenye magugu (majirani wenye watoto kisirani) na hivyo hatimaye magugu pia huingia shambani kwako kwa kushtukizia na kwa athari mbaya zaidi. Maana, wanao ni weupe na hawana wanalolijua.

Hebu, tuangalie sampuli kadhaa za wazazi na jinsi wanavyoathiri viongozi wa kesho na keshokutwa. Tuanze na huyu masikini aliyeko barabarani na ana watoto kadhaa. Watoto hao hawaendi shule bali wanamsaidia mzazi wao kazi. Kwa kuwa kazi ya baba au mama ni ombaomba, wanamsaidia kuomba kama mzazi wao. Hebu fikiria wewe mwenyewe je huyu atakuwa Mtanzania wa aina gani akiwa mtu mzima?

Baadhi ya wazzazi tunalia machozi ya mamba. Tunajifanya tuna uchungu sana na mayatima. Tunaanzisha vituo vya kulea mayatima. Lakini ukiangalia kwa undani vituo hivyo havina dhati ya kuwalea mayatima hao bali kumpatia mwenye kituo utajiri wa haraka haraka. Hivi kweli watoto waliotoka katika mateso ya uyatima au mama wa kambo wakakutana na kadhia kama hii watakuwa na utu gani. Na kwa nini yatima alelewe kwenye kituo. Kuna yatima wangapi Tanzania? HIvi haiwezekani kwa watu wenye uwezo kuwachukua na kuwalea mayatima hawa majumbani mwao ili wawe na maisha yaliyofanana na ya watoto wenye wazazi wawili? Hatujui dini yako inasemaje, wlala thawabu utakazopata au madhambi utakayofutiwa, lakini kitendo hiki kitahakikisha kuwepo kwa taifa bora zaidi kuliko hali ikiwa kinyume cha hivyo.

Aina nyingine ya wazazi ni wale wa tabaka la chini kimaisha. Wazazi hawa aidha wanafanya kazi au wana biashara fulani au ni wakulima. Lakini kutokana na ugumu wa maisha baba anaamua kuwa mlevi, wengine wanazidisha starehe ili wasahau maumivu na wengine wanakwepa majukumu yao kama wazazi. Si uongo, ulevi noma. Familia nyingi zinasambaratika kutokana na baba na balaa zaidi hata mama kuwa walevi. Je, matangazo kwenye redio na televisheni yanatosha kuwafanya wazazi hawa wapunguze idadi ya sigara na chupa za bia wanazosaidia serikali kuongeza bajeti yake?

Umewahi kukutana na mtoto wa mlevi au baba asiyejua majukumu yake kwa familia yake ? Nguo chakavu na chafu, kapauka (hana mafuta ya kujipaka), midomo mikavu (hakupata kifungua kinywa asubuhi), hana begi labda mfuko wa marlboro na kadhalika. Ikionesha dalili kwamba hakuna kitu kinachoitwa ustawi wa jamii hapa nchini na kama kipo basi hakifanyi kazi. Kimekufa. Je, taasisi hiyo inasaia kujenga chuki, husuda na roho mbaya miongoni mwa watoto kama hawa au inajenga amani na umoja wa kesho?

Kuna wazazi wa lile tabaka la pili ambao juzi na jana walikuwa na hali nzuri kiasi, wana nyumba, gari na wanakula milo 3 kwa siku. Lakini toka peteroli na bei ya vyakula ianze kupaa juu kuliko roketi na shilingi kuzidi kuporomoka maamuzi magumu yanabidi kufanyika. Kuweka gari peteroli na kula ugali kwa matembere au....

La ajabu, katika familia hizi tofauti na wenzetu kwingineko Afrika Mashariki pamoja na jamaa hawa kuwa na intaneti hakuna anayewafundisha wanawe ujasiriamali, ubunifu na uzuzi wa mambo mapya. Tunalea 'Kisukuma' baba linafanya kazi zote na wake na watoto wake kazi yao ni kula tu. Na jinsi mtu anavyolisha watu wengi ndivyo anavyozidi kuwa maarufu.

Lakini ni dhahiri kuwa vijana wa miaka 14 sio watoto tena. Hawa ni watu wanaoweza kufunzwa jinsi ya kushiriki moja au mawili ya faida kwao na wazazi wao leo na kesho. Tunapojenga utegemezi wa kupita kiasi mwishowe ni kuwa na nyumba zinazofanana na zile za Uswahilini pale Kariakoo. Utamkuta baba na mama, watoto wo wa kiume wanne na sita wa kike. Na hao watoto sita wa kike wote wamezalia nyumnbani na wajuku wanalelewa na bibi na babu. Kazi kweli! Uzazi wa namna hii ni chanzo kikubwa cha umasikini wa uzeeni. Na kama serikali ina nia ya kweli ya kuwasaidia wazee basi ianze kwa kuwapunguzia wazazi wa namna hii mzigo kama huu.

Ni wazazi hawa pia wanaotujali kwa kutuletea kizazi kipya na bidhaa zao. IKiwemo muziki wa kuiga au wa kinyani toka Marekani, kuvaa suruali inayoacha nusu ya makalio nje au sketi na vigauni ambavyo vinaacha sentimeta chache tu kuona sehemu nyeti-kwa kisingizio cha kwenda na wakati. Na baba na mama nyumbani wanawaunga mkono watoto wao. Mwisho wa yote humjui mzazi ni nani na mtoto ni yupi. Wote ngoma sawa. Balaa na mikosi ikianza kila mtu anaanza kumlaumu Muumba, maana hata kuomba tena hawajui. Uhuru huu usiokuwa na mipaka sio uhuru unaowasaidia vijana wetu wala taifa letu. Ya ngoswe muachieni ngose. Nina hakika tukiuenzi Uafrika wetu na kutunza adabu na heshima yetu basi tutakuwa na bidhaa bora zaidi na zinakubalika kimataifa kuliko ilivyo sasa. Msaada wa vyombo vya habari katika hili ni muhimu sana.

Halafu, tuna wazazi wa tabaka la tatu au matajiri wakubwa au vizito. Hawa wanaajiri, hawaajiriwi. Wana viwanda, biashara kubwa au shule au vyuo au hospitali na kadhalika. Kutokana na wingi wa mali hata watoto wao wa miaka 10 huchukua magari na kuingia nayo barabarani. Kwa kuwa sina utajiri wa kiasi hicho, labda niulize tu hivi mzazi kumfanya mwanawe aamini utajiri wake ni utajiri wa mwanawe pia kunamsaidia au kunambomoa kijana wake. Aidha, kwa viongozi au vigogo wa kisiasa wanaojua kazi moja tu ya kufundisha watoto wao-siasa, je, kutaka mwanao awe kama wewe kunamsaidia au kunamdumaza mwanao. Na je, ulicho wewe ndicho anachoweza kuwa yeye ? Baadhi ya wazazi ndio wanaomiliki televisheni. Tuwaulize wanaridhika kwa wajukuu zao kuona kile kinachooneshwa ?

Awe ni mtoto wa masikini au tajiri, mwenye wazazi au yatima, mwenye akili au mjinga, mweupe au mweusi, Mkiristo au Mwislamu hawa wote ni watoto wetu na hii ni nchi yetu na haya ndiyo malezi yetu. Swali la mwisho ni je hii amani na huu umoja tunaojivunia sana hapa Afrika watavirithi kwa malezi haya ?

Friday, July 8, 2011

Sabasaba: Dhana na Upeo wake vipanuliwe

Maonyesho kama yale ya Sabasaba kama yakiangaliwa upya na eneo kubwa zaii kupatikana yanaweza kuwa ni kivutio kikubwa cha utalii, wawekezaji na biashara kubwa kubwa duniani.


Katika kujipanga upya huko, kwanza, eneo jipya litafutwe ambako kutajengwa uwanja mpya utakaofaa uitwe Dar es salaam Internationl Expo -Tanzania.

Maonyesho haya yawe ni ya kimataifa. Yaani, bidhaa, tekhonhama na mitambo mbalimbali itakayooneshwa hapo iwe ni ile inayoweza kununuliwa na nchi zote zinazotuzunguka.

Uwanja huu unastahili kuwa ni wa ubora wa kimataifa na ingelikuwa ni vyema upatiwe kiwanja kipya ambacho kitaweza kuwa ni kijiji cha kudumu kwa maonyesho ya expo mbalimbali.

Wakati huo huo, kila mkoa unastahili kuwa na maonyesho yake ya sabasaba wakati ule ule yale ya Dar es salaam yanapofanyika.

Katika kufanya hivyo tutadhihirishia umma kwamba Dar es salaam sio Tanzania, na Tanzania sio Dar es salaam. Ajira zitaongezeka na kusambaa kwa sababu sasa patahitajika makundi 30 ya wawakilishi kwa kila Kampuni nchini kwenda katika mikoa 30 ya Tanzania. Kubwa zaidi, mikoa inayolala kwa kukosa kujua kuwepo kwa bidhaa na vifaa vya aina ambazo zinaweza kuwafanya waondokane na umaskini wao haitakaa ilale tena maana sabasaba kila mwaka itaizindua. Ndivyo inavyostahili pia kuwa kwa maonyesho ya nanenane. Yasiendelee kufanyika kisiasa bali yawe kweli ni maonyesho ya Expo-Kilimo International. Hali kadhalika mikoa nayo iwe na maonyesho yao kwa kadri ya uwezo, changamoto na matarajio yao.

Maonyesho yote haya yajikite kwanza na awali ya yote katika matatizo ya Watanzania, yawe ya kiuchumi, kijamii, kiutamaduni au kiteknolojia.

Kazi yake kubwa iwe ni kuoesha kipya kilichovumbuliwa na Watanzania na watu wengine ambacho kinaweza kuwa ufumbuzi wa tatizo au shida fulani. Kwa hiyo, miaka inavyokwenda matatizo ya Biashara, Kilimo na Viwanda yatakuwa yakipatiwa majibu yake katika maonyesho hayo.

Ni muhimu kwa maeneo kuwamakubwa zaidi na shughuli nzima iwe ni kivutio sio tu kwa wananchi wa kawaida, bali wawekezaji nawatalii pia. Hii iwe sawa na sherehe kubwa ya wiki nzima kitaifa ambako Watanzania watakuwa wakitafakari majibu ya matatizo yao na changamoto ambazo bado zinawakabili kuelekea kwenye dunia ya pili baada ya kugura ile ya kwanza.

Dhana nzima ya mashindano haya inapotezwa kwa kuangalia eti banda gani ni zuri na linalopendeza zaidi. Ninaamini wakati umefika kuvibadili vigezo vya ushindi na kuwachagua washindi kutokana na jinsi ambavyo banda husika limejitahidi kupata jibu sahihi kwa tatizo fulani linalowakabili Tanzania. Kwa mfano, bado tunanunua pampu za maji toka nje, je, zawadi si apewe aliyetengeneza pampu hiyo hapa nchini -iwe Mtanzania au mgeni!

Tuna tatizo la kupata zana za uchimbaji madini na hususan kwa wachimbaji wadogo, je, kwanini zawadi hiyo asipewe mtu atakayevumbua zana au mashine za kuchimba madini hapa nchini?

Tuna tatizo la uzalishaji na upatikanaji umeme, je, kwanini mzawadiwa asiwe ni Mtanzania au mgeni aliyekuja kuwekeza nchini na akaweza kuzalisha umeme kwa njia mbadala na umeme huo ukawa wa gharama nafuu zaidi.

Tuna matatizo ya kuzalisha magari, malori na mabasi yetu wenyewe kwanini zawadi zisiende kwa wale wa kwanza kabisa kutengeneza gari la Kitanzania hata kama teknolojia nzima itaazimwa au kuibwa nje?

Hivi atakayetengeneza trekta dogo la Kitanzania kwa kuazima teknolojia ya nje na ikawezekana trekta hilo kuuzwa kwa chini ya shilingi milioni mbili huyu si ndiye anayestahili kuwa mshindi kwenye Sabasaba Expo ijayo?

Watoto mashuleni hawana madeski, vitabu na vifaa vya kujifunzia vya kila aina. Je, kwanini zawadi wasipate wale watakaokuja na ufumbuzi wa matatizo hayo.

Mahospitali yetu yanafungwa na huduma kusimama kila kona nchini. Je, ushindani utakaofaa si ule wa utengenezaji wa zana na vifaa mbalimbali vya mahospitali hapa nchini ili viuzwe kwingineko kwa bei nafuu kuliko vinavyotoka nchi za nje? Maana, ukiwa na teknolojia duni katika hospitali au chuo ndivyo pia shule yenye inavyokuwa duni na ovyo kihali na kimazingira. Teknolojia ya kisasa inalazimisha usasa kwa kiwango cha juu ikiwemo usafi, mandhari na mazingira bora zaidi.

Mambo mengi yako ndani ya uwezo wetu. Kinachotakiwa ni kuona kwamba keki ya taifa inagawika kwa namna ambayo wajasiriamali na wazalishaji mali mbalimbali nao wanapata kitu cha uhakika ili kuleta mabadiliko tuliyokusudia nchini.

Nia na sababu ya kuwepo kwa maonyesho ya sabasaba ilikuwa ni kuiwezesha nchi kuwa na kipimamaendeleo kitakachoonesha jana tulikuwa wapi na leo tumefikia wapi. Lakini tukiwa mwaka nenda, mwaka rudi tunaonesha vilevile vya juzi basi kuna walakini mkubwa hapo. Utandawazi na makuzi ya teknolojia hayaturuhusu kuwa goigoi na wenda pole kiasi hicho.

Kiwanja kipya cha sabasaba lazima kiwe kikubwa kweli kiasi cha
kuwa na uwanja wa ndege mdogo, kituo cha treni, kituo cha basi, mabohari na vingine kama hivyo. Hili likifanyika foleni za kutisha zitakuwa historia maeneo ya Temeke. Na ili kuanza kutekeleza azma njema ya kutenga maeneo ya biashara na makazi ya wau au maofisi ni vyema kama uwanja wa Sabasaba hivi sasa utafanywa kuwa ni TEMEKE PUBLIC SHOPPING PLAZA AND SUPERMARKETS.

Uwanja mpya lazima uwe pia na hoteli ya hadhi ya kitalii kwa maana ya nyota 5 kwenda mbele. Uwanja wa golfu wa kisasa kabisa na vilevile uwanja wa mbio za langalanga (Formula 1) ili kutumika kwa uwanja huo mara kwa mara uwe ni kitu cha uhakika.

Wakati wa maonesho ni vyema uwanja huo ukawa na redio stesheni na TV ya maalum kwa ajili ya mawasiliano. Kwa upande mwingine kutakuwa na eneo la Tovuti au Intaneti ambako wafanyabiashara na wajasiriamali wa kila aina na rika watapata fursa ya kujifunza kufanya kazi zao kwa kutumia Teknohama.

Katika kufanya mabadiliko haya makubwa ni muhimu
kuwashirikisha watu wa nje kama Wajerumani, Wajapani na Wachina waliokubuhu katika mambo ya 'expo'.

Thursday, July 7, 2011

Kiswahili ndio ufunguo wa maendeleo yetu

TANZANIA miaka hamsini baada ya Uhuru ni motokaa mpya kimaendeleo ambayo mpaka leo bado linasukumwa kwa kuwa ufunguo wa kuliwasha gari hilo bado haujapatikana.

Ufunguo huo si mwingine ila ni kutaradadi kwa Kiswahili ili kitawale na kuendesha mambo yetu yote huku tukijua fika kwamba idadi ya Watanzania ambao hawatakuna wala kufanya biashara na wageni ili kuhitaji kutumia lugha nyingine ni zaidi ya asilimia 95.Kwa maneno mengine, ni asilimia tano tu au chini ya hapo ambao wanahitaji kujua lugha za kigeni.

Ili kuyakabili matatatizo au changamoto mbalimbali zinazokabili nchi na watu wetu ni lazima Kiswahili kituongoze na sio sisi tukiongoze Kiswahili. Waliojaribu kukionogza Kiswahili ili kituongoze ndio waliotufikisha hapa tulipo leo tofauti na watu wanaotumia lugha mama yao kuendeleza nchi zao.

Inaonekana jitihada za kuzibana lugha za Kienyeji nchini ili Kiswahili kitawale hazikuweza kutumika pia kuwa jibu kwa utandawazi kwa Kiswahili kutuongoza katika kukabiliana na changamoto hizo kwa sababu ya kulaghaiwa na wazungumzaji lugha ya kikoloni-Kiingereza.

Katika miaka hii ambayo nchi zinazozungumza Kiingereza zimeanza kushuka ngazi na zile zinazozungumza lugha nyingine ndio kwanza zinapanda juu na juu zaidi ni wakati muafaka wa kujiuliza kama ni sahihi kukubali kuhadaiwa na tafiti na fedha za misaada ili tuendelee kukiacha KIswahili kama lugha yatima.


ILI kusoma makala yote tuandikie SMS yenye e-mail yako: 0787-808539.

Wednesday, June 15, 2011

Tatizo sio Posho ni haki na usawa katika kugawana keki ya taifa....

SISHANGAI kwanini baadhi ya wabunge hawajagutukia mtego uliopo katika kashikashi ya posho iwepo au isiwepo. Kwa tunaojaribu kuangali mbali na kuona mbele tunatambua kwamba tatizo hapa sio POSHO bali ni ile hali ya umaskini wa kutisha aliyonayo Mtanzania wa kawaida.


Kwa bahati mbaya waheshimiwa wabunge wetu wanachokiona ni kutaka kuporwa na pengine na wale 'walioneemeka kwa njia nyingine' hata kile ambacho bado wao wanakiona ni kidogo.

Wale waliokwishazunguka mijini na vijijini baada ya kubaini kwamba wanaweza kutumia matatizo na dhiki mbalimbali za wananchi kama mtaji wa kisiasa hawajachelewa kufanya hivyo.
Na wale wanaokurupuka na majibu ya haraka haraka bila shaka watajikuta wanajiumbua wenyewe na kubaki wameshangaa ni kitu gani kinachoendelea.

Wenzetu wasingelikuwa wanasumbuliwa na ule ugonjwa niliowahi kuusilimisha kwa jina la 'ndivyotunavyofikir' wangekuwa wajanja kidogo tu, wangelitambua wanaowawakilisha wanauliza na wanataka majibu ya ni nini taifa hili linalovuna na kinachovunwa kinagawanywa vipi ?

Ni vigumu kuandika makala kama hii bila kuegemea upande wa walalahoi na wasiofaidika na mfumo uliopo lakini nitajaribu kutokupendelea upande wowote kwa mara ya kwanza.

Mlipuko wa mawasiliano rahisi kati ya mtu na mtu kupitia simu za mkononi, redio, televisheni, tovuti, blogi, twitter na facebook mijini na vijijini vinawaarifu wananchi mambo mengi kupita hata uwezo wao wa kuyatafakari na kuyachambua. Lakini, kila mmoja akihabarika kiasi cha kuanza kuuuliza je hicho kinachovunwa na taifa ni
nani anayekipata, yuko wapi hapa nchini, anakipata wakati gani, na kwanini anapata yeye na sio wengine ?

Dakika moja tu inatosha kwa mtoto wa mkulima kule kijijini kufahamu kutoka kwa mwanawe kwamba senti anazomtumia inabidi zipungue kwa sababu uwezo wake wa kifedha sasa umeterereka. Gharama mbalimbali zimepanda na wa kulaumiwa ni serikali na chama tawala. Kwa maneno mengine, kazi ya kuwaumbua, kuwasingizia, kuwapakazia na kulaumu viongozi na serikali imekuwa rahisi kufikishwa hadi kijijini -ambako watu kwa kawaida walikuwa wamelala na wasioamin kwamba serikali inaweza kuwa na nia mbaya na wanachi wake achilia mbali kuwafanyia ubaya huku ikijua inawafanyia ubaya.


Je, kuna usawa na haki katika kile kinachopatikana kwa maana wananchi wote wana fursa sawa, wako huru kukifanya au kuna wanaojichagua na kufaidi wao tu. Na kama kuna matatizo, je, kuna wanaoyashughulikia matatizo hayo kwa wakati na kwa manufaa ya jamii husika.
Au kila kiongozi toka ngazi ya chini hadi juu yuko 'bize' na mambo mengine lakini sio matatizo ya wananchi. Na je, wale wanaotumwa kwenda kuwawakilisha wananchi je wanafanya hivyo au wanawakilisha watu au taasisi nyingine ?


Je, mfumo na miundo ya kiuchumi na kijamii iliyopo inaonesha kuwa na uwezekano wa kuwapa wananchi fursa ya kutatua matatizo yao na kujiendeleza wao wenyewe bila kuhadaiwa na siasa au wanasiasa au watu wengine ?

Hii ni miaka ambayo wananchi watakuwa wanauliza maswali yaliyokuwa hayaulizwi sana huko nyuma. Mathalani, wanaweza kuuliza je, hao wanaopata kilicho kikubwa na zaidi ya wengine kutoka kwenye keki ya taifa wanastahili kupata wanachokipata. Au wanakipata kitu wasichokitolea jasho, yaani, wasichokistahili kwa uhalali kabisa, kwa maana kuwepo kwao ni mzigo tu kwa wananchi na watu hao hawasaidii wananchi kuapta unafuu wowote katika maisha yao ?

Yaani, wanaopata zaidi wanakula haramu na jasho la wananchi bue kwa kupata zaidi au wanapendelewa au wanajipendelea bila kuwa na sababu yoyote ya kuridhisha? Utakumbuka wale tulioikuwa tunasoma sekondari za kulala au hata za siku ambazo kuna chakaula cha mchana au jioni. Katika dhambi kubwa niliyowahi kujisikia ni ile ya kujimegea mimi binafsi wali mwingi na mboga nyingi kuliko wanafunzi wenzangu tuliokuwa tunakula kwenye meza moja. Nilifanya hivyo baada ya kuguswa na kosa nililolifanya. Nikaugawa tena wali wangu kwa kuwapunguzia wenzangu na mimi kubakiwa na kiasi kidogo kuliko wao. Kuanzia hapo, palikuwa hapana swali ni nani anastahili kugawa chakula katika meza yetu.

Swali dada na hili ni lile la nani wanaopata kidogo au wanaokosa kabisa ? Na kama kukosa kwao kunatokana na wao kuwa duni, wajinga, wavivu na wasiojituma kwa kiasi hicho au kwa kuwa wamezidiwa tu ujanja na uelewa na wale waliotangulia kupata mitaji na wanaowaongoza?

Kwanini wanakosa ? Kwanini hawatosheki, hawaridhiki na hawashibi kwa yale mazuri viongozi na wanasiasa wanayoamini tayari wamekwishawafanyia toka kuwepo kwao madarkaani?

Na je, mfumo mapokeo tuliourithi na tulio nao hadi leona uloanzia toka tukiwa na watu milioni 9 (1960) unafaa baada ya miaka 50 ambako tunakadiriwa kuwa watu milioni 50 ? Au kwa maneno mengine, kama Karl Marx alivyohoji, je, mahesabu yetu ya 'production' na 'reproduction' na 'redistribution' ya mapato ya taifa yapo sawa na sio yameachiwa huru mno kiasi ambacho tunachezea bomu la tofauti kubwa ya kipato kati ya walionacho na wasionacho?

Tanzania inafikisha miaka 50 ya Uhuru wa benderea ikiwa na tofauti kubwa kati ya mtu wa kipato cha chini na yule wa kipato cha juu pengine kwa uwiano wa 1: 10,000. Hii sio tu ni hatari bali ni aibu na fedheha kwa nchi ambayo Mungu na kiongozi wake wa mwanzo alishawaonyesha ubaya wa tofauti kubwa namna hii kati ya walionacho na wasio nacho.

Na kama Wahenga walivyosema,' Mwenye shibe, hamjui mwenye njaa', jambo hilo sasa, yaani walionacho kushindwa kujua kwanini kuna umasikini na kwanini watu hawana fedha mifukoni mwao na majumbani mwao, limefikia hadi kwenye ngazi za juu za uongozi wetu? Majemadari wanaotakiwa kuwatoa Watanzania toka kwenye umasikini hawajui upana, urefu na kina cha umasikini nchini mwao na miongoni mwa watu wao!!

Upo uwezekano mkubwa kwa nchi hii na viongozi kujiabisha kuhusu hali ya maisha ya Mtanzania kutokana na kulewa na sifa za viongozi wa nje na wale wanaowatumia kisiasa kwa faida zao wanazozijua wao wenyewe.

Katika kupanga tufanye nini wakati wa kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru tuwe waangalifu sana ili sherehe hizo zisiwe chanzo cha kujiaibisha na kujifedhehesha badala ya nafasi nzuri ya kurekebisha makosa yaliyopo na kuifanya siku hiyo siku ya kuzindua yale yatakayowapa wananchi matumaini na faraja.

Ni wakati muafaka kwa hiyo kuoanisha suala la 'posho ya wabunge' na lile la 'riziki ya kila siku ya mwananchi wa kawaida' na wawakilishi wetu kujiuliza kama hakuna uhusiano kati yake na hali halisi ya yule wanayemwakilisha bila kuzingatia dhiki na umaskini wake huko bungeni na kulipa hilo uzito unaostahili bila kuburuzwa na mtu au taasisi yoyote ambayo imeamua kufumbia macho jambo hili ?
Au kuna wanaowafunga macho kwa kitambaa cha khaki tena khaki nyeusi katika usiku mweusi wa hali halisi ya kiuchumi ya Mtanzania?

Je tunaweza kuongeza kinachovunwa? Kwa njia gani na mbinu zipi na mikakati ipi ya chapchapu ? Na hivi ukiwauliza Watanzania kwanini wao ni masikini na wewe una wajibu wa kuwatoa toka kwenye umaskini je, unawajibika kweli na je, unawatendea haki Watanzania masikini? Je, Taasisi ya Utafiti kuhusu umaskini hapa nchini imefikia wapi na yale ambayo imekwishayatafiti hadi wa leo yamefanyiwa kazi kiasi gani? Kwa maneno mengine, je, taasisi hiyo imekuwa na manufaa yaliyokusudiwa kwa Watanzania masikini au imewashibisha tu waliomo katika taasisi hiyo na nyingine kama hizo?

Na, je, ukiritimba katika masuala ya uongozi wa kijamii na uchumi ndio utakaotusaidia kutoka kwenye umasikini na matatizo yetu au tunaung'ang'ania tu kwa sababu ya mazoea na uoga wa kujaribu kilicho kipya?

Maana kuna wanaoamini kwamba serikali kuu inapswa kugawa madaraka ya maamuzi na utekelezaji sio tu kwa mikoa, wilaya, vyama vya kisiasa, mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali, makundi mbalimbali ya kijamii na watu mmoja mmoja kushiriki na kuchangia kikamilifu katika kuziona na kuzitumia fursa za kiuchumi na kijamii zilizopo nchini kuliko tulivyowahi kufanza huko siku za nyuma na vilevile kuyatafakari matatizo mbalimbali yanayowakabili Watanzania na kisha kuweka mkakati unaosadikisha kwamba 'utatuaji matatizo kila sekta, katika kila jamii' kila kona nchini ndiyo ajenda yetu ya kwanza kwa kila mpango tulionao na tutakaokuwa nao.
Tuiaminishe pia jamii yetu kwamba tukijipanga upya, kimkakati, kiakili na kwa hekina na busara zaidi tunaweza kupatia ufumbuzi sisi wenyewe matatizo na changamoto nyingi zinazotukabili.

Na pale msaada wa serikali, sekta binafsi na wasamaria wema inapohitajika inakuwa ni pale ambapo hatuna ujanja kwani kiakili, kiteknolojia na kirasilimali nyinginezo tumekwama na hatuna ujanja.

Nguvu na akili-jamii na ujasiriamali-kijamii ndio njia pekee ya kuinua ubora wa maisha ya Mtanzania.

Serikali yetu lazima ifike siku irudie maneno ya Mwalimu Nyerere kwamba, 'Serikali na Watanzania hatuna fedha. Na fedha na mtaji wetu ni akili, nguvu, maarifa, juhudi na bidii zetu wenyewe katika kutatua matatizo na changamoto mbalimbali zinazotukabili.'


Serikali ikiendelea kujifanya ndio bwana mkubwa, tajiri, ina mali, ina uwezo, ina nguvu na inaweza kila kitu na haishindwi na chochote lazima kuna siku tataibika na tutakwama.

Ninaamini ni Watanzania ndio wanaostahili kuwa BWANA MKUBWA, MATAJIRI, MFANO WA MUKTADIRI, KWA MAPENZI NA BARAKA ZA MWENYEZI MUNGU WANAWEZA KILA JAMBO, HAWASHINDWI NA LOLOTE na wingi, nguvu, matakwa na maslahi yao ndiyo yanayopasa kutawala na kuendesha nchi hii na sio vinginevyo. Demokrasia kwanza, mengine ni mazungumzo baada ya habari.

Tunaweza kumlaumu Mtanzania kuwa chanzo cha kukosa mahitaji yake ya msingi, maradhi, ujinga na umaskini wake lakini tusisahau kwamba upo uwezekano pia ikawa ni mundo na mifumo tuliyo nayo na ukiritimba wa serikali katika mipango, maamuzi na utekelezaji wake vikawa ndio sababu ya umasikini wa Mtanzania.

Katiba, wabunge na posho...

LABDA wabunge wanaotaka wasilipwe posho wameaona kile wanachokula hakilingani na kazi wanayowafanyia masikini wa Kitanzania katika jitihada zao za kutuondoa na umaskini, ujinga na maradhi.

Wametangulia Katiba katika kuleta mabadiliko ya kimsingi yanayohitajika, kwa maana ya kwamba, kipato cha kila kiongozi wa Kitanzania kwanza, kinatakiwa kinaoanishwa na mchango wake katika kupiga vita umaskini, ujinga na maradhi awali ya yote. Na kwa upande mwingine ipo haja kujenga miundo na mifumo inayomsaidia mwananchi kuondakana na umaskini badala ya miundo inayomwingiza mwananchi kwenye umaskini zaidi.

Wakati tunasubiri ujio wa Katiba mpya na namna itakayolishughulikia suala la keki ya taifa na inavyostahili kugawanywa kwa namna ambayo kila Mtanzania anakuwa na arri na motisha ya juu kuiondoa nchi hii kwenye daraja la tatu na umaskini mkubwa kwenda kwenye daraja la pili la kiuchumi kidunia lenye nafuu, utu na ubinadamu zaidi.

Saturday, June 11, 2011

Tofauti kati ya Uchumi-nchi na Uchumi-mtu

KUNA msemo ambao hudhalilisha sana matumizi ya takwimu katika taarifa mbalimbali unaosema kuna aina tatu za uongo (Ona kitabu cha Lies, Damn Lies and Statistics). Kuna uongo wa kawaida, halafu kuna uongo mweupeee na uongo wa tatu unaitwa TAKWIMU !

Katika kitabu hicho mwandishi anajaribu kuoensha kwamba uongo ulio mbaya na wa hatari zaidi ni takwimu kwa sababu wanaoziandaa takwimu huziandaa aghalabu kupotosha ukweli ulivyo; wanaozitangaza takwimu wanajua wanasema uongo lakini wanaamini katika uongo huo na wanaosikia uongo huo hawajui waamini lipi kati ya takwimu kadhaa zinazokuja kivyakevyake kila moja ikiwa na ajenda yake ya siri.

Uchumi-nchi ( Macroeconomics ) na uchumi-mtu ( Microeconomics) vyote huwasilishwa kinadharia katika takwimu zinazohusiana na maeneo husika. Mara nyingi sio rahisi kuchukua takwimu na hesabu za kila eneo kwa hiyo wakati mwingine watu huchagua kati ya maeneo kadhaa na kuwasilisha kile wanachoamini kinazungumza kwa faida ya wengine wote.

Ndio maana leo kuna Watanzania wanaoshindwa kuelewa na wanaoshangaa kwanini wakati nchi inaendelea kwa kasi kubwakutokana na takwimu zinazoonesha kuwa eti pato la Mtanzania sasa ni zaidi ya dola 500 kwa mwaka na kuwa pato la taifa linakuwa kwa asilimia sita kama sio zaidi ya hapo kuna Watanzania wasioliona hili na kulisifia na kuwasifia viongozi wao.

Ukiwauliza wataalamu wa uchumi kama sijakosea tatizo hili linaletwa na viongozi wetu kujikita zaidi katika masuala ya uchumi-nchi na kujisahau au kuwaachia wababaishaji kusimamia masuala ya uchumi-mtu.

Kwa tafsiri uchumi-nchi ni uchumi-jumla wa nchi ambao daima hutoa picha kubwa kiuchumi kwa nchi na hauangazii tu hali ya kiuchumi ya mtu mmoja mmoja. Japo chumi hizi mbili zinategemeana, zinaingiliana na kuoana sana lakini kila moja ina nafasi na wajibu wake katika jamii husika. Kwa upande mmoja, maendeleo ya nchi kiujumla huwa kivutio kwa wawekezaji, wabia wa kibiashara na kiuchumi na watalii na watu kama hao, wakati hilo halimpi sababu mwananchi mjini au kijijini kufarajika kwa sababu anaweza awe ananufaika na uchumi-nchi au kinyume cha hivyo.

Hali ilivyo kwa Tanzania ni asilimia ndogo sana ya Watanzania ndio wanaonufaika na takwimu na hali halisi ya uchumi-nchi . Hawa wanaonufaika ni pamoja na viongozi wa nchi wanaolipwa mishahara na marupurupu mazuri na wakati mwingine hawalipi kodi mbalimbali; wawekezaji na wafanyabiashara na wenye viwanda wanaoweza kuwabebesha walaji gharama zinazoongezeka katika biashara au viwanda vyao na hivyo kubakia pale pale kiuchumi hata kama mfumuko wa bei na gharama mbalimbali zimezidi kuongezeka mno katika kipindi kilichopita.

Wengine wanaonufaika na uchumi-nchi katika hali ambayo bei na mfumuko wa bei vimekuwa vikikuwa siku hadi siku ni wale waliomo katika mashirika ya kimatiafa, mashirika ya kiserikali na walanguzi wa kila aina na ukubwa.

Kwa hiyo uchumi-nchi unaoweza kuwa umekua au unakua lakini faida yote inaenda kwa wale wanaolipwa mishahara na marupurupu na posho nene, wawekezaji, wafanyabiashara, wenye viwanda, makampuni makubwa ya kitalii, waagizaji mafuta na peteroli, wenye viwanda, wafanyakazi wa mashirika ya kimataifa, wafuasi wa chama kinachotawala na watu kama hao tu na sio kwa Mtanzania wa kawaida.

Katika hali kama hii nchi inakuwa kama timu ambayo wachezaji fulani kwa kuitwa wachezaji nyota basi wanalipwa mamilioni ya fedha huku wachezaji wenzao wakipata chini ya nusu ya kile wenzao wanachokipata. Kimya kimya wachezaji walio wengi (asilimia 90) wanaamua kuwaachia wachezaji wanaolipwa vizuri sana ndani ya timu wacheze wenyewe na timu ishinde. Eti timu inaachiwa kucheza bila kucheza kama timu. Wote kwa kuitazama Real Madrid na Chelsea tunajua ni kitu gani kitakachotokea.

Ili nchi kama timu ishinde inahitaji zaidi ya viwango vya kukua uchumi, wawekezaji, mipango na bajeti za serikali. Nchi inahitaji kwanza, watu waamini kwamba wamo katika safari moja na sio kila mtu ana safari yake. Pili, lazima tuwe na visheni moja ya kule tuendako sio kila mtu awe na dira au ndoto binafsi ya kule anakotaka kwenda. Tatu, lazima tujenge uchumi wetu kama timu moja, kama kitu kimoja na sio kinyume cha hiyvo. Nne, lazima akilini mwetu sote tuwe na picha ya kile tunachotaka kukijenga kama vile mfano wa nyumba inayotakiwa kujengwa. Na mwisho lakini sio jambo dogo akili zetu ziione nchi nzima, mikoa, wilaya, tarafa, kata, miji, vijiji na mitaa kama MFUMO MMMOJA mkubwa ulio na mifumo kadhaa midogo midogo nayo yote ikiingiliana kila wakati na kwamba mfumo mdogo mmoja mdogo ukiwa na tatizo basi mifumo mingine yote midogo na huo mkubwa utakuwa katika matatizo pia. Na mfumo huo mkubwa itambulike pia ni sehemu ya mfumo mkubwa kabisa wa dunia na ulimwengu kiujumla ambao kwa sasa watambulika kama utandawazi. Nasi tukiwa na jukumu la kujipanga kwa namna ambayo kwayo tunanufaika badala ya kuathirika vibaya na huo utandawazi.

Tumewahi kuzungumzia huko nyuma kuwa mahitaji muhimu ya binadamu ni pamoja na maji, chakula, mahitaji ya kijamii, mavazi, makazi/nyumba, afya na tiba, elimu na usalama wa watu na mali zao. Vitu hivi ndivyo vinavyostahili kutumika kama kigezo cha kuamua uchumi umekua au haujakua katika medani ya uchumi-mtu na wala sio takwimu za aina nyingine.

Tuwaulize wanauchumi wetu kama Tanzania ya mwaka jana wa bejeti walikuwa na hali bora zaidi au mbaya zaidi katika suala la upatikanaji maji, chakula,mahiraji ya kijamii kama huduma mbalimbali za usafiri ikiwemo wa daladala, usafi na umeme ? Majibu ya hili pengine yatawafungua macho waliofunga macho na walio katika usingizi wa kuridhika na kutosheka na hali kama ilivyo.

Je, wanauchumi wetu walio huru nchini wanasema kwamba Watanzania wameacha kuvaa mitumba kama Mwinyi na Mkapa walivyotuacha au bado tunaendea na mtumba.

Je, hivi leo ni rahisi kujenga na kumiliki nyumba kama ilivyokuwa mwaka jana au hali imezidi kuwa mbaya zaidi. Jibu kwa hili nalo litatuonesha kama tuna sababu ya kukenua meno au ya kufunga vinywa kwa hasira ya ukata na kutokuridhika.

Wanauchumi wetu waambaje katika masuala ya afya na tiba na kama shida na dhiki za kina mama na watoto na wagonjwa wengine katika mahospitali yetu zimeisha au bado zinaendelea. Ziada ya ndogondogo ikiwa je, wale mbu wa Muhimbili wametushinda au tumewadhinda ? Kama mbu hao wametushinda nina mashaka kama tumepiga hatua yoyote mbele ya maana na inayoonekana.

Hali hii ya kuutazama uchumi kutoka juu na kushindwa kuutazama toka chini utaendelea kujenga msimamo na mtazamo wa wale walioko madarakani kujijali zaidi wao wenyewe kwanza na wale wanaowaweka madarakani na kamwe 'haiwezekani' wao kuwa na mipango na sera zinazotoka chini kwenda juu, yaani, kumneemesha kwanza mnyonge kisha ndio vigogo na vizito waneemeke zaidi ya walivyoneemeka. Na hiki ndio chanzo cha wao kuona kwa miwani yenye lensi kubwa uchumi-nchi na kutazamia uchumi-mtu kwa miwani yenye lensi ndogo.

Isitoshe uchumi wowote unaojengwa kwa kutegemea zaidi rasilimali na uwekezaji nyonyaji-sana toka nje hauwezi kamwe kuleta maendeleo linganifu ya uchumi-nchi na uchumi-mtu. Na hili benki ya dunia na IMF wameliona na wanalitambua na ndio maana wanaishauri serikali kupitia upya mikataba na wawekezaji katika sekta ya madini na migodi.

Aidha, nchi inayoshindwa kucheza na kuoanisha mahesabu na takwimu kwa nadharia na vitendo katika masuala ya pande-toaji/ugavi (supply) na pande-mahitaji (demand) katika ngazi ya uchumi-mtu haiwezi kamwe kuwa na maendeleo endelevu na ambayo huwa nadra kuguswa vibaya au kuathirika na kile kinachotokea ndani na nje ya nchi. Hili kama alivyosema Shaaban Robert linahitaji KIASI. Vigogo na vizito wakpata zaidi ya KIASI na walalahoi wakikosa chini ya KIASI basi inakuwa muhali na vigumu sana kujenga pia mtaji wa kijamii ambao hutegemea watu na sio fedha katika nchi husika.

Tunafanya kosa kubwa sana kiuchumi na hususan kibajeti kwa kukosa kuwa na mipango na mikakati adhimu ya kulifanya soko la ndani lifanye kazi kubwa linaloweza kuifanya kwa kujishughulisha zaidi na soko la nje, tena kwa upande wa manunuzi ya vitu vya anasa kwa sana.

Katika kipindi tulichomo na hali tuliyo nayo kiuchumi tulitakiwa tutumie muda mkubwa zaidi na fedha nyingi zaidi za kukuza uchumi-mtu kwanza na sio vinginevyo. Bajeti ya hivi majuzi haioneshi kuwa rafiki wa Malengo ya Milenia (MDGs) ukitazama mgawo wa bajeti ulivyokwenda. Na wala hakuna panapoonesha ni kwa namna na njia gani Tanzania katika kipindi cha bajeti kijacho itajitahidi kuhakikisha wananchi wake wanapata angalau sehemu ya kuridhisha ya mahitaji yao ya msingi. Pengine kwa viongozi kuamini kuwa kwa kuwa uchumi-nchi unakuwa basi watu wana fedha tele mifukoni mwao, kitu ambacho si kweli.

Friday, June 3, 2011

Taarab asili ni Urithi usiostahili kupotea

KWENYE miaka ya hivi karibuni kumekuwa na jitihada zenye mwelekeo potofu katika vyombo vya habari mbalimbali kupotosha maana na dhana halisi ya taarabu na kile ambacho taarabu inastahili kuwa na kuitwa.

Baada ya Watanzania kugeukawavivu wa kila kitu ikiwemo kupiga ala za muziki na kutaka mteremko katika kila jambo wale waliozuka na mitindo inayotumia mashairi au tungo zenye vina na mizani au isivyo hivyo wakaona urahisi ni kuita miziki yao 'modern taarab'. Miziki hiyo ninakaata sio taarabu bali inastahili kuitwa mipasho, kiduku, rusha na roho au mnanda na vitu kama hivyo lakini sio kamwe taarabu.

Muziki wa taarabu una asili na fasili yake katika watu wa pwani na visiwani na maeneo ya mwambao wa Afrika Mashariki.
Umeathirika kwa kiasi kikubwa na muziki wa Mashariki ya Kati, India na kaswida za Kiislamu.

Sifa moja kubwa ya muziki wa taarabu tofauti na wengi wanavyofikiri sio maneno na mpangilio wake, bali ala za muziki huo na mipangilio yake na ule ufundi wa kila mwanataarabu kuwa bingwa au stadi katika kupiga chombo fulani. Taarabu isipokuwa na ala hizi sio taarabu ni igizo tu kwa kiasi fulani la kitu kama taarabu. Taarab kwa kawaida ni kitulizo cha fikra ndani ya nyumba na katika hadhara isiyoshawishiwa na usasa na umagharibi kiasi cha kupuuza maadili na mila za wahusika.

Ala za taarabu ni nyingi na swahiba wangu Ali Salehe ambaye sio tu shabiki wa taarabu bali ni mtunzi pia wa nyimbo za taarab anaweza baadaye kunipokea hapa na kuelezea zaidi kwanini tunastahili kuwekeza kwenye taarab asilia kama eneo la utamaduni linalostahili kuhifadhiwa na kuenziwa.

Taarabu kama walivyoiendelza kina Siti binti Sadi, Bi Kidude, Juma Bhalo na kina Sheikh Ilyas, Machapurala bila kuwasahau mamia ya wanawake na wanaume wa Kizanzibar na Kimrima waliochangia maendeleo ya tasnia hii adimu lakini iliyo na sifa ya kuwa sehemu muhimu ya utamaduni wa mwambao ya Pwani ya Afrika Mashariki na usiostahili kuachiwa kupotea.

Taarabu ni muziki wa enzi na enzi. Ni sehemu ya utamaduni endelevu na hususan katika mikoa ya pwani ya Afrika Mashariki. Taarab ni ustaarabu, utaratibu, upole na uungwana. Taarabu ni kitulizo cha mawazo na gundi ya kuunganisha familia kama sio ukoo mzima. Sifa ambayo si mipasho, sio rusha roho sio mnanda unayo.

Taarab kiasili sio muziki wa kucheza bali wa kutazama, kusikiliza, kutafakari na kutunza. Huu ni muziki uliokuwa ukisikilizwa na watu wenye fikira, busara na hekima kuwapa muda wa kuwaza na kuwazua juu ya hili au lile. Muziki wa kupayuka, kujiona, msshauzi, kusemana, kutukanana, kuumbuana na wenye nyimbo ambazo hazina staha, usiri wala taadibu ya kuimbwa katika mafumbo hauwezi kuitwa taarab.

Ni muziki ambao kwa kawaida una ala takriban ya ishirini. Na kwa wapenzi halisi wa taarabu hufuatilia upigaji wa kila ala na ufundi au ugwiji wa yule anayetumia ala husika. Aidha, mashairi ya taarab hayaangalii tu mlingano wa vina na mizani bali maudhui na mantiki ya kile kilichomo tena kikiwe kwenye mafumbo kuweza kusomeka vyema na wanaosikiliza wimbo husika.

Ni muziki ambao hutungwa kwa mafumbo na kwa namna ambayo hauzui familia nzima, yaani, babu, bibi,baba,mama, kaka na dada wote kujumuika kwa pamoja bila kutokea chochote ambacho kinaweza kuwafanya washindwe kuzungumza au kutazamana. Taarab kiasili uliunga pamoja familia za wakazi wa mji husika. Tofauti na hiyo inayoitwa 'modern taarab' ambayo kwa kiasi kikubwa inazivunja familia katika kila mji na kijiji.

Siti bint Saad (1928) ndiye nyota wa kwanza wa taarab
ambaye kwa mara ya kwanza badala ya kuimba kwa Kiarabu aliimba kwa Kiswahili. Alifyatua mamia ya santuri za nyimbo India na wapenda muziki wa enzi hizo hakuna aliyekosa wimbo wake nyumbani.

Muziki wa taarab asili hauna tofauti na 'Classical Music' wa Ulaya au 'Country Music' wa Marekani. Miziki hiyo ilikuwepo, imekuwepo na itakuwepo bila kubadilika wala kuitwa kwa jina jingine wala kupigwa kwa namna nyingine tofauti na ilivyokuwa, ilivyo sasa na itakavyokuwa kesho.
Ni sehemu ya kudumu ya utamduni wa watu na sio kitu cha kupita na kusahaulika.

Aina hizo za miziki pamoja na kuzuka kwa miziki ya kila aina Ulaya na Marekani bado inatambulika kwa nembo na jina lake. Country ni country na classical ni classical. Hapajakuwepo muziki mwingine uliopewa umodern kuhusiana na miziki hii, hakuna kitu kama modern country au modern classic.

Rouget katika Music and Trance anafafanua kwamba neno taarab linatokana na neno la kiarabu 'tariba' likiwa na maana ya hisia za kusisimka, kudhihirisha au kutaka kufanya kitu fulani kama vile kuimba au kucheza taarab.

Taarab asili ilingia kwanza hapa Afrika Mashariki kupitia Zanzibar kunako miaka ya 1870. Aliileta Sultan Seyyid Barghash ambaye alileta kikundi cha wanamzuki toka Misri kukaa kwenye jumba lake la Kifalme.

Tofauti na viongozi wetu wa leo, Barghash aliwapeleka Wazanzibari kadhaa wakiongozwa na IbrahimMohammed kwenda kusomea muzki nchini Misri nao waliporudi waliunda kikundi cha kwanza pengine cha taarabu Afrika Mashariki kilichoitwa Zanzibar Taarab Orchestra.

Kunako 1905 kikundi cha pili cha taarabu kilizaliwa huko huko Unguja kikiitwa Ikwhani Safaa Musical Club. Kikundi hicho kipo hadi wa leo, lakini kama vilivyo vikundi vingine vya taarab 'hasa' havina msaada wowote wa maana toka kwa yeyote yule, kwani inavyoelekea wengi pamoja na viongozi wa serikali wametekwa na rusharoho na mipasho.

Taarab asili haistahili kuonekana kama ni taarab tu. Ni zaidi ya taarab. Hii ni hazina ya utamaduni katika mwambao wa Afrika Mashariki kuanzisa Lamu hadi Kilwa na Sofala.


Kama jitihada zinavyofanyika kukarabati na kutunza maeneo kama vile Mji Mkongwe Zanzibar, Bagamoyo na Kilwa ili iendelee kuwepo basi upo umuhimu pia wa wanaohusika katika serikali zetu kuhakikisha kuwa muziki wa taarab asili na wanamuziki wake wanakumbukwa na kuenziwa na kisha kizazi kipya kinajengwa ili kuendeleza muziki huu kwa faida ya vizazi vijavyo. Kwa maana, ukweli ni kwamba taarab asili ikipotea ndio utakuwa mwisho wa taarab hapa Afrika Mashariki.

Kwanini tuhifadhi taarab asilia

Kwa bahati mbaya wengi tumezoea kuchukulia vitu kama ardhi, fedha, nyumba, magari kuwa ndio rasilimali tu. Lakini muziki wa kiasili nao ni rasilimali muhimu kimaendeleo na kisaikolojia. Bila urithi wa namna hii tutakuwa ni taifa lipolipo tu ambalo si jambo zuri.

Pamoja na mambo mengine kuifufua, kuitunza na kuiendelza taarab asili ni jambo lenye faida kadhaa ikiwemo kuendeleza mila na utamaduni wetu; kuzileta familia pamoja mara kwa mara; kujenga maadili bora katika jamii; kuwa na muziki usioendana kinyume na maadili ya dini; kukuza na kuendeleza ushairi na Kiswahili; kuwa kivutio kwa wageni wa leo na kesho
na kuzienzi na kuendeleza ala asili za muziki na upigaji wake.

Ninatoa wito maalum pia kwa vyombo vya habari kuacha kuuchanganya umma juu ya muziki wa taarab. Tafadhali Bi Hindu, Dida, Mzee Chapuo, Bi Chau, Miriam wa Migomba, Kristina wa Mbezi kwa kuturahisisishia hili kwa kubaini kwamba Afrika Mashariki kuna taarab moja tu, nayo ni taarab asilia ambayo kwa kawaida hupigwa na vyombo vingi, hutumia mafumbo na usiri katika nyimbo zake na hauchezwi achilia mbali kunenguliwa na kutingishiwa mawowowo.

Miziki inayojiita modern taarab iitwe kwa majina yao yanayostahili kama ni kiduku basi kiduku, kama ni rusha roho basi rusha roho fulani, kama ni mipasho basi ni mipasho na kama ni mnanda uitwe mnanda
na miziki hii isiruhusiwe kutumia mgongo wa taarab kujijenga isipostahili.

Nikiri kuwa nilitaka sana nitembelee Lamu, Malindi, Mombasa, Tanga na Zanzibar kuzungumza na wakereketwa wenzangu wa taarabu asili kabla ya kuandika makala haya lakini haikuwezekana. Ninaamini, hata hivyo kupitia makala haya ujumbe unaweza kufika kwa kiasi fulani.

Ninawashauri wanaharakati wa kulinda na kuendeleza utamaduni wetu kuangalia uwezekano wa haya yafuatayo: Kusaidia juhudi binafsi zilizopo za kufufua na kuendeleza vikundi vya taarabu kupitia vilabu na vyuo vya upigaji ala za asili za taarab (mathalani juhudi za Bi Hamndani, Zanzibar) ; Kushirikiana na UNESCO kuhifadhi taarab asili kwa kutumia TEKNOHAMA;
Kuwatafuta wanataarab asil waliko na kuwaunganisha ili kuufufua na kuchochea kuwepo kwa muziki huo kiasili na kuongeza vionjo viwili vitatu vya kuvutia familia zaidi kuliko mtu mmoja mmoja.

Aidha, kusaidia vikundi vilivyopo lakini havina ala za kutosha za muziki toka Misri na Uarabuni; kuenzi Ushairi katika vyombo vya habari kukuza vipaji vya washairi chipukizi na
kuchukulia Taarab asili kama urithi usiostahili kupotea kwa msaada wa UNESCO na wapenda utamaduni wetu wengineo.


http://www.gmail.com
sammy.i.makilla@gmail.com