Friday, September 16, 2011

Mikopo kwa wanafunzi na matumizi ya kadi za krediti

NIMEKUWA nikifuatilia sakata la mikopo kwa wanafunzi hapa nchini kwa muda sasa.
Majumuisho yangu yasiyo rasmi ni pamoja na kwamba taasisi iliyopo, muundo uliyo nayo, mifumo iliyopo, mipango iliyopo, taratibu zinazofuatwa-vyote vimeanzishwa kwa makosa na visingestahili kuwepo.

Serikali iliyopo madarakani kwa sababu ambazo inazijua yenyewe ilianzisha bodi ya mikopo ili isaidie kitu kingine lakini sio kuwasaidia wanafunzi wanaohitaji mikopo.

Wimbo wa serikali inatakiwa kujitoa kwenye masuala ya uchumi na biashara uliishia katikati, maana ulistahili kuendelea kwa kubainisha pia serikali inatakiwa kujitoa kwenye masuala yote ya kifedha na mikopo isiyoihusu serikali moja kwa moja.

Kinachoendelea hivi sasa ni kwamba serikali imejiingiza katika sekta ya Benki na mikopo bila kuwa na uwezo, vifaa, rasilimali watu,utaalamu wa kuendesha kwa makini na kibiashara na kwa faida shughuli ya mikopo kwa wanafunzi nchini. Upo uwezekano mkubwa kwamba hapo baadaye serikali italazimika kufuta mikopo yote vitabuni mwake kwani itakuwa ni mikopo mibovu.

Waliostahili kuifanya kazi hii walistahili kuwa benki mbalimbali nchini kwa ushirikiano na Mamlaka ya Kodi nchini (TRA), chama cha Waajiri nchini (ATE), chama kikuu cha wafanyakazi nchini (TFTU), mashirika ya hifadhi ya wafanyakazi mbalimbali nchini, makampuni mbalimbali ya bima nchini na waajiri waliopo na waajiri tarajiwa nchini.

Kilichotakiwa kufanyika ili serikali isijiingize katika matatizo, ili wajanja wachache wasitumie mwanya huo kujinufaisha wao wenyewe na jamaa zao na hali kadhalika wanafunzi na wazazi wao wasisumbuke ilikuwa ni kuvipa dhima vyombo hivyo kuanzisha KADI YA KREDITI kwa wanafunzi mbalimbali watarajiwa kwa namna ambayo ingelipunguza urasimu; umangimeza; kujuana, yaani, huyu mtoto wa nani na yule wa nani; ubabaishaji; usumbufu; matumizi ya fomu na makaratasi ambayo ni rahisi kupotea na wakati huo huo kuwezesha kuwaingiza wakopaji katika mifumo ya kompyuta ya serikali, benki husika, taasisi mbalimbali ikiwemo TRA na Mkaguzi Mkuu wa serikali na mkaguzi wa mikopo ya wanafunzi (kama yupo) kwa sababu za kiudhibiti na ufuatiliaji kuanzia mkopo unapochukuliwa hadi unapolipwa.

Nitatoa mfano,CRDB Benki kwa ruksa ya serikali inanunua dhamana za serikali (government bonds au treasury bills) toka hazina kwa kiasi cha mikopo inayohitajika na wanafunzi. Bila kubagua wanafunzi wote wanaoingia kwenye vyuo vya juu wanapewa krediti kadi ya CRDB Bank toka kitengo cha Mikopo Maalum kwa Wanafunzi kitakachokuwa kinajitegemea ndani ya benki hiyo. Ikumbukwe hii ni benki pekee ya wazawa nchi ambayo tunastahili kuibeba kwa hali na mali.

Benki hii kwa kushirikiana na taasisi husika haitafanya kazi hii bure. Italipwa. Na malipo yenyewe yatatokana na kuendesha shughuli nzima ya mikopo kwa wanafunzi kibiasharra kati ya benki na serikali kwa upande mmoja; na kwa upande wa pili kama huduma kati yake na wanafunzi wa vyuo vya juu waliopo na watarajiwa.

Kwa maneno mengine nia ya serikali kutoa huduma ya mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vya juu itatimia kwa benki hiyo kuisaidia serikali katika jukumu lake.

Na kwa upande mwingine benki na taasisi ya fedha husika kwa kukabidhiwa kazi hiyo na kulipwa na serikali itakuwa imerejeshewa kufanya kile ambacho kwa kweli ndiyo kazi zake za kila siku. Wote kwa namna hii wataibuka ni washindi, ingawa serikali itakuwa mshindi zaidi kwa maana sasa itaondokana na aibu ya kuzodolewa kila siku na wazazi na wanafunzi kuhusu suala hili la mikopo kwa wanafunzi.
Benki tofauti na serikali kwa kiasi fulani, itakuwa na kumbukumbu zote za kila mkopo inayouhudumia na mkopaji na jinsi ya kumfuatilia toka mwanzo mpaka mwisho.

Kwa kushirikiana na TRA, mkaguzi mkuu wa serikali na mkaguzi wa elimu ya juu, benki itawatambua wanaostahili kukopa na wasiostahili kukopa. Wasiostahili kukopa watabebeshwa riba kubwa zaidi na muda wao kulipa kuwa mfupi zaidi, na wanaostahili kukopa riba ndogo na kupewa muda mrefu zaidi kulipa deni lao.

Jukumu la kuhudumia mkopo huo sasa halitakuwa tena la serikali bali la mwanafunzi na mzazi wake au mlezi wake wakishirikiana na benki husika. Akili au mkono mtu katika suala zima utakuwa na fursa ndogo sana ya kuharibu nia hii nzuri ya serikali kwa watu wake.

Kwa wasiojua, kadi ya krediti ni kadi kama ilivyo Tembo Card ya CRDB Bank au nyinginezo kama hii ambayo badala ya kuwa na fedha za mwenye kadi, ni benki husika inayomwekea kiwango fulani cha fedha anazoweza kutumia kama mkopo kwa shughuli zake binafsi ili mradi tu havuki ukomo aliowekewa (maana kadi yenyewe haitamruhusu kufanza hivyo). Kama zilivyo kadi nyingine kadi hii ya krediti inaweka kumbukumbu zote muhimu kwa njia ya kistaarabu na kwa namna ambayo sio rahisi kumbukumbu hizo kupotea. Kadi ya krediti itamruhusu mwanafunzi kulipia tuisheni au gharama za mafunzo; vitabu; mitihani; malazi; chakula; afya na tiba; usafiri; utafiti; mafunzo kwa vitendo na majukumu mengine mbalimbali ya kiuanafunzi.

Ili kuwawezesha wanafunzi kutumia vyema na ipasavyo hizi Kadi za Krediti CRDB Benki itaendesha mafunzo kwa kushirikiana na wahusika wengine kwa wanafunzi/ wakopaji wote. Baada ya hapo itakuwa ni mtihani kwa mtumiaji mwenyewe kuitumia kadi hiyo ya krediti kwa namna ambayo itampunguzia deni laki huko baadaye na hata kumnufaisha wakati wa masomo kwa kumuwezesha kuwa mjasiriamali na mtu anayejiajiri hata kabla hajamaliza chuo.

Wahisani au wafadhili wanaweza kukaribishwa ili wachangie kupunguza gharama za mikopo hiyo na kuwawezesha wanafunzi wanaostahili kukopa kutokulipa riba yoyote.

Katika miaka hii ni rahisi sana kuwa na viongozi ambao uwezo wao wa uamuzi, uchambuzi, uchaguzi, uteuzi na utekelezaji sahili na sahihi ni dhaifu kuliko wa baadhi ya wale wanaowaongoza. Kwa hiyo ni muhimu pale inapoonekana katika jambo au kazi fulani ambayo inawahusu raia walio wengi kujitokeza kwa viongozi zaidi ya viongozi ili kurekebisha mambo.

Mipango, utaratibu na utekelezaji mzima wa suala la mikopo kwa wanafunzi sio tu vinaonesha walakini mkubwa lakini kunaashiria dhuluma, ujanja, kutorejeshwa kabisa mikopo na matatizo yasiyo na mwisho. Ni kwa sababu hii ndio maana ninapendekeza kwamba shirika la Hakielimu liingilie kati ili kubadili mustakabali wa jambo lenyewe. Hata kama tumeanza vibaya jambo lililo muhimu zaidi ni kumaliza jambo lenyewe kwa kupatikana haki kwa wale wote wanaostahili haki, ikiwemo jamii ya walipa kodi nchini.

Hakielimu inaweza kuingilia kati kwa kujitolea kuanzisha kazi ya kuundwa makundi mbalimbali ya washikadau katika elimu na kisha kuwasapoti katika kurasimisha uundwaji na kuwepo kwa makundi hayo na pia mikutano yao ya awali.

Mathalni, tuna maprofesa na walimu wastaafu wengi tu ambao wakiwezeshwa wanaweza kuzungumzia mengi mazuri tu kuhusu utekelezaji wa masuala mbalimbali ya elimu hapa nchini kwa sekta ya umma na sekta binafsi. Makundi mengine ni pamoja na mainspekta wastaafu wa elimu, washauri na watafiti katika masuala ya elimu na mafunzo, waandishi wa masuala ya elimu na mafunzo, wakuu wa vyuo na walimu wakuu wastaafu; watumishi wa wizara ya elimu wastaafu; viongozi katika vyuo vikuu, vyuo vya kawaida, shule za sekondari, shule za msingi na wamiliki wa shule na vyuo mbalimbali.

Maamuzi mengi ambayo yanaishia kuwa bomu kwa kufanywa kidikteta na kwa maslahi ya watu au taasisi fulani sasa yatapatiwa changamoto na haitakuwa rahisi siku za mbele kuwa na maamuzi mengi mabovu katika elimu na taasisi za elimu kama ilivyo sasa.

Hasara za mfumo uliopo hivi sasa ni pamoja na: kuwepo urasimu na umangimeza unaoharibu zaidi ya kutengeneza; dhuluma na upendeleo katika utoaji mkopo; kuiongezea serikali gharama za uendeshaji na utoaji mikopo; unadra wa mikopo kulipwa kwa wakati; kutokuwepo mbeba dhamnana inayotolewa a serikali; kuzinyima benki na taasisi za fedha fursa za kiuchumi inazostahili; kuwa na watu wanaoajiriwa na kulipwa mishahara bila sababu ya msingi; kufedheheka serikali mbele ya macho ya wannanchi wake na dunia nzima; kuruhusu kulipwa mikopo wasiostahili na wanaostahili kutokulipwa na kadhalika.


Faida za kadi za krediti ni pamoja na kuondoa: matatizo yanayoletwa na akili na mkono wa binadamu; kuondoa urasimu; ;kuondoa upendeleo na dhuluma; kurahisisha zoezi zima la kukopa na kulipa mkopo; kudhibti wadaiwa na malipo husika; kukuza uchumi kwa kuongeza mzunguko wa fedha; kuhamisha jukumu la kujisimamia kifedha kwa wazazi na wanafunzi wenyewe; kuondoa gharama kwa kuwepo na taasisi na majengo maalum kwa shughuli hiyo na kuongeza haki na usawa katika medani ya maisha ya kitaifa nchini.

Uwekezaji kaika kilimo unufaishe vijiji na wanavijiji

Kuna kosa la kihistoria ambalo lilikwishatokea na linaloendelea kutokea kwa sababu serikali imeshindwa hadi wa leo kufanya tathmini halisi, halali na ya haki ya watu na utamaduni wao, mtaji wao wa kijamii, vijiji vyao na ardhi na mali asili walizonazo.

Aidha serikali imepindua kinyemela madaraka na mamlaka ya wananchi wanayostahili kuwa nayo kwa mujibu wa katiba juu ya uongozi na maamuzi ya nchi, ardhi na mali asili zao na kujiweka juu kwenye nafasi ya muamuzi mkuu na mmiliki wa ardhi badala ya wananchi kuwa ndio wanaofanya maamuzi na wanaomiliki kihalali ardhi na rasilimali nyinginezo katika nchi hii, kiasi kwamba serikali inaweza kuamua wakati wowote kuwapora wananchi ardhi yao na wananchi walipwe kidunchu tu au sawa na kutokulipwa na wakati mwingine hata kuporwa kimaguvu ardhi na mali asili zao nyingine na wale wanaoitwa wawakilishi wa serikali.

Isitoshe, ardhi na sekta ya kilimo ndiyo inayowagusa wananchi walio wengi Tanzania na maamuzi katika eneo hili ni lazima yawe na manufaa kwa wanavijiji walio wengi na sio wanamji na wawekezaji wawili watatu wa ndani na nje.

Kihistoria, haikanushiki pia kwamba japo katiba ya nchi hii inataka uwiano na ulinganifu katika maendeleo, hali llivyo leo ni kwamba bado watu wa mjini na sehemu za mijini zimekuwa zikipewa upendeleo mkubwa kuliko watu wa vijijini na maeneo ya vijijini. Uvumilivu, subira na ukawaida wa watu wa vijijini umechangia sana katika hili pengine kwa wao kuonekana wanaoridhika kirahisi au mabwege wasioweza kuwafanya wakubwa lolote. Lakini kuendelea na hali hii sio tu ni dhuluma na uonevu kwa watu wa
vijijini bali ni kukosa kuona mbali na mbele na kuamini kuwa siku zote watu wa vijijini watakuwa wavumilivu, wenye subira na mabwege na mafala kuhusu haki zao, matakwa na matarajio yao.

Hali kadhalika, matatizo mengi yanayotokea katika miji yetu hapa nchini hivi leo yanasababishwa na upendeleo huu wa miji dhidi ya vijiji iwe ni katika wingi wa watu wasiobebeka mjini, wizi, wingi wa magari na foleni, kukosekana huduma muhimu mijini na kadhalika.

Ndio maana tunasema kwamba bila ya sera ya Kilimo Kwanza na Uwekezaji katika kilimo kumnufaisha moja kwa moja mwanakijiji basi mapinduzi ya kilimo nchini yatakuwa ni sawa na kazi ya kupanda kilima kirefu chenye majabali yenye ncha kali na mijoka iliyojificha.

Katika siku za hivi karibuni kilimo kwanza ambayo ni sera iliyoanza siku nyingi lakini imeendelea kubadilishwa majina kama vile yapo matarajio yasiyokufa kwamba eti jina ndilo linaloweza kuifanya ifanikiwe imekuwa ikipigia debe nchi za nje kupewa ardhi ya Watanzania kwa ajili ya kilimo kama vile hakuna Watanzania wanaoweza kuingia kwenye ubia na wawekezaji toka nje kwa faida ya pande zote zinazohusika.
Nchi zinazozungumziwa sana ni ile ya Korea Kusini, Iran, Uturuki na zile za Kiarabu.

NInaamini kuzipa nchi hizi za nje ardhi ya Watanzania moja kwa moja kama vile ardhi hiyo haina wamiliki wake wa asili na haina thamani yoyote na Watanzania wahusika hawastahili wao wenyewe kufanya maamuzi juu ya ardhi yao ni kukiuka katiba na kwamba mamlaka na madaraka juu ya maamuzi ya matumizi ya rasilimali za nchi hii inayo wananchi wenyewe na serikali ni watendaji na watekelezaji wa maamuzi ya wananchi na sio vinginevyo. Kwa kila hali serikali na viongozi wake wamepituka uwezo ambao tumekasimu kwao.

Kutokujua au ujinga wa wananchi kuhusu haki zao katika ardhi, sio tu kiumilikaji na kiunufaikaji, ila katika kubwa zaidi kwamba wao ndio wanaostahili kuwa wamiliki wa rasilimali zao na maamuzi yote juu ya matumizi ya ardhi yanastahili kufanywa na jamii zao ndiko kulikochangia wajanja wachache kujinufaisha kwa kuwatumikia wakuu wa mikoa na wilaya sio tu kujimegea ardhi katika maeneo wasiyo na nasaba au ukuruba nayo, bali pia kuwauzia wawekezaji wao wakanufaika na wananchi wakaendelea kuwa maskini japo rasilimali yao imeuzwa na walistahili kunufaika na mauzo hayo.

Hakuna anayepinga nchi, kampuni na watu kutoka nje kuwekeza katika kilimo nchini. Tunachokipinga ni uwekezaji unaofanywa kwa namna ambayo kilimo vijijini mwetu na wakulima katika vijiji vyetu hawatasaidiwa kubadilika kitu na uwekezaji kama huo.

Uwekezaji tunaostahili kuupigia debe ni ule ambao nchi fulani duniani au kampuni fulani au mtu fulani anayekuja kuwekeza Tanzania ANAINGIA UBIA na mojawapo ya vijiji vyetu ili kuitumia ardhi ya kijiji kulima, kufuga, kuvua au kufanza mradi wowote ule huku wananchi wa kijiji husika na mwekezaji mwenyewe wakivuna na kugawana kinachopatikana kwa namna watakayokubaliana wenyewe kwa manufaa ya wote.

Kwa mtaji huu mwanakijiji atakuwa sio tu na soko la nguvu kazi yake; bali pia atanufaika na soko la nje, elimu, ujuzi na teknolojia atakayoleta mwekezaji huku wakizalisha mali ambayo itachangia kunyanyua hali ya maisha ya wanavijiji wahusika na kipato cha mwekezaji na nchi kadhalika.

Kabla ya nchi- wawekezaji kuruhusiwa kuwekeza katika kilimo hapa nchini ni muhimu benki ya wakulima iwe tayari imeanzishwa. Fedha zinazolipwa na nchi, kampuni na watu wanaowekeza katika kilimo zitawekwa katika benki hii zikigawanywa katika mafungu ya hisa za mwekezaji na kiasi fulani kutumika kuendeleza miundo mbinu na huduma muhimu vijijini na sio vinginevyo. Tathmini halali, halisi na haki ya thamani ya mtaji watu wa kijiji husika, utamaduni na urithi wao, ardhi yao, misitu yao na mali asili zao nyingine ikishafanyika Benki ya Wakulima itatoa hati ya uwekezaji au mkopo inayolingana na thamani ya rasilimali za kijiji. Thamani hii itakayokuwa katika shilingi ya Kitanzania itakuwa ni sehemu ya uwekezaji wa kijiji husika wenye thamani sawa na fedha zilizochangwa na mwekezaji katika kijiji chao.

Tunapaswa kukubali kuwa hii ndiyo njia pekee ya vijiji vyetu kulala maskini na kuamka matajiri kesho yake. Na kwamba serikali inawjibika kuwezesha na kurahisisha hili, kwani haina namna yoyote nyingine inayoweza kuondoa tofauti kati ya vijiji na miji na kupunguza matatizo ya miji yanayotokana na kusahaulika kimaendeleo kwa vijiji ila tu kwa mkakati na mbinu hii. Katika muktadha uliopo ni muhimu viongozi wetu wabadilike kimawazo ili nchi iweze kuendelea kijamii na kiuchumi. Mustakabali wa ustawi na mafanikio ya vijiji vyetu unategemea hili kuliko kitu kingine chochote duniani.

Hakuna kiongozi wa zamani au leo binafsi ambaye kwa kuwekeza mwenyewe katika kilimo na ufugaji anaweza akatutoa kutoka kwenye dunia ya tatu na kutupandisha hadi ya pili. Ni pale wakulima wote kwa pamoja wanapopewa fursa hii ndio hili litakuwa na nafasi angalau ya kuwezekana.

Sera za MKUKUTA wa I na wa II zimeshindwa kuchangia cha maana katika kuondoa umaskini wa Mtanzania kwa sababu hazikufanikiwa kuainisha kwa usahihi chanzo cha umaskini wetu. Na chanzo hicho sio kingine ila ardhi na mali asili nyingine za Tanzania kutokuwa na thamani halisi, halali na ya haki kiasi cha kuwanufaisha Watanzania kupitia umilikaji wao katika harakati zao za kujikomboa kiuchumi.
Bila umiliki huu, maamuzi na usimamizi wa ardhi na mali asili za wanajamii kufanywa na wananchi wenyewe rasmi haitakuwa rahisi nchi yetu kuondokana na umaskini wa kutupwa kwa walio wengi.

Tathmini ya haki, halisi na halali ikifanyika watu, urithi na utamaduni wao, vijiji vyao, maliasili zao, ardhi na rutuba yake, uoto, maji na ujumla wa mtaji wao wa kijamii ni vitu vyenye thamani sawa na fedha, mashine na mitambo yote itakayoletwa na mwekezaji yoyote yule.

Hii ina maana kwamba vijiji vyetu na jamii zake vina kitu cha thamani au rasilimali ya kuwekeza bila kutoa senti hata moja mfukoni mwao.

Ili kusahihisha kosa hilo la kihistoria hapo juu ninashauri kwamba sio vyema nchi, makampuni na watu kutoka nje kupewa ardhi ya Watanzania moja kwa moja bila ushirikishwaji na ubia wa vijiji na wanavijiji katika uzalishaji na uuzwaji na unufaikaji wa mazao husika.

Ni wataalamu wa tathmini ya mambo husika na sio wanasiasa wanaostahili kuamua kwamba kijiji na wanakijiji fulani kwa ujumla wao wana mali za thamani ya kiasi gani na muwekezaji akishawekeza mgawa wa mapato kutokana na shughuli za kilimo zitakazoendeshwa utakuwa vipi?

Saturday, September 10, 2011

Maafa yakishatokea ndipo tunapopata akili

USAFIRI na UCHUKUZI Tanzania uwe wa barabarani, angani au majini umezungukwa na kila aina ya mapungufu na kukosa ukaguzi na udhibiti wa kutosha.

Aghalabu tunakuwa na akili pale balaa linapotokea na roho zinapopotea. Wakubwa na mamlaka zao wamekaa zaidi mkao wa kufurahia ukubwa na vyeo vyao na wala sio kutekeleza kile ukubwa au cheo husika kinachowataka kutekeleza. Na hakuna anayewasema wala kuwachukulia hatua, maana pengine na wakubwa nao wamekaa mkao huohuo.


Maafa kama yaliyotokea mkondo wa Nungwi ni kitu kilichokuwa kikisubiriwa tu kitoke na Mungu aepushilie mbali yapo mengine kama hayo yanayotusubiri kwenye maziwa na bahari zetu, barabarani na angani kama tusipozinduka na kuanza kudhibiti kila kazi inayogusa maisha ya watu hapa nchini, ili kuwe na uhakika na usalama wa maisha ya watu na mali zao.

Ilivyo hivi leo ni kwamba mtu akiwa na fedha au cheo anaweza akafanya lolote hata kama kwa kufanya analolifanya anahatarisha maisha ya maelfu ya Watanzania wasio na kosa. Na sheria zilizopo ni sheria bibi au sheria nyanya ambazo hazimsaidii mzawa kwa lolote zaidi ya mamba kumwaga machozi yao na huruma za kisiasa ili watu wahurumiwe kwa kuonekana wana huruma wakati huruma yao ilikuwa inatakiwa ionekane kwa kuona mbali na mbele, kupanga na tathadhari kuchukuliwa kabla ya janga husika. Ambayo hii kwa hakika ndiyo kazi ya uongozi, yaani, kazi ya uongozi ni kuona mbali na mbele na kuwaepusha wananchi na matatizo yanayoweza kutokea aidha kutokana na uzembe wa watu au amri ya Mwenyezi Mungu.

Hakuna tume itakayoundwa na ikamsaidia mtu yeyote kama serikali na waendeshaji wake wasipojichunguza na kuangalia utendaji wao na kwa kiasi gani unakidhi changamoto za usalama na ulinzi wa raia na mali zao.

Wataalamu wanadhihirisha Watanzania ni wazuri sana kwa mipango na kupanga lakini ni wabovu katika utekelezaji wa kila jambo kwa sababu udhibiti, ukaguzi na ufuatiliaji mambo husika haupo au upo kwa kiwango cha chini sana.

Ieleweke kwamba, hatumlaumu yeyote kwa sasa lakini tukubaliane kwamba 'uswahili', yaani, ubabaishaji au kufanya kazi tu mkubwa anapokuwepo au kwa kubebembelezwa, au kule kufanya mambo kama vile mtu hutaki au kuamini kwamba kitakachotokea ni amri ya Mungu na huwezi kukizuia, sio tu utatugharimu maisha na mali nyingi sisi wenyewe bali utawafukuza pia watalii na wawekezaji watakapoona umezidi na hauvumiliki. Ni lazima tubadilike.

Ingelifaa sote, pamoja na tume husika tujiulize maswali yafuatayo:

.Je ni kweli au si kweli kwamba meli zilizo katika bahari ya Hindi na katika maziwa ya Tanganyika, Victoria na Nyasa ni chakavu na zimeshapita muda wake wa kuishi lakini tunazilazimisha kuendelea kubeba abiria?

.Je ni kweli au si kweli kwamba meli nyingi zinazosafiri kwenye bahari na Hindi pamoja na kuwepo kwa SUMATRA na maofisa bahari na forodha bado zinasafiri bila kuwa na vifaa tosha kama 'lifejackets' kuokoa maisha ya watu meli inapozama? Na kwamba ukaguzi na udhibiti kwa hili ni mdogo mno au sawa na haupo?

.Je ni kweli au si kweli kwamba moto ukitokea katika migodi, nyumba, shule, hospitali, meli, basi au treni ni watu wachache sana watakaonusurika kwa sababu hatua zinazolazimisha kuwepo na vizimia moto vya dharura haziheshimiwi na hazionekani kama ni muhimu. Na Uswahili unatawala kuliko utawala wa kisheria?

.Je ni kweli au si kweli, kwamba barabarani ukishakuwa tajiri au na cheo kikubwa unaweza ukavunja sheria na usifanzwe lolote?

.Je ni kweli au si kweli kwamba wenye mali au vyeo au wapambe wao wanamiliki magari mabovu yanayobeba kama mende mizigo usiku na hayaachi kufa njiani kila siku katikati ya barabara na kuua mamia ya Watanzania wanaoshtukizia wameshaingia nyuma yao.

.Je ni kweli au si kweli, kwamba mamia ya daladala jijini ni mbovu na hazifai kubeba abiria lakini kwa kuwa zinamilikiwa na wakubwa au jamaa zao zipo na zinaendelea kufanya kazi bila kubughudhiwa na mtu?

.Je ni kweli au si kweli, au reli zetu zimeoza na zinafaa kung'olewa na kuwekwa mpya ila kuhakikisha usalama wa wanaozitumia?

.Je ni kweli au si kweli kwamba balaa la maji au mafuriko au gharika ikitokea tutaangaza angaza macho tu kuiongojea nusura ya Mwenyezi Mungu na serikali yetu na tunaowalipa kodi hawataweza kutusaida kwa lolote!

.Je ni kweli au si kweli kwamba Tsunami ikitokea kwenye pwani Pemba, Unguja au Mrima kitakuwa ndio kiama kwa wakazi wengi wa maeneo ya huko maana hatuna lolote kitahadhari tulilowahi kulifanya huko wala tunalolifikiria kufanya hivi sasa?

.Je ni kweli au si kweli kwamba tufani au upepo mkubwa vikiikamia Tanzania hakuna miti wala zana maalum za kupunguza makali ya balaa litakalotuangukia?

.Je ni kweli au si kweli kwamba migodi na machimbo yetu mengi hayana usalama wa kutosha na waliomo humo wanapona tu kwa kudra ya Mwenyezi Mungu?

.Je ni kweli au si kweli kwamba baadhi ya vyakaula na vinywaji vinavyoruhusiwa kuingia nchini toka nchi za nje ni hatari kwa uzima na afya ya Watanzania?

.Je ni kweli au si kweli kwamba maji, vyakula na viliwa vingine katika mahoteli yetu uswahilini yasiyo na vyoo wala vilinda afya na siha havina tofauti na kula sumu. Na kwamba pakiwa na viwango vinavyodhibtiwa sio tu afya na usalama wa walaji vitahakikishwa bali tutajijengea heshima mbele ya watalii, wawekezaji na wageni kwa ujumla?

Katika miaka hii ya utandawazi, hatuna muda wa kupoteza. Ni muhimu kubadilika mara moja. Kazi kubwa kuliko nyingine zote za serikali ni kuhakikisha kuwa maisha na mali ya raia zake inalindwa. Serikali ikiterereka katika hili huo unakuwa ni mtihani mkubwa kwetu sote!

Na je ni kweli au si kweli kwamba ubabe na uzembe wa wenye vyombo vya usafiri na uchukuzi hapa nchini unatokana na thamani ya Mtanzania kuonekana ndogo kuliko ya ng'ombe au punda na fidia ya maisha ya Mtanzania anayepoteza kufa maisha kuwa vijisenti tuchache tu? Na kwamba fidia hiyo ingekuwa kubwa kiasi cha kumfilisi mmiliki wa chombo ajali ZINGEPUNGUA SAAANA!!!

Benki Kuu iwe na kapu la sarafu mchanganyiko

HALI ya kifedha na kiuchumi ya Marekani na misuguano ya kisiasa inayoendelea nchini humo haitupi moyo Watanzania kwamba panaweza kuwa na mabadiliko ya maana kiuchumi duniani hivi karibuni.

Marekani na nchi za Ulaya zenye matatizo makubwa zimekuwa zikiishi nje ya uwezo wao kifedha. Kwa maana ya kwamba serikali za nchi hizo zimekuwa zinatumia fedha nyingi kuliko fedha zinazoingiza kila mwaka, na hivyo kukuza mzunguko wa deni na riba serikali hizo zinazodaiwa kwa hasara ya wananchi wao. Wote tunajua hatari ya mtu anayedaiwa. Akiugua ghafla au kupatwa na janga fulani basi ndio wanaomdai wasahau tena kupata chochote kutoka kwake. Ndivyo zilivyo serikali ambazo baadhi yake nchi zetu zimewekeza na hivi leo zina matatizo makubwa ya kifedha. Hali ikiwa mbaya zaidi katika nchi hizo hawatatufikiria sisi kwanza bali wananchi wao kwa hasara yetu na nchi zetu. Ndio maana, wazo la kuwa na kapu la benki kuu lenye sarafu mbalimbali halitofautiani sana na kuweka mayai waliotaga kuku wetu wa kiuchumi katika makapu mbalimbali na sio kapu moja.

Ukizingatia pia kwamba hali ya kifedha ya Jumuiya ya Nchi za Ulaya kwa baadhi ya wanachama wake ni muflisi, ipo haja ya Waafrika na hususan Watanzania kuzinduka na kukagua upya kama sarafu na vito vya thamani vilivyoko katika hazina yetu ndivyo vinavyoweza kutunusuru kama hali ya kiuchumi duniani itaendelea kuzorota au kuwa mbaya zaidi ya ilivyo hivi sasa.

Hivi karibuni, Gavana wa Benki kuu ya Shirikisho la Nigeria, Sanussi Lamido Sanussi, ametangaza kwamba benki kuu ya nchi hiyo kuanzia sasa itaweka akiba yeke ipatayo asilimia 10 katika fedha za Kichina au Yuan. Hiki ni kitendo cha kijasiri na kiume na ambacho kinastahili kuwa fundisho kwa nchi nyingine za kiafrika ambazo kwa miaka mingi sasa zimekuwa kama mateka kama sio watumwa wa dola ya Marekani au Faranga ya Kifaransa au Pauni ya Kiingereza.

Hili liliweza kuwa sawa wakati ambapo dalili zote zilionesha nchi hizo ni kubwa na zenye uchumi usioterereka na uliokuwa ukikua kwa kasi inayobashirika. Katika miaka hii ambayo, utegemezi wa nchi hizo kwa rasilimali na biashara toka nje umeendelea kuongezeka ni hatari sana kukubali hifadhi ya taifa kuwa katika sarafu ya nchi moja au mbili tu.

Jambo hili tofauti na huko nyuma inafaa lizungumzwe na wananchi wakiongozwa na wataalamu wa uchumi na mambo ya fedha badala ya kuishia kufanyiwa uamuzi na serikali au benki kuu peke yake. Ukiritimba huu wa maamuzi ndio uliosababisha dhahabu kupakuliwa toka Benki Kuu kiujanja na kuiacha Tanzania ikipata kipigo kushoto na kulia kutokana na kushuka kwa thamani ya sarafu yake na kupanda kwa bei ya mafuta.

Mazungumzo kama hayo yatatusaidia pia kuepuka kudanganywa na nchi zilizoendelea kwa kugaiwa kondomu na chandalue zenye dawa za bure huku nchi hizo zikihamisha vitu vyenye thamani mara elfu kumi kama sio zaidi kwa matani kwenda kuwatajirisha huko kwao na kuendelea kutuacha sisi masikini wa kutupwa na ombaomba.

Yuan inapigwa vita kwa madai kwamba China bado ni nchi ya kikomunisti na kidikteta, hoja ambayo inakataliwa na wengi kwamba sio kikwazo maana Wachina walio wengi wanaridhika na mfumo huo kwa kuwa umewaletea shibe na neema. Kuna maana gani ya kuwa huru, huku ni masikini unayetumika na wakubwa?

Hali kadhalika, kutokana na wingi wao ni vigumu kuwa na nchi isyodhibtiwa kwa karibu. Viongozi wa Kichina wanaonekana pia kuwa bado ni wanafunzi katika demokrasia na siasa za kiliberali na hivyo wanahitaji kupewa muda zaidi kuweza kuachia mambo yawe yanayojiendesha yenyewe.

Dai lingine ni kuwa fedha ya China inadhibitiwa na haiachiwi kutulia na kuamua thamani yake halisi ukilinganisha na fedha nyingine duniani. Jambo hili nalo linaeleweka na kwa yakini nchi zinazoendelea zinachagizwa kuiga vivyo hivyo, kwani ukiilazimisha sarafu yako kupimwa na sarafu zenye nguvu zaidi, daima ni wewe utakayeumia na sio wale wenye nguvu. Wachunguzi wanaamini katika hili pia China inahitaji muda ili kuhakikisha ughali wa vitu vinavyotengenezwa Ulaya kwa sababu ya mishahara mikubwa ya Wamarekani na Wazungu haiingilii biashara na faida ya Wachina ambao wanalipa mishahara midogo na kukubali kuishi kimasikini ili wenzao katika nchi zinazoendelea wapate bidhaa zisizokuwa ghali.

Ni lazima tuoanishe mahitaji yetu toka nje na sarafu za nchi tunazotakiwa kuwa nazo katika hazina ya benki kuu. Ninaamini masuala kama mitambo, magari na mashine, mafuta, wapewa kandarasi za ujenzi wa miundo mbinu, masoko ya mazao yetu, masoko tunayonunua teknolojia zetu mbalimbali, wanakotoka wawekezaji wetu wakubwa, wataalamu na rasilimali watu muhimu tunazohitaji vinaweza kutumika kuchagua kapu la sarafu Benki Kuu yetu inayostahili kuwa nazo wakati wowote kwa ajili ya kujikinga na kupanda na kushuka kwa uchumi wa dunia na thamani ya shilingi yetu.

Ni dhahiri katika kufikia uamuzi wa jambo hili kuna wengi watakaopinga. Lakini kwa watu kama hao tunawataka watofautishe maamuzi ya kifedha/kirasilimali na maamuzi ya ya kisiasa na mazoea. Pamoja na mapungufu yake kadhaa kisiasa na katika haki za binadamu bado ukweli unabakia pale pale kwamba hatuwezi kukwepa kufanza biashara au kuwa na miradi inayojengwa na Wachina hapa nchini. Kwalo hilo tu, litatuondolea adha ya shilingi kupungua ukilinganisha na dola, maana thamani kati ya yuan na shilingi inaweza ikabakia pale pale kwa faida yetu.

Kwa kuikubali yuan ya Uchina tutawarahisishia pia wawekezaji wa Kichina na Mashariki ya mbali kwa ujumla wanaotaka kuwekeza hapa nchini, kwani tayari yuan inakubalika kama sarafu ya uwekezaji sehemu mbalimbali duniani. Hii ina maana wawekezaji wazawa hapa nchini wanaweza kuuza hisa katika yuan kwa Wachina ili wawe wabia wao katika uwekezaji na hivyo kupata wawekezaji wazito zaidi kutoka huko, kuliko tunaowapata hivi leo ambao wameishia kushindana na Wamachinga Kariakoo.

Aidha tunaweza kukopa toka Uchina kwa kununua hawala za Kichina kwenye sarafu yao ya yuan/renminbi na hivyo kupunugza machungu ya riba kubwa kutokana na kushuka kwa thamani ya dola ukifananisha na shilingi ya Tanzania.

Wazo kubwa hata hivyo kwa wakati tulionao unaitaka Afrika Mashariki kuanzisha sarafu yake ndani ya sarafu zilizopo. Sarafu hiyo, tuseme, iitwe, Pauni au Dola ya Afrika Mashariki itaundwa kwa kuzihusisha sarafu muhimu duniani kama Pauni ya Uingereza, dola, yuan ya Uchina, Yen ya Japan, Kronor za Scandinavia, Escudo za Brazil, rupia za India na Euro ya Jumuiya ya nchi za Ulaya. Sarafu hii itaachiwa taratibu kama ilivyo kwa Euro Ulaya kuzing'oa sarafu binafsi za kila nchi na hivyo kurahisisha kuja kwa soko la kifedha la pamoja la Afrika Mashariki na masoko mengine yatakayofuatilia.

Ieleweke kwamba pale msiba unapotokea kwa mwenzio, kwako kunaweza kuwa harusi,kwa maana kweli unaoza mwana au kwa kuwa jirani yako alikuwa mchawi.

Uchumi wa dunia unapotatizika, sio lazima uchumi wetu nao pia uwe kwenye matatizo. Lakini hili linahitaji uangavu, uweledi wa mambo, uzuzi na ubunifu wa yale yasiyoyumkinika na ambayo wengi huchelea kuyafanza kwa kuhofia hasara kumbe kwa kuyafanya watanufaika na kunufaisha nchi na watu wao. Huu ni wakati kama huo, kwa kutumia fursa za kiutandawazi tunaweza kugeuza matatizo yetu yakawa ndiyo chanzo chetu cha kufanikiwa katika mengi ambayo huko nyumba tulishindwa. Maana maendeleo yote hutoka katika akili za mtu, lakini sio wale wanaoiba na wasiojua undani na usadifu wa wazo husika.

Sunday, August 28, 2011

Tuwachunguze walio kati ya viongozi na wananchi

KUNA tofauti kati ya bibi na nyanya. Bibi ni mama yake baba. Na nyanya ni mama yake mama. Bibi aghalabu huwa mkali na akilea hulea vyema na wajukuu wakawa watu bora. Nyanya ana tabia ya kudekeza na matokeo yake ni kuwaharibu wajukuu.

Mataifa bibi ni kama vile Australia, Uingereza na Singapore. Sifa yao kubwa ni kukithiri katika kulinda wananchi wao na kuingilia maisha yao ya kila siku. Wakati mataifa nyanya sifa yake kubwa ni kulegeza kama sio kudharau kabisa utawala wa sheria. Wakati wanakuwa na uhuru unaopindukia mipaka na hivyo kuingilia maisha na usalama wa wengine kwa njia moja au nyingine na aghalabu kwa ubaya na sio wema, wizi na sio uaminifu, uongo na sio ukweli, na ubabaishaji sio uchapakazi.

Mathalani, viongozi fulani kwa kutumia kofia ya chama au taasisi ya serikali huweza kufanya maamuzi yanayowanufaisha wachache na kuwagharimu wengi isivyo haki au halali.

Yeyote anayepewa chochote au kuhongwa na viongozi kama hawa lazima atawasifu na kuwapenda. Lakini watu kama hao wanashindwa kuelewa kwamba wao wanaponufaika asilimia zaidi ya 99.9999 ya Waanzania wanakuwa wameibiwa, wamedhulumiwa au wamenyonywa kijanja janja tu. Tumeona hayo Igunga, Dodoma na kwingineko.

Katika kulea na kutokuukwaza utawala wa kisheria hayumkiniki Tanzania kuwa nchi salama kwa watalii kama sheria zetu za barabarani ni dhaifu kiasi hiki. Jiulize ni mtalii gani atakayevinjari jiji kama Dar es salaam akijua fika daladala, bajaji, pikipiki, maguta, mikokoteni na kadhalika havina njia wala sheria na wakati wowote anaweza kugongwa na isijulikane kagongwa na nini au nani?
Bila utawala wa kisheria unaodhibiti maingiliano kati ya watu mitaani ni vigumu nchi kustaarabika.

Uongozi wowote unaoshindwa kufanya kazi (mathalani Wizara ya Madini na Nishati) kwa kulitia taifa katika matatizo yasiyokwisha na kushindwa kupata ufumbuzi wa maana na unaofanya kazi kwa matatizo ya wananchi hujiingiza katika kuridhishana na kupongezana wenyewe kwa wenyewe. Hutafuta kufanikisha mambo yao kwa siasa za bei sawa na bure. Au kwa maneno mengine siasa za ubabaishaji na maneno matupu yasiyomnufaisha mwananchi wa kawaida. Sera zinazoongeza tofauti na wivu kati ya walionacho na wasio nacho. Sera zinazojenga tofauti kuu ambazo hatimaye huchangia sana kuwa chanzo cha mifarakano katika jamii.

La kutisha ni upofu uliopo katika wizara, mikoa na wilaya kwa viongozi wa maeneo yao kutoona alama za nyakati kwa kubaini ukweli kuhusu umaskini wa kutisha wa wananchi mijini na vijijini. Nusu bilioni sio kitu kidogo kufanya sherehe, tena kwa wizara ambayo haina ufanisi wala ufanifu katika mambo yake, bali imelitia hasara taifa kwa kila hali.

Umefika wakati kwa viongozi wetu kujijua wao wenyewe na dhima walyo nayo kwa masikini wa nchi hii na kisha kuijua na kuikubali hali halisi ya umaskini Tanzania na kujiepusha kutapanya fedha katika masuala ambayo haimpi nafuu wala usalama wa maisha Mtanzania wa kawaida. Kinyume cha hivyo, ni kwa viongozi wetu kukubaliana na kile kilichomo katika biblia katika maneno kama, "masikini watakuwa nanyi daima!' na kisha kuhalalisha wao kupata na masikini kukosa kama ilivyo kwa hivi sasa lakini kwa maafa ya kizazi kijacho.

Inavyoelekea kuna viongozi Wizarani, Ikulu, mikoani na wilayani ambao wanataka kuendeleza kile tusichokitaka kiendelee, ambacho sio kingine, ila viongozi na matajiri nchini hapa kuishi kifahari na kwa raha wakati bahari ya masikini, yaani, wananchi walio wengi wakiendelea kuishi katika umasikini na uhitaji wa kutisha.

Pengine ni kwa sababu hii ndio maana nchi kama Tanzania zinaitwa 'mataifa nyanya'. Yanalea vibaya, yanadekeza na kuharibu kizazi kipya. Yanajifanya ndio baba ndio mama na yatawatimizia wote mahitaji yao, wakati ukweli ni kuwa hayawezi na jamii ni muhimu iwe na kiwango fulani cha kujiegemea kwa kutumia nguvu zao na mitaji yao asili. Na leo hii, tuna kizazi cha Watanzania wanaotaka tuishi kama vile tayari wao kwa kuwa viongozi basi eti nchi hii iko kwenye neema. Wamechemsha hapo. Na hawa sio viongozi wanaoweza kuleta mabadiliko ya kweli vijijini kuliko na masikini wengi.

Zipo gharama kwa kila fursa. Ukitumia nusu bilioni kujipongeza basi kuna wanafunzi wanaokosa mikopo, vijana wanaokosa ajira na vijiji vinakosa ama maji au dawa au pembejeo.

Matatizo yetu kwa kiasi fulani yanachangiwa na mifumo mbalimbali kukosa kumbukumbu, kuingiliana, kusuguana na kutegeana kwa hila katika hili au lile ili mtu au kikundi cha watu binafsi kifanikishe maslahi yake hata kama kwa kufanya wananchi walio wengi wanaumia. Bila mihimili ya taifa, yaani, serikali, bunge, mahakama na vyombo vya habari kuwa na viongozi na watumishi wanaojiona sawa kwa kila hali na sio watumiwaji wa wengine sio rahisi kufanikisha azma zetu mbalimbali za maendeleo kijamii, kidemokrasia na kiuchumi.

Kazi za kiongozi wa nchi ambayo inatambua ilikotoka, ilipo na inakotaka kwenda kwa faida ya watu wake wote sio kutetea kama kipofu maslahi ya kundi lolote lile iwe la kisiasa au vinginevyo kuendelea kuwepo achilia kushikilia madaraka fulani. Kama nchi ikiwa na kiongozi wa namna hiyo wakati ambapo mabadiliko katika jamii husika na utandawazi unadai vinginevyo basi huo ndio mwanzo wa kuuana wenyewe kwa wenyewe.

Kazi za kiongozi yeyote katika kipindi hiki ni:
kuhakikisha haki inatendeka kwa wote bila uonevu; kusimamia usawa na kupiga vita ubaguzi;
kuwafanza watu waamini na kuipenda serikali yake
na kujua na kudhibiti tabia za walio chini yake na katikati yake na wananchi
ili kuepusha matapeli na makuwadi wa kisiasa kuiingiza serikali mkenge.

Aidha ni kazi ya kiongozi kuhakikisha shibe ya watu wake wote bila ubaguzi; kuona maji yanatiririka kila mji kila kijiji wakati wote; wagonjwa wanaangaliwa vyema na kutibiwa; wazee, wajane, watoto, mayatima na watu dhaifu wanalindwa kwa hali na mali. Kazi kama hii, kamwe, haiwezi rais ambaye sio imara na madhubuti na wakati huo huo ni mwenyekiti wa chama cha kisiasa nchini.

Nchi ikiwa na miundo na mifumo inayofanya kazi, hata kiongozi dhaifu huweza kuonekana bora. Lakini kinyume cha hivyo, hata kiongozi mzuri anaweza kuonekana kanyaboya na mbabaishaji.

Awamu ya nne ilianza na baraza kubwa sana la mawaziri. Limepunguzwa katika kipindi cha pili cha awamu hiyo. Lakini bado kuna wanaoamini uratibu umekuwa mgumu kama ilivyotabiriwa. Viongozi na watumishi wanakanyagana. Bado tunaamini Tanzania inaweza kuongozwa vizuri tu kwa kuwa na wizara kati ya 12-15. Ziada hapo bora kuwa wakala au programu au taasisi maalum.

Udhaifu hujidhirisha pale viongozi au watumishi wa chini wanapofanya maamuzi bila idhini ya mkuu wao wa kazi; watumishi wa serikali wanapopokea amri kutoka kwa matajiri na sio viongozi wa serikali; baadhi ya watu wanaponufaika na rasilimali za taifa za ziada wanazopata isivyo halali na kisha watu hao kuwaabudu wale wanaowagia ngawira hiyo haramu; pale haramu inapogeuzwa halali; uzito wa kufanya maamuzi magumu pale mwanakundi haramu anapofanya kosa; kiongozi au mkuu wa kazi anapoamini kila kitu kinakwenda sawa kwa sababu ya kusifiwa kiuongo na walio chini yake; kiongozi au mkuu wa kazi anapodanganywa na kufichwa ukweli na kisha kuamini uongo ndio ukweli; taarifa kamili na zisizochujwa kutomfikia kiongozi au mkuu wa kazi.

Aidha udhaifu huonekana pale ambapo walio chini ya mkuu huyo wanapowatumia ndugu, watoto, jamaa na watu wa karibu naye kwa kuwapa kilicho haramu ili wahalalishiwe uharamu au dhuluma yao kwa wananchi walio wengi; serikali husika inapofadhiliwa na matajiri wenye malengo binafsi na sio ukombozi wa masikini; kushindwa kutofautisha maslahi binafsi na yale ya nchi; kushindwa kuelewa hali ya wale wanaoongozwa (kitu kilichonfanya Harun Al-Rashid kutowaamini moja kwa moja walio chini yake, na mara kadhaa kujifanya mtu mwingine na kuranda mitaa usiku ili ajue hali ya watu wake na matatizo yao).

Kundi la watendaji au watekekelzaji walioko kati ya viongozi na wananchi ni kundi nyeti sana. Linaweza kuijenga nchi au kuiangusha nchi. Na kama kuna gamba liliostahili kuvuliwa awali ya yote basi lilikuwa ni kulidhibiti kundi hili ambalo kwa siri au dhahiri linaamua kupora wananchi, bunge na hata serikali yenyewe nafasi na mamlaka yake na kujianzishia serikali nje ya serikali. Huu ndio ukweli wa mambo, kama hatuajauona sasa tufungue macho na kuliona. Kama ofisa wa nchi anajiona ana uwezo kuliko Waziri Mkuu na Bunge na Ikulu inaogopwa kuliko rais anavyoogopwa basi kuna walakini mkubwa mahala fulani.

Wednesday, August 17, 2011

Nini chanzo cha migogoro kati ya wananchi na wawekezaji




NI kitu cha aibu kwamba hata viongozi wetu wa juu hapa nchini wameamua kuingia kwenye mbio za PRIMITIVE ACCUMULATION, labda pengine kutokana na kisomo chao duni na kushindwa kupata nafasi kimataifa kujipatia kipato baada ya kustaafu.

Lakini wakati huo huo ni nafasi ya wazi kabisa kuona jinsi ubinafsi na umimi unavyojijenga toka juu kabisa serikali hadi chini kabisa. Kisha mtu ajiulize hawa ndio watu waliokusudiwa kweli kujenga taifa la kijamaa au Nyerere alizaliwa katika nchi tofauti kabisa.

Binafsi, haya yote ninayaona katika macho ya ubinadamu na uhalisia wa mambo-kwamba hakuna mtu anayezaliwa kuwa mjamaa na hakuna Mtanzania anayependa mwenzake apate, ili anataka apate yeye tu, hata kama hana uwezo, akili na nguvu za kukitumia hicho anachojilimbikizia.

Huu ndio utamaduni wetu, na hao ni viongozi wetu na kizazi chao. Je, sasa tufanye nini. Ninaamini ya kwamba maendeleo yetu yatakuwa sawa na kupanda mlima mkubwa zaidi ya Kilimanjaro kama tusiporudia kwenye mambo ya msingi katika siasa za waasisi wetu na hususan Mwalimu Nyerere.

Kwanza, badala ya viongozi tena wa chama tawala chenye historia kongwe ya vita dhidi ya ubinafsi na kujilimbikizia mijimali lazima watangulize wananchi na hususan wanavijiji wa Tanzania mbele.

Badala ya kujijenga hekalu mbadala wake ungelikuwa ni kuwajengea wanavijiji 5,000 katika kijiji fulani kila familia nyumba ya kisasa ya vyumba vitatu.

Tunalalamikia foleni na kufurika kwa watu mjini lakini sio siri kuwa vijiji vikiwa na maji ya bomba, umeme, barabara safi na kumbi za starehe na huduma zote muhimu nchini ni wachache watakaotaka kubakia mjini.
Ukileta neema zaidi ya wanavijiji kutumia matrekta madogo kwa makubwa badala ya kisigirima ndio kabisa watu wataanza kuhama kuelekea vijijini na hivyo kuipa miji nafasi ya kupumua na mingine kufa kifo cha kawaida.

Ili hili lifanyike ni lazima viongozi wa kisiasa waache kutanguliza tamaa zao binafsi, uroho wa mali na kujilimbikizia na kuweka vipaumbele kichwa chini miguu juu.

Tatizo la Watanzania ni umaskini mkubwa na kukosa ajira na kipato cha kutosha kujiendeleza kwa vijana na wakulima nchini.

Yapo mambo mengi ambayo tukikaa na kutafakari tunaweza kuyafanya kwa pamoja au mtu mmoja mmoja na fumba na kufumbua kila tatizo nchini likageuka ni fursa ya kiuchumi au ya kuisongesha mbele jamii yetu.

Kabla hatujafikia hapo ni lazima kwanza TUWATHAMINI WATU WETU, TUTATHMINI UPYA THAMANI YA ARDHI, MADINI NA MALI ASILI ZETU NA TUTHAMINI UPYA UTU, MILA NA UTAMADUNI WETU KAMA RASILIMALI WATU YA KWANZA NA MUHIMU KULIKO ZOTE KWA FAIDA YA SIKU ZETU ZA USONI-WATU WETU.

Kuanzia Arusha hadi Zanzibar haipiti siku bila kusikia habari kwamba kuna tatizo kati ya wananchi na wawekezaji kwenye eneo fulani. Habari hizi za kuwepo na kuendelea kuwepo kwa mgogoro fulani ni dalili kwamba kuna ugonjwa fulani ambao umeanza na unaendelea kuenea na mgonjwa hata hajaonwa na daktari.

Kwanini wananchi wachome hoteli ya Kitalii; kwanini wananchi wavamie mgodi na baadhi yao kuuawa; kwanini viongozi wa juu wa serikali wa sasa na wa zamani walalamikiwe kuhondhi maeneo wasiyoyaendeleza na waliyopewa bure au sawa na bure ?

Sipendi kujifanya kwamba nina majibu ya kila tatizo linaloisibu nchi hii na watu wake. Ninaamini wapo wengi tu wanaojua zaidi yangu, lakini kwa sababu moja au nyingine wameamua kulifumbia tatizo hili macho. Kati yao wakiwemo wataalamu wa mambo ya ardhi, wanasheria na wanasiasa.

Ndio maana ninaamua kuwaandikia watu wa kawaida kwa njia ya maswali yasiyo na majibu ili waamke na wafanye kile kinachoonekana. Na umma uliolala ukizinduliwa toka usingizini hauwezi kamwe kuwaachia viongozi waendelee kupiga usingizi huku matatizo yao mbalimbali yakiwa hayajapata ufumbuzi.

Katika migogoro hii inayowahusisha wananchi na wawekezaji wa nje na wa ndani, inafaa kuuliza maswali kadhaa ya msingi kama vile, je, matatizo hayo yalianza lini? Yanapungua au yanaongezeka kila mwaka?

Hivi ni kweli kwamba Watanzania wengi kwa sababu wanazozijua wao wenyewe hawapendi wawekezaji ? Au wawekezaji hao na wakubwa wanaowakaribisha kuwekeza hapa nchini na mangimeza wa serikali na kati ya viongozi wa serikali za vijiji na mitaa kuna mkono wa mtu, na wanachokifanya ambacho kinawaudhi na kuonekana ni dhuluma kwa wananchi?

Kama zilivyo nchi nyingi za Kiafrika ni mwekezaji na hususan mtu mwenye ngozi nyeupe ndiye anayethaminiwa lakini sio raia na hususan yule mwenye ngozi nyeusi au mzawa ? Daraja hizi mbili au tatu za thamani tofauti kwa binadamu zinaigharimu nini jamii na nchi yetu? Na, je, huu ni mkakati muafaka wa kuiwezesha nchi kuja kuondokana na umaskini na kuwepo nyuma kimaendeleo hapo kesho na kesho - kutwa?

Na swali ambalo ningeliita ni MAMA WA MASWALI YOTE: Je, serikali yetu inaipa ardhi, mali asili, madini, gesi, mashamba, vijiji na utamaduni wa watu wetu thamani halisi na ya haki?

Nionavyo mimi, serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo na ile ya Zanzibar zimeshindwa kuvipa vitu hivi thamani halisi na ya haki na uhakika na ndio chanzo kikuu cha matatizo yanayoendelea kushoto na kulia nchini. Na huu ni mwanzo tu, utafiti wa kina na hatua za haraka visipochukuliwa hali inaweza kuwa mbaya zaidi.

Tanzania kama zilivyo nchi nyingi za Kiafrika ni nchi ambayo wanasiasa na viongozi wake hujiweka wao mbele kwanza na wameamua kujipa wao thamani kuliko mtu au kitu kingine nchini. Na wao wakishathaminiwa kama sio kuogopwa, kutetemekewa na kunyenyekewa na wale wanaowaneemesha basi sio kitu watu wanaowaongoza wakionekana hawana thamani. Mifano iko mingi, tazama mkubwa mmoja anavyopita njiani na kusababisha kinamama kujifungua njiani; tazama anavyozungukwa na ulinzi wa kutia kufuru; tazama hekalu au kasri anayojijengea na familia yake (kama vile kizazi chake kitamudu kutunza); tazama wapinzani wanapoandamana na mamilioni yanayofujwa ili kuwadhibiti; tazama wizara zinavyosherekea kupita kwa bajeti zao na tazama misafara ya wakubwa wakienda nchi za nje au kutembelea mikoani.

Angalia pia wanavijiji wanavyouawa na korokoroni wa migodi ya dhahabu na undumilakuwili wa serikali; wananchi wanaoathirika na ajali kila mwaka na fidia wanayolipwa; viongozi wanavyowatumia ma-RC na ma-DC kujimegea maeneo makubwa makubwa ya ardhi kwenye mikoa wasiyo na nasaba wala udugu nayo na wananchi wanavyohamishwa na fidia ndogo wanayolipwa.

Hii ndiyo hali halisi ilivyo. Wananchi mikoani na wilayani hawana sauti juu ya mali zao walizorithi toka kwa wazee wao. Na mtu anaweza kuzuka huko aliko iwe makao makuu ya wilaya au mkoa au nchi akatangaza eneo fulani kuchukuliwa kama vile mtu anajigawia shamba la baba yake aliyefariki. Na mwananchi hatakiwi kulalama au kupiga kelele, maana eti, hili ni la manufaa kwa nchi na watu wake. Lakini sio kwa manufaa ya mwananchi mhusika. Hivi, jambo hili sio kichekesho cha wakati wetu kwa kweli?

Maisha ya Mtanzania hayana thamani kwa sababu mali alizonazo hazipewi thamani halali, halisi na ya haki. Hata kwa ardhi iliyo duni au mbaya kabisa kwa ekari moja mwananchi hatakiwi kukosa angalau chini ya shilingi milioni mbili (kama iko mbali na mji). Na kama ardhi hiyo iko kwenye eneo lenye maji na ina rutuba haiwezi kuwa na thamani ya chini ya milioni tano. Ukizungumzia ardhi ambayo imegundulika chini kuna madini au mafuta au maji au nguvu ya kutoa nishati ya umeme, haiwezi kamwe kuwa na thamani ya chini ya milioni 25 kwa ekari. Na hizi ni thamani za chini kabisa, lakini sio mbaya kuanzia.

Hata hivyo, kwa miaka hamsini toka tupate uhuru, viongozi wetu wakishapewa chao cha chambele kwa mbele na
kuondokana na umaskini wao wa kuzaliwa, wawekezaji wamekuwa wakihalalishiwa kuwadhulumu wanavijiji kwa ushirikiano usio mtakatifu kati ya viongozi wa juu, viongozi wa mikoa na wilaya na viongozi wa vijiji.

Wanasiasa, wanauchumi, wabunge, wataalamu wa ardhi na wanasheria wetu wana deni kubwa la Watanzania ambao babu na baba zao wamedhulumiwa na mfumo uliopo hivi leo kuhakikisha hata kabla katiba mpya haijaandikwa dhuluma hii inakomeshwa.

Ni jukumu lao pia kuona kwamba katiba mpya itakuwa na vifungu vyote muafaka vinavyowawezesha wananchi wao wenyewe, ardhi yao, madini yao na mali asili zao nyingine kuwa na thamani ambayo kama wanabadilishana na wawekezaji basi watoto na wajukuu zao watakuwa hawana tena sababu ya kufa maskini.

Mtaji wa Masikini

Mtaji wa Mtanzania masikini sio tu nguvu zake mwenyewe bali pia ardhi, misitu, bahari, madini, gesi,mkaa, mafuta na mali asili zake zote. Umaskini wetu kwa kiasi fulani unasababishwa na muasisi wa msemo huu na serikali yake na uongozi mzima unaoshindwa kuvipa thamani majaliwa ya watu na vitu vilivyooneshwa hapo juu kwa sababu wanazozijua wao wenyewe.

Remi Isaac na Jos van Der Sterren (2004) wameliona hili na ndicho wanachokiita chanzo cha msingi cha kimuundo na kimfumo cha umaskini wa nchi nyingi za Kiafrika.

Watu wanamiliki ardhi au mashamba; wana mifugo; wanaishi pembeni ya bahari na maziwa yenye samaki kabakaba; wana misitu yenye miti adimu; wana mila na utamaduni wao; na wana mali asili za kila aina chini ya ardhi yao, achilia mbali mazingira yao ambayo awali ya yote ni salama kuliko kwa wawekezaji, lakini serikali zao zinapofikia makubaliano na wawekezaji vitu hivi vyote
eti vinaonekana kukosa thamani kabisa. Wizi ulioje huu? Na kwanini usikome kuanzia sasa ?

Wananchi waelewe ardhi na mali asili zao ndio jambo muhimu kuliko kitu kingine chochote kwenye katiba yao. Katiba sio jambo la chama tawala kung'ang'ania madarakani au upinzani kuking'oa au wasomi wa sheria kunufaika na kupalilia nafasi zao bali ni ngao ya mnyonge na maskini. Katiba ni andiko takatifu linalomrejeshea raia wa kawaida uhuru wa kuamua wale wanaomtawala wana haki zipi na yeye raia kama mtawaliwa ana haki zipi. Lakini mamlaka na madaraka yote anayo yeye raia na kiongozi au viongozi ni waajiriwa wake na sio mabwana zake. Ni katika mustakabali huu ndipo umuhimu wa wananchi kushiriki katika mchakato wa kuandikwa kwa katiba mpya unapokuwa na umuhimu wa juu zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Ardhi isipolindwa na isipotunufaisha kupitia katiba basi nchi inaweza ikaja uzwa na kongozi yoyote yule ajaye-awe tioka chama tawala au upinzani. Ni lazima wananchi waamue ni utajiri gani kama mtaji au mali ya msingi ambao ardhi, wao wenyewe, mali asili zao mbalimbali na utamaduni na mila zao wanastahili kuwa nayo na kuchangia katika miradi mbalimbali.

Mwekezaji aliyewekeza Geita, Bulyanhulu au Nyamongo alistahili kuambiwa kwamba ardhi yenye madini anayopewa ina thamani ya bilioni kadhaa na sio vijisenti kadhaa. Na wamiliki wake ni wakazi waliokuwepo. Kwa mtaji huu wakazi wa maeneo yote hayo hivi leo wangelikuwa ama ni wanahisa katika kampuni zinazochimba dhahabu huko kwa hivi sasa au wangekwishasepa na mamilioni yao na kwenda kuwekeza kwenye kile wanachokipenda na kukiamini zaidi kuliko uchimbaji madini.

Kadhalika badala ya wananchi kupewa maharagwe na sembe pembezoni mwa mbuga za wanyama kama kuna ardhi yao ilichukuliwa, basi wananchi hao walistahili kabisa kuwa na hisa katika TANAPA nchi nzima na kila mwaka wangelikuwa na haki ya kupata mgawo wao tokana na kinachoingizwa na shirika hilo.

Aidha, masikini ambao juzi walikuwa ndio wamiliki wa ardhi ya Mnazi Bay au Songosongo au Merelani au Liganga au Mchuchuma au Mwadui au Songea au Chunya na kwingineko kwenye gesi au uranium au mafuta au madini mengineyo au mali asili nyingine hivi leo sio tu wangelikumbukwa na wagumu wa kukumbuka watu kama TANESCO bali pia wangelikuwa ni watu wenye mali na nafasi zao kijamii. Lakini muundo na mfumo uliopo uliwadhulumu, umewadhulumu na unaendelea kuwadhulumu na pengine hivi leo hali zao ni mbaya zaidi kuliko zilivyokuwa kabla ya uwekezaji uliohalallishwa na kubarikiwa na watawala wetu wa nyakati hizi, bila kuwajali wananchi wanaotakiwa sio tu kuwaongoza bali kuwalinda, kuwawezesha na kuwaneemesha pia.

Katika hali kama hii, ninaamini, hata kwa mtu asiyekwenda shule, hawezi kushindwa kuelewa ni kwanini kuna migogoro kati ya wananchi na wawekezaji. Na sio tu yapo yaliyopo bali yapo mengi tu yatakayozuka kesho na kesho kutwa. Amani na umoja wetu utakuwa mashakani. Ni heri nusu ya shari kuliko shari kamili. Tujifunze kutokana na makosa yetu huko nyuma. Tujisahihishe. Ng'ombe wa maskini pengine anaweza asizae, lakini ardhi ya masikini lazima ima fa ima katika miaka hii IZAE tena izae kwa sana tu! Ni ardhi na vilivyomo ndani yake itakyotujenga au itakayotuangusha.


Mwekezaji ambaye si tapeli bali muadilifu, anayeona mbali na mbele na anayetaka kuwa sehemu ya maendeleo ya nchi yetu na watu wake ni yule ambaye atakubali kukaa nasi na kuona ni kwa jinsi na namna gani shughuli zake zinaweza kuoanishwa na mahitaji, matakwa, matamanio na ndoto za Watanzania kama kitu kimoja na sio vinginevyo.

Thursday, August 11, 2011

Tumebinafsisha visivyostahili kubinafsishwa




BAADA ya zaidi ya miaka 15 ya kubinafsisha vitu mbalimbali Tanzania sio vyote vilivyobinafsishwa vimekidhi matarajio yetu.

Wakati mashirika ya umma yanabinafsishwa watu walitarajia kuona uzalishaji ukiongezeka, ajira zikiwa za kumwaga na umaskini nchini ukipungua. Hivi leo kilichoonekana kuleta matumaini na mategemeo makubwa hakibebeki. Kizito. Kigumu. Na mbele kinachoonekana ni giza tu.

Ingawa kuna mafanikio kwa baadhi ya kampuni zilizobinafsishwa, zipo nyingi ambazo leo ndio sababu ya malalamiko na kilio chetu kikubwa.

Inavyoelekea, hatua la kubinafsisha ilifanywa haraka kutokana na msukumo wa IMF/WB ambao hawakutupa muda wa kuangalia kasoro mbalimbali zilizojitokeza na kisha kuainisha sababu hizo na kuzihakiki na kuona nini na sio tu kubinafsisha kungeweza kuliokoa jahazi letu la maendeleo.

Ninaamini kwamba jambo lolote katika nchi zetu za Kiafrika linalogusa maisha ya walio wengi linahitaji tahadhari kubwa katika uamuzi wa kutaifisha au kubinafsisha. Ni kweli, tunataka Serikali ifanye kazi za kiserikali na uendeshaji kampuni na biashara ufanywe na watu mbalimbali nchini na toka nje, lakini kuna mengine kwa kuzingatia saikolojia ya binadamu sio vizuri kuvibinafisha bila kuwa na mibadala sheria na kanuni zinazoweza kutumika kurekebisha mambo pale yanapoharibika.

Hali inazidi kuwa ngumu zaidi kutokana na Tanzania kutoka kwenye ujamaa na kuingia kwenye ubepari. Viongozi waliojikuta hawana lolote wanachakarika huku na huko ili nao saa kumi na mbili jioni waneemeke na watajirike. Wanachoshindwa kuelewa ni kwamba unaweza ukachuma eneo fulani, mathalani siasa, lakini ukijiingiza kwenye biashara unakwenda na maji.

Pupa hii ya viongozi wa serikali na vyama vya kisiasa, hata hivyo, ndio iliyoiingiza nchi mahala ilipofikia, kiasi cha benki kuu kusafishwa na mafisadi, mikataba bomu kutawala baraza la mawaziri na sasa hata vitu kama UDA kuuzwa kinyemelea ili kuwawezesha wakubwa kuishi maisha ya ukubwa kama ilivyokuwa zamani.

Mojawapo ni eneo la petroli na dizeli au mafuta yanayotumiwa na magari na vyombo mbalimbali vya usafiri na uchukuzi. Kwa maoni yangu, ni vyema shughuli ya uagizaji wa mafuta toka nje au uchimbaji wake hapa ndani ukafanywa kwa ubia kati ya Serikali na kampuni au nchi za nje. Serikali katika nafasi yake ina uwezo wa kununua kwa bei za sasa na za baadaye na kisha kuhifadhi mafuta kwa wingi wa kutosha kuiepusha nchi kuyumba kutokana na kupanda bei ya mafuta au kupungua kwake katika vipindi vifupi kutokana na hali ya uzalishaji mafuta hayo na bei yake katika wakati husika.

Uuzaji mafuta ndani ya nchi unaweza ukafanywa na watu binafsi na kwa kuwa Serikali ndiyo mwagizaji mkuu ni rahisi kuratibu na kupanga bei wakati wowote. Tunachohitaji ni mameneja waadilifu na wazuri ambao hawataingiiwa na wanasiasa katika kazi zao.

Ni muhimu pia kwa serikali na hususan TASAF kuingia maeneo ya mjini na kusaidia kuwawezesha wananchi kuanzisha miradi ya kijamii ikiwemo ya usambazaji na uuzaji rejareja wa petroli ili kupunguza makali ya sekta hii kushikwa mia kwa mia na watu binafsi.

TAFICO ilianzishwa ili Watanzania wapate kitoweo cha bei nafuu. Haieleweki ni katika mazingira gani shirika hili linalohitajika kufa na kupona na wananchi liliuzwa. Lakini sinema inayoendelea leo, iwe ile ya Samaki wa Magufuli au Samaki toka Ujapani zinazohofiwa kuwa na mianzi ya 'yuraniamu' ni matokeo ya uongozi na nchi ambayo imeshindwa kutunza kitu ambacho kingetunza nchi na watu wake na pengine hata kulinda lishe na afya yao. Haliingii kichwani kwa mtu wa pwani au maziwani kushindwa kibiashara kazi ya uvuvi. TAFICO lilikufa tu kwa sababu wakubwa waliliingilia kisiasa kama yalivyokuwa mashirika mengine yaliyokufa. Mashirika mengi yaliuawa na hayakujifia yenyewe. Na baadhi ya walioua mashirika hayo wapo hai, lakini kwa kuwa walikula na wakubwa na wenye nchi hakuna wa kuwagusa.

Eneo jlingine ambalo ni hatari kwa usalama wa raia na maslahi yao ya kiuchumi ni lile la maji. Serikali haiwezi kukaa pembeni na ikamkabidhi mtu toka nje au ndani ya nchi mashirika yetu ya usambazaji na uuzaji maji na hasa kwa miradi mikubwa ya miji kama Arusha, Tanga, Dar es salaam, Dodoma, Mwanza, Mbeya na Zanzibar.

Maji ni uhai. Lakini maji pia ni kifo. Hasa yakiwa mikononi mwa watu wasioaminika na wasio na uchungu na maisha ya Mtanzania.

Wote tunafahamu jinsi ambavyo DMT na baadaye UDA lilivyoendeshwa kistaarabu na kwa utu wa hali ya juu. Ilikuwa makosa kugeuza upungufu wa mameneja na watumishi wa shirika hilo kuwa ndio sababu ya kulinyonga shirika hilo. UDA bado linahitajika na ikipatikana fomula ya kuwapata mameneja wazuri hata kama ni kutoka nje; uwekezaji wa wanajamii na mchango wa Benki Kuu na benki nyingine bado jiji hili linaweza kwa mara nyingine kupata usafiri unaoaminika na unaothamini na kuheshimu abiria kuliko ilivyo sasa.

Daladala hivi leo ni mfafhaiko mtupu. Ni jinamizi ambalo kila mtoto wa shule akiliota hawezi kamwe kufaulu vyema. Ni jinamizi ambalo kila mfanyakazi akilifikiria hawezi kuwa na ubunifu au uvumbuizi wa aina yoyote ile.

Haya yote yanatokea kisaikolojia kwa kuwa mtu binafsi anajali yeye apate lakini sio mwingine apone achilia mbali kupata. Haileweki barabara za kasi zinazozungumwa kama ni stori ya Alinacha au ni kitu cha kweli? Palikuw ana porojo ya kutumia reli inayooza yenyewe kwa usafiri wa jiji, lakini Watanzania wanaamini hivi leo wanasiasa wao ni wapiga porojo tu na hakuna kitakachofanyika. Tuombe iwe kinyume cha hivyo.

Watu wengi wanauliza kwamba, hivi serikali yetu ilikuwa na njaa na umasikini kiasi gani kiasi cha kubinafsisha sekta ya uchimbaji madini kwa hasara. Ni dhahiri kuwa tathmini ya utajiri huo haukufanywa ipasavyo na wala haukuzingatia thamani ya ardhi yetu, watu wetu na mali asili zetu.

Haifahamiki ni kwa nini tuliweka Chuo cha Utafiti na Madini hapa Dar es salaam wala kitivo cha jiolojia pale Mlimani wakati wataalamu wake inavyoelekea upo uwezekano mkubwa kwamba hawakushirikishwa kabisa katika uamuzi huu ambao leo ni msiba na majonzi kwa taifa.

Hivi leo unaweza ukiwa na dhamana kukodi sio kununua mitambo ya kila aina duniani. Kukodisha mitambo ni nafuu kuliko kuinunua. Na hili lingefanyika Watanzania leo wangekuwa wanachimba dhahabu yao wenyewe. Isitoshe hivi kuwapa watu maeneo 3-5 kwa mpigo kuchimba madini ilikuwa ni akili au ujinga? Au ndio kuukata kwa wenzetu waliobahatika?

Kuhusu benki, CRDB Bank ni benki pekee iliyobinafsishwa na kuwa na manufaa kwa Watanzania.. Nyingine zimebinafsishwa kihasara na leo hatujui twende wapi wala tukamlilie nani.

Ukitaka kujua nchi iliyochanganyikiwa basi ni Tanzania. Hivi leo eti tunaanza tena kutafutana kuanzisha Benki za wananchi kama vile Community Bank, Benki ya Akinamama, Benki ya Wakulima, Benki ya Wanawake, Benki ya walimu na kadhalika. Hivi hatukuliona hili kabla? Au ni kwa sababu Mtanzania bahili kutoa teni pasenti basi ilibidi tuwauzie wazungu wanaokubali teni pasenti ?

Shirika letu la Ndege nalo limekumbwa na ila hiyohiyo. Kama baba na mwanao unamjua hana uwezo wa kufanya kitu fulani nawe una uwezo wa kuwekeza, basi ni vizuri uajiri mtu mwenye uwezo afanye kazi hiyo na mwanao akae pembeni na kwa kuwa unampenda umpe posho ya kila mwezi au sio?

Aidha, ni vyema kwamba tumeshindwa kuliuza shirika la simu (TTCL), ingawa tumelinyofoa hapa na pale, lakini hili ni shirika ambalo halistahili kuuzwa kwa kuona faida ambayo Tigo, Vodacom na Airtel wanaipata.

Katika tafiti zangu zinazoendelea nimegundua kwamba pamoja na kubinafsisha ulinzi na usalama nchini kwa kiasi fulani usalama nchini umepungua. Sio mimi ninayesema hivyo. Watalii. Pengine ipo haja ya kufanya utafiti kuyakinisha hili. Na utafiti huo usifanyike kijuujuu na kuacha kuona maana pana ya usalama toka kwenye macho ya mgeni au mtalii na sio mwenyeji.

Kwa mtalii, ukosefu wa usalama ni pamoja na kutokuwa na kinga za kuridhisha dhidi ya hali ya hewa, moto, maji na vitu kama hivyo. Kama ilivyo kwa hatari mbalimbali ambazo ulegevu wa sheria zetu za barabarani unamtia mashaka mtalii kutembea mjini kwa kuhofia kugongwa na daladala, bajaji, pikipiki au baiskeli au hata na watembeaji kwa miguu kwa sababu nchi haina nidhamu katika maingiliano ya watu majirani. Aidha kukosekana kwa treni na kubakia magari kama njia kuu ya usafiri ni kitu kinachoupa usafiri na uchukuzi wetu maksi sifuri kiusalama.

Ukosefu wa usalama kwa mtalii ni pamoja na kuwepo kwa nzi mahotelini, mbu vyumbani na maji yasiyoaminika hata kwa kunawia na kuogea.

Nitaliongelea hili peke yake katika makala zangu zijazo. Itosheleze tu kusema kuwa usalama ni zaidi ya mtu kuibiwa, kupigwa au kuuawa.

Ukitembelea mashamba yaliyokuwa yakimilikiwa na Serikali kule Masama au West Kilimanjaro, Mbeya, Iringa na kwingineko utatamani kulia. Ninaamini kwamba bado serikali kwa kushirikiana na Chuo Kikuu chetu cha Kilimo cha Sokoine, Mashirika ya utafiti wa tija katika mazao, mifugo na samaki basi yanaweza kugeuzwa kwa namna ambayo yakaendelea kuwa ni shule kwa wakulima, wavuvi na wafugaji wetu wadogo ili wawe wakubwa kesho na keshokutwa.

Silo la kuhifadhia nafaka nazo ninasikia lakini sina uhakika kwamba baadhi yake zimebinafsishwa. Kama ni hivyo, hili nalo ni kosa. Hivi miaka elfu ngapi baada ya Nabii Yusufu kuikoa Misri, sisi Tanzania tunashindwa kuwa na chakula cha kututosha kwa angalau hiyo miaka 7 tu?

Baadhi ya nyumba na majengo ya serikali yamebinafsishwa sawa na kutolewa bure. Pengine kwa kuwa walionufaika ni kina mama zetu wakubwa, watoto wetu, ndugu, jamaa na marafiki. Lakini tukumbuke hizo ni mali za serikali na kufanya hivyo ni kuwadhulumu watu wengine. Dhuluma inayoendelea kupandwa juu ya dhuluma nyingine ambayo inaweza kuwa sababu ya kuchangia nchi hii kukosa mwelekeo na dhamira ya kweli katika kuwaondoa watu wetu kwenye umaskini.

Tumetaifisha viwanda vingine, lakini kinachoendelea ni kwa waliowekeza kuuza mitambo yote na kisha kugeuza viwanda hivyo kuwa bohari zao za biashara na ubebaji mizigo. Hiki ndicho tulichoazimia. Na kwa nini hatua huzichukulia. Au mikataba iliwaruhusu watu kama hao kufanya lolote lile watakalo?

Hivi leo, eti tunazungumzia kuanzisha viwanda kama vile hatukuwa navyo kabisa. Mbona tunachezeana akili na 'intelligence' yetu ya kuzaliwa jamani? Au wote tunaonekana kuwa na akili fupi kiasi hicho, kiasi cha kutokumbuka mambo ambayo yametokea katika miaka isiyozidi ishirini tu iliyopita? Ninapendekeza kabla ya kugusa kodi ya Mtanzania kila aliyebinafsishiwa kiwanda achunguzwe kwanza na akionekana kafanya ndivyo sivyo arudishe majengo, mitambo na vifaa vingine ili wanajamii chini ya uongozi wa nguvu ya umma waweze kuvifufua viwanda vyetu. Hatuwezi kukubali kuibiwa kila upande, juu, chini, kulia, kushoto na kadhalika, tutakwisha, tutasambaratika kama nchi.
Lazima tuwe na dhamira ya kukaa kuwa soko la wengine. Ndio tuagize tusivyovitengeneza, lakini tutengeneze vyetu navyo viende kwenye masoko ya nje.
Ni kukosa tafakuri na usononi wa maendeleo ya watu na nchi yetu, kuzungumzia nchi haina ajira za kutosha wakati majengo ya viwanda tulivyovijenga hivi leo yanatumiwa na wahuni wachache kufanya kile wanachokijua wao wenyewe.

Changamoto zinazobakia kwetu baada ya kutambua tumebinafsisha vilivyokuwa havistahili kubinafsishwa, ni kujipanga kimkakati na kuanza kuwa na visheni na dira mpya ya kimaendeleo. Mambo yatakayotulazimisha pamoja na mengineyo, kutokutegemea nchi za nje kwa mahitaji yetu yote. Na kilele chake kitafikiwa pale sisi kama taifa tutakapojenga uwezo wa kujitosheleza kwa vitu vyote vinavyohitajika kila siku au mara kwa mara na hususan katika uzalishaji mali, usafiri na huduma mbalimbali. Bila hivyo, ndege ya maendeleo ya Tanzania haiwezi kutembea kwenye 'runaway' achilia mbali kuruka juu. Viongozi watainigia, watatoka, wataingia -watakula na kuondoka na nchi itabaki palepale kimaendeleo au kiumaskini!