Tuesday, November 8, 2011

Muungano kama hawa

Kitupu changu kibaba, japo ninaitwa baba,
Wanangu wananikaba, njaa yawapa adhaba,
Nimemlilia toba, naisubiri ratiba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?



Muungano ni mahaba, au kula na kushiba,
Kiwapi changu kiroba, nyumbani nikakibeba,
Abu, kazi ya bawaba, na mlango haujashiba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?

Jua njaa yake tiba, si dawa ila kushiba,
Iwe Dovya au Goba, waitaka hii tiba,
Hawaishi kwa ghiliba, utawaumbua msiba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?

Hata uvae majuba, njaa haina haiba,
Kwa kila mtu ni mwiba, kuzidi kuuziriba,
Na ukizikosa raba, donda huzidi mraba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?

Unguja si kama Pemba, Tanganyika si kisiwa,
Kukunana ni habiba, kibaba mpe kibaba,
Hukurubisha nasaba, na kuchipuka mahaba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?

Kazi wote kuzibeba, kubanana na kukaba,
Kutegea si haiba, husababisha msiba,
Wengine hawali riba,kuwaepusha ni toba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?

Kuukuza uswahiba, lazima wote kushiba,
Tuzieupuke kadhaba, na nyufa kuja ziziba,
Wafanye kazi ngariba, kutahiri waso hiba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?

Namshukuru Hassaba. hesabu mwenye kutamba,
Atwepushe na ghiliba, ukweli ziwe hutuba,
Pasiwe wanaoiba, wakakwaza ukuruba,
Muungano ni mahaba, au kula na kushiba?

Kina kabla ya uhuru

Hawa ninawaambia, kabla walozaliwa,
Uhuru kuingia, Tanganyika na Zanzibar,
Tuwatunuku hidaya, ila kuongoza baa,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!



Mtakuwa ni raia, haki zote mtapewa,
Ila kutusimamia, hilo tunalikataa,
Nchi mmeifumua, kushonwa inatakiwa,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

Vijana wanatakiwa, kompyuta kuzivaa,
Ofisini wakikaa, wajua yanayotokea,
Mizubao na sinzia, kuondoka ni huria,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

Twataka wanaojua, uchumi kuutibia,
Isiwe tunaugua, malale na kusinzia,
Hoja kuzichanganua, miradi ije tufaa,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

KazI mmeshatufanyia, nchi ni kutuachia,
Ushauri kuutoa, pembeni mmesogea,
Nasi tutawachambulia, Tanzania kuja paa,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

Wenyewe kujichagua, bila jina kwangalia,
Ujuzi umejaliwa na kazi unaijua,
Ndani utajaingia, ufanye ya manufaa,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

Barabara kujijengea, hatua tutazichukua,
Reli kukarabatia, msaada si ruia,
Na umeme kusambaa, hiyo kazi ya siku moya,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

Maji tutawamiminia, maziwani kuyavua,
Mito tutajihamia, yazidi maji kujaa,
Na misitu kuridhia, wananchi kujilindia,
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

Ardhi hatutaigawa, kwa wageni bila ubia,
Hati tutatishikilia, hadi kijapo kiyama,
Nani wa kutununua, na sisi wote wazawa?
Kina kabla ya uhuru, baibai mnapewa!

Kuiba kura mauaji

eri wa mali ni mwizi, wa kura ni muuaji,
Haki anaidarizi, kumpa aso na mji,
Ni msanja wa kunazi, haubebi hata maji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!



Anamzidi jambazi, kura anayezifoji,
Si mthamini kizazi, huyu wa wazi mkabaji,
Anajal imatanuzi, na ukubwa kuuhiji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!

Hana radhi ya mazi, huyu ni mgeuzaji,
Na kinyesi na ushuzi, kwake yeye upambaji,
Ukilifanya fumanizi, usiache utekaji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!

Ni gunia la viazi, lisilo na mbebaji,
Kunyanyuka haliwezi, hadi aje mchukuaji,
Ni chombo kisicho kazi, kutupwa ni mataraji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!

Tabia yake ushenzi, hata ikiwa ya jaji,
Huuzwa kwa manunuzi, haki tusijeitaraji,
Ni mbegu za maangamizi, hazifanzi uokoaji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!

Havistahi makuzi, ni kama mnenguaji,
Kiuno bila shimizi, ndio chazidi kuchaji,
Na ya jana sio juzi, hautaivaa beji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!

Kibirizi, kibirizi, mlinzi na mauaji,
Hili ni kama jinamizi, kuponya linahitaji,
Na usalama si wizi, kama hivyo hatuuhitaji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!

Utu sio sisimizi, watu viumbe hojaji,
Usitumiwe kama ngazi, kesho haitakufariji,
Kama umekosa kazi, kwingine tafuta mtaji,
Kuiba mali ni wizi, kuiba kura mauaji!

Siasa na umafia

Yabadilika dunia, na ujanja unakua,
Ili kutokudhaniwa, jambazi polisi hua,
Vigumu kutuhumiwa, wadhifa anaopewa,
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'



Padri ukishakua, nani atakudhania,
Zinaa ukiingia, na uchafu kukujaa,
Wengine watashukiwa, salama utabakia,
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'

Ustadhi ukishakua, mcha Mungu wakujua,
Uovu ukipania, gizani hawatajua,
Siri utajifichia, hadi zizidi tamaa,
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'

Na siasa nazo pia, upupu zinachukua,
Fikra zazidi via, nani anayefikiria,
Roboti utadhaia, wanayozungumzia,
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'

Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'
Watu wasio ulua, fani wameivamia,
Kuiba waazimia, ni nani atawajua ?
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'

Uongozi wakikwaa, ganzi wameshajipatia,
Mbwa mwitu hujavaa, ngozi ya kondoo mliwa,
Kundini wakishaingia, kazi yao kutanua,
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'

Wanono watajilia, tena kimya kimya,
Hakuna atayejua, hadi mtu kufichua,
Ila taifa huvia, na kuzidi kusinyaa,
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'

Na vyama vyajatokea, udokozi kuulea,
Hazina kujaingia, kila kitu kupakua,
Pasiwe cha kubakia, ilo mifupa masalia,
Watu kinachoibia, si chama hao 'mafia.'

Monday, November 7, 2011

Vyama vya kisiasa Tanzania vimepitwa na wakati ? Sehemu- I

MABADILIKO yanayotokea duniani yanawawia vigumu vikongwe wa kisiasa kuyaelewa na kuyatafsiri katika mtazamo na macho ya ulimwengu wa sasa. Kama ilivyo kawaida kwa mwanadamu hatua za kwanza wanazochukua ni kupambana ili kuzuia mabadaliko hayo yasijiri makwao.


Haijawahi kutokea katika nchi yoyote ile duniani kwa mabadiliko makubwa ya kisiasa, kiuchumi na kijamii kufanyika kirahisi na bila kuwa na upinzani mkali, mkubwa na wa kutisha toka kwa wattu waoga, mbumbu, wasiojua kinachoendelea, wanaonufaika na mfumo wa hali iliyopo au wale wanaotumiwa na wanaonufaika kuwalinda wao na mali zao.


Ninasema vyama vya siasa Tanzania vimepitwa na wakati kwa sababu kile kilichozoea ukiritimba wa mfumo wa chama kimoja kinajiendesha kama wito na kazi yake kuu ni kupambana na wale wanaotaka kife; wakati wale wa iwezekanayo kuwa serikali mbadala na katika mfumo ambao si tofauti sana na wa chama kimoja katika mambo mengi, wanajiendesha kama vile kazi yao kubwa ni kuja kuingia madarakani kwa udi na uvumba. Hakuna kati yao ambaye anatoa uzito stahilifu kwa matatizo na changamoto za wananchi. Na kwa maana hii sio tu ninaona vimepitwa na wakati bali ninadhani vyama vyote havistahili hata kuwepo na nchi imekosa tu watu wanaoweza kuthubutu kuvifagia pembeni hata kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

Mabadiliko ambayo Tanzania inastahili kuyafanya hivi sasa hayana tofauti kwa namna yoyote ile na mabadiliko mengine kama hayo yanayotokea kwingine duniani na yaliyokwishatokea pengine na katika karne nyingine huko nyuma yetu.

Tofauti tu iliyopo hivi sasa ni kuwa sisi kama watu mmoja mmoja na kitaifa hatujajipanga ipasavyo kuweza kuhakikisha kuwa mabadiliko hayo yanatokea kwa faida na manufaa yetu na sio kwa ujibari, ujivuni, kisirani na hasara kwa upande wetu.

Na katika hili kiongozi mkuu wa kujipanga kuyakabili mabadiliko anatakiwa awe ni chama cha kisiasa cnenye viongozi wanaojua watu wanataka kuelekea wapi, nchi inaelekea wapi, duniani inaelekea wapi, nani wanastahili kuwa rafiki zetu na nani hatustahili kuwaamini, kuwathamini na kuwaingiza katika siri na mambo yetu mengine.

Ni chama kinachostahili kuwa na mipango, mikakati, sera, muundo, mfumo, taratibu na kanuni za utekelezaji zinazokipa chama ukuu na nguvu juu ya mwanachama mmoja mmoja au kundi la wanachama fulani ndani ya chama husika katika mustakabali wa kujenga umoja wa chama lakini ndani ya mfumo wa demokrasia hai na inayofanya kazi. Ugonjwa wa 'ndivyotunavyofikiri' ukiachiwa kutambaa kwenye mwili-siasa wa jamii hivi leo ni dhahiri maradhi makubwa zaidi yatajitokeza na kupona kwa mgonjwa kutahitaji manabii na miujiza.

Ni chama ambacho kina 'visheni' na 'misheni' bayana ambazo wanaokiongoza hata wakikurupushwa usingizini wanavikariri bila kukosea hata neno moja.

Ni chama kinachotakiwa kuwa na mizizi yake vijijini zaidi kwa kukivewezesha vijiji na wanavijiji na sio mjini kwenye watu wachache na walioelimika vya kutosha. Ni chama ambacho ofisi zake vijijini vitakuwa ni vituo muhimu katika kazi zake mbalimbali na ofisi ambazo zina nafasi kwa ofisi za viongozi wa wilaya, mkoa na kitaifa na ukumbi wa mkutano ambao vikao vikubwa kwa vidogo vya chama vinaweza kufanyika huko bila wasiwasi na uwepo wa sehemu kama hiyo kuwa ni hamira au chachu ya maendeleo ya kijiji na wanakijiji husika.

Ni kawaida pia kinachopingwa, kupinga na kupambana na kile kinachokipinga. Lakini kwa jambo lolote ambalo wakati wake umefika ni muhali na kazi bure kulipinga. Ima-fa-ima lazima mabadiliko yanayopaswa kufanyika yatafanyika tu.

Ili kutopotezeana muda ni vyema kufunguana macho na kuhamasisha jamii kufagia yale yote yenye kunukia uzee au ukongwe usio na faida na ambayo yanaweza kusababisha kuvunjika kwa amani na umoja katika nchi hii eti tu kwa kuwa ukongwe huo unakataa mabadiliko yasitokee.

Hali ilivyo sasa ni kwamba wanasiasa waliopo wamezoea kutawala kwa kutumia mabavu na maguvu; udikteta na ukiritimba katika maamuzi na uendeshaji vyama; kusukumiza kwenye makoo ya raia zao katiba na sheria zisizokubalika; kupora mamlaka na madaraka ya wananchi kinyume na katiba; kutumia njia za haramu kupata mapato yao na ya chama; kutumia vyombo vya dola kwa faida na maslahi yake; uzaini na uongo; kununua na kuwatumia watu; kugawa na kutawala; kulea ukabila wa kichama kwa maana ya kuwabeba tu wanachama wa chama tawala kuwa viongozi na kuwaacha wasio wanachama bila kazi wala changamoto za maana katika kuendeleza wilaya au mkoa au taifa;

uroho, choyo, inda na ulafi wa hali ya juu kutaka kutawala hata pale chama husika kisipokuwa na sapoti ya kutosha; kutumia vyombo vya usalama vya taifa kwa matumizi binafsi na sio kwa maslahi ya kitaifa; kutumia vyombo vya habari kukwamisha uwazi na kudanganya badala ya kusema ukweli; Viongozi wasio na mwelekeo wa kuinufaisha nchi hii na watu bali zaidi wao wenyewe na watu wa nje, kutumia makundi ya kijamii kama vile wanawake, vijana, wazee, wazazi, wanavijiji, wanafunzi, walimu, wafanyakazi na kadhalika kwa manufaa yao na sio ya kitaifa au ya umma; kuwatumia waandishi habari kama askari wa kukodiwa kufanikisha malengo yao; kushirikiana na mafisadi na wevi kufanikisha malengo ya kichama; kuingiza udini na ukabila katika uongozi na uanachama; kutumiwa na viongozi wa nje wa serikali na makampuni kwa maslahi yao na sio ya Watanzania; kushindwa kujenga imani na kujiamini kwamba kwa kutumia rasilimali zetu wenyewe tunaweza kunufaika zaidi kuliko kudanganywa kwa misaada toka nchi za nje ambayo ni sawa na mtu kupewa perememde wewe ukaibiwa kipande cha almasi au vito vingine vyenye thamani.

Mlolongo huo hapo juu ni ushahidi tosha unaonesha ni kwa kiasi gani vyama vya kisiasa nchini Tanzania vimepitwa na wakati na vinahitaji kufa au kupona 'kusasaishwa' ili sio tu viende na wakati bali viweze kutekeleza kwa ukamilifu na usahihi zaidi majukumu yao ya kisiasa, kijamii na kitaifa.

Ili kwenda na wakati vyama vya kisiasa vinastahili pamoja na mambo mengine kuwa na wanasiasa wasioshindwa na wasiotishika katika kutumia nguvu ya hoja, uchanganuzi, uchambuzi na ubunifu katika kuongoza na wanaostawi katika kutofautiana kimawazo, kifikra na kimaono.

Lazima kila chama kihakikisha kuwepo kwa demokrasia na uhuru wa kuchagua au kuchaguliwa ndani na nje ya chama; kuruhusu kuwepo kwa katiba na sheria zilizoandikwa na wanachama au wananchi wenyewe na sio wao kama viongozi au watawala; na pia kutumia njia za halali na zinazokubalika na zisizowaumiza watu wengine kupata mapato yao na ya chama.

Ni wajibu wa chama chochote ndani au nje ya madaraka kuvhiheshimu, kushirikiana na kuvitumia vyombo vya dola kwa faida na maslahi ya umma na si watu wachache; na kujali usawa, haki na ukweli wakati wote.

Kila chama kinastahili kuthamini utu na ubinadamu wa raia wote; kujenga umoja katika tofauti za kiimani na kiitikadi; kukana na kuharamisha ukabila wa aina zote ukiwemo ule ukabila wa kichama, udugu, ujamaa na urafiki katika kazi na majukumu mengine ya kitaifa.

Chama lazima kidhibiti wakati wote uroho, choyo, inda na ulafi miongoni mwa wanachama na viongozi wake; kuwaachia wengine kutawala pale chama kisipokubalika na wakazi husika; na kutotumia vyombo vya usalama wa taifa kwa maslahi, matakwa na haja binafsi ikiwemo kuwachunguza viongozi wastaafu, wanaharakati na wanachama na viongozi wa upinzani.

KIla chama kinawajibika kutotumia vyombo vya habari kudanganya wale wenye uelewa duni wa mambo; kutowaweka waavijiji katika giza la kuelewa na kukubali kuwa demokrasia na vyama vingi ni jambo lenye manufaa kwetu kama nchi na watu; na pia kutowatumia waandishi habari kama askari wa kukodiwa kufanikisha malengo ya chama na viongozi wake.

Chama kinawajibika kutoshirikiana na matajiri na mafisadi katika kupora madini na maliasili za nchi hii; kutowagawa Watanzania katika makundi ya kijamii yanayoweza kuja kuwa hatari kwa taifa baadaye, k.m, vijana, wazee, wanafunzi, wanawake, wazazi wa chama fulani n.k.

Chama kiwe makini na kutoingiza udini na ukabila katika uongozi na uanachama; kutotumiwa na viongozi wa nje wa serikali na makampuni kwa maslahi yao na sio ya Watanzania; kufanikisha kujenga imani na kujiamini miongoni mwa Watanzania kwamba kwa kutumia watu wetu wenyewe, wazungu wasio na ajira makwao, rasilimali zetu wenyewe tunaweza kunufaika zaidi kuliko kudanganywa kwa misaada toka nchi za nje ambayo ni sawa na mtu kupewa perememde wewe ukaibiwa kipande cha almasi au vito vingine vyenye thamani na wewe ukaridhika na kuona ndiye uliyefaidi kuliko aliyefaidi kikweli.


Chama cha kisiasa sahihi na kinachostahili kuwepo katika karne ya 21 nchini Tanzania ni kile kitakachoweza kufanya mikutano yake mikubwa na midogo, kwa siku kama sio wiki kadhaa, katika kijiji chochote, mkoa wowote Tanzania kwani mikoa na vijiji hivyo vitakuwa na serikali na utawala bora unaoweza kukimu na kuruzuku mambo hayo kutokana na kuwezeshwa na chama husika na wafuasi wake na watu wengine wanaozingatia misaada kufika kule inakotakiwa na sio vinginevyo..

Vyama vya kisiasa Tanzania vimepitwa na wakati ? Sehemu- II

Ili 'kuvisasaisha' vyama vya kisiasa Tanzania kuna mambo kama 15 hivi yanayostahili kufanyika. Mambo hayo, yakiwemo hayo machache yaliyogusiwa hapo juu ni pamoja na mabadiliko ya miundo; mifumo kazi; uwakilishi mikoani na matawini; kuwa na wanachama hai; kuwa na vyanzo halali vya mapato; elimu isiyokoma kwa vingozi na wanachama; matumizi ya Teknohama; kutumia sayansi ya logistiki; kuwa na mipango na mikakati ya kisasa; kuwa na mbinu za kunufaika na kutohasirika na mahusiano ya kimataifa na utandawazi; kubuni njia bora za kupata viongozi; mafunzo ya menejimenti, uchumi na maarifa muhimu kwa viongozi; namna mpya za kukabiliana na matatizo na changamoto za wafuasi na wananchi kwa ujumla; na jinsi ya kuwa mwendelezaji, mwekezaji na mshiriki katika kuzitumia fursa za kimaendeleo za kiuchumi na kijamii kuanzia ngazi ya chini ya tawi hadi ya juu kitaifa kwa faida ya nchi nzima na watu wake.

( Makala haya yanauzwa; wasiliana nasi kupitia SMS : +255714265218 wakati wowote na uapata majibu chini ya saa 24.).......

Sunday, November 6, 2011

Tukubali ushoga au tuachane na nchi za Magharibi ?

ZIPO habari kwamba serikali ya Uingereza iko mbioni kuandaa utaratibu ambao nchi zinazokataa 'ushoga' , kwa maana ya mwanamme kujigeuza mwanamke na kuwa na haki ya kuolewa na kuwekwa ndani kama mke, zitakuwa zikinyimwa fedha za jamala ambazo kwa Waafrika walio wengi sio msaada ila ni sawa na kurudisha kile ambacho Waingereza na ndugu zao walikwiba, wanakwiba na wanaendelea kukwiba toka kwa Watanzania na Waafrika wengine kupitia ukoloni, ukoloni mambo leo na unyonyaji mkuu wa kibiashara na kiuchumi kimataifa.


Mama wa demokrasia duniani, Uingereza, anataka kwa mabavu kupandikiza ushoga katika nchi za Kiafrika ikiwemo Tanzania kwa kuwazaini Waafrika kwa pipi na shanga kama ilivyokuwa zamani wakati makampuni yake hayachoti tu dhahabu na madini yetu mengine bali pia hata fedha zetu kidogo zilizo katika hazina yetu.

Uingereza ndio nchi iliyoitawala Tanganyika tokea ilipomshinda Mjerumani ikisaidiwa na rafiki zake mwaka 1918-1961 bila kufikia hata nusu ya mafaniko yaliyofanywa na Mjerumani katika miaka yake 30 hivi ya kuitawala Tanganyika. Lakini ndiyo iliyofanikisha kujenga unyonyaji wa hali ya juu wa nchi hii, hadi hii leo ikiwmo kasumba ya viongozi na matajiri wetu kuwapeleka watoto wao kwenda kusomeshwa Uingereza.

Hili hata hivi linatufungua macho Watanzania kwa kutambua kwamba serikali ya Uingereza na Jumuiya ya Madola ni kama vile zinaamini kwamba zimeziweka mfukoni nchi maskini za Kiafrika na kwamba zinaweza kutumia udikteta kufosi kwenye makoo yao chochote kile wanachokitaka wao kwa kuwa ni matajiri na watu wa nchi zetu kwa kuwa maskini wakakubali kirahisi tu.

Hili huwa linawezekana kwa sababu Uingereza na Marekani huwa linawatumia watu waliosoma au kufanya kazi kwao kuja 'kuunyakua' uongozi wa nchi sio kwa sababu nyingine ila kuendeleza maslahi ya Uingereza na Marekani katika nchi husika. Katika wimbi la demokrasia katika nchi zetu hivi sasa tuwe macho sana na viongozi wa kupandikizwa kwa sababu ya nguvu ya fedha. Watu hao kwa kawaida hutumwa na mabepari wa dunia ambao ni kama asilimia 1 tu ya watu duniani kuja kukwiba utajiri wenu kwa kuunda genge la asilimia 0.005 ya mabepari na wanasiasa matapeli ndani ya nchi husika.

Kwa wasiojua dunia ya ubepari tuliyoikaribisha Tanzania ni mfumo ambao unaendeshwa na asilimia 1 tu ya matajiri duniani lakini ulio na sauti na nguvu sio tu juu ya serikali zao bali pia serikali za nchi zinazoendelea ambazo huzitegemea nchi zao. Asilimia hii moja ndiyo inayoipa nguvu asilimia nyingine kama 15-20 za mabepari wa kati wanaokuja kuwekeza katika nchi zetu na kuwanu nua viongozi na matajiri wachache nchini (labda asilimia 2-3), ili kudhulumu asilimia 97-98 ya raia wenzao kwa heri na shari.

Katika hili, mimi sina tatizo hata kidogo kuona wanawake, wazee, vijana, wafanyakazi, wakulima na makundi mengine katika jamii yakifanya uamuzi ya kuandamana na kuwapasha Waingereza na Wamarekani na wenzao kama wao kwamba hatutaki na hatukubali ushoga katika urithi, desturi, utamdauni na mila zetu za Kiafrika hapa Tanzania na kwingineko Afrika.

Ushoga kwa wale wanaoamini katika Quran Tukufu na Biblia ndiyo mambo yaliyosambaratisha nchi za Sodom na Gomorrah. Wakati kuna dalili za Marekani na nchi za Ulaya kuwa katika masahibu ya kila aina, zipo hisia kwamba Waingereza wanachotaka kukifanya ni sawa na mtu anayezama kutaka kufa na wale wanaoweza kuwasaidia na wanaotaka kumuokoa.

Ni kichekesho kwa Uingereza kuwa na msimamo kama huu katika karne ya 22, kama vile bado tupo kwenye karne za 19 au 20.

Inaonekana kama vile Uingereza na nchi nyingine tajiri bado zinaamini kwamba nchi za Kiafrika ni nchi zinazoongozwa na watu ambao uroho na tamaa yao ya misaada vinaweza kuwafanya wakubali lolote lile hata likiwa baya kwa mila, desturi, imani, utamaduni na utu wa watu wao.

Hivi leo uchumi wa Ulaya na Marekani upo kwenye misukosuko sio kwa sababu nyingine bali kwa sababu ya uchumi kukosa haya na aibu au kile kinachoitwa, 'economics without ethics', uchumi bila maadili. Na misaada toka nchi hizo nazo sasa inataka kugeuzwa kuwa ni 'aid without ethics' au misaada bila maadili. Vitu hivi tusivikubali. Na huu ni wakati wa kuwashauri Wazungu kuanza kitu kitakachoitwa uchumi na misaada yenye maadili kama masomo katika shule zao za viongozi na hasa wale wa kimataifa. (Ethiconomics na aideconomics) ili watuelewe na kutufahamu zaidi. Umaskini hauimanishi maskini kukubali kuuza roho, utu na imani yake kwa ajili ya kupewa misaada.

Lakini ni ajabu pia kwa sababu hivi sasa nchi za BRIC-Brazili, Russia, India, Uchina na bila kusahau nchi za Kiarabu, zile zilizokuwa katika ile iliyokuwa ikiitwa Urussi ya zamani, Malaysia, Indonesia, Korea Kusini, Vietnam, Japani na zile za Scandinavia nazo zinatuhitaji zaidi kuliko wao wanavyotuhitaji.

Ili kuwafunza jamaa hawa ningelishauri nchi za Kiafrika kama zilikuwa zikiwapa fursa 8 kati ya 10 Waingereza na wamarekani nchini mwao, sasa zigeuze kibao na kuyapa mataifa haya mapya na yanayokuwa kwa kasi zaidi asilimia 80 ya biashara, uwekezaji na ushirikiano kati yao na kuwabakizia wakongwe Uingereza na Marekani asilimia 20 tu, ili vitisho vyao viwe kazi bure huko tunakokwenda.

Mambo yetu Waafrika kwa kiasi kikubwa yameharibika kutokana na ukaribu na kukubali bila kujiuliza tamaduni za nje, hususan, za Kiingereza na Kimarekani. Ni dhahiri kwamba tungelikuwa tunaujali utamaduni wetu wenyewe na tukashirikiana zaidi na zaidi na nchi tofauti na hizi mbili, hivi leo labda hadithi ya Afrika isngelikuwa hii iliyopo hivi sasa.

Ni nchi za Magharibi na hususan Uingereza, Ujerumani, Ufaransa, Italia na Marekani ndizo zilizochangia na zinazoendelea kuchangia kudhoofisha utu, utamaduni, imani na udugu wetu kwa sababu wanazozijua vizuri kuliko sisi wenyewe. Kutokana na umaskini wetu tumeendelea kuwaganda huku wanatunyonga taratibu.

Huu ni wakati muafaka kwa viongozi wa dini na wafuasi wao nao kuja juu kiddedea na kuwaonyesha mabwana na mabibi zetu wa zamani kwamba Tanzania ya leo sio ya jana na sio nchi ya kuichezea tena!

Viongozi wa dini watumie fursa hii kuzungumza moja kwa moja na walipa kodi wa Uingereza wakiwemo Wakiristo, Waislamu na Wayahudi kuwaomba washinikize serikali ya Uingereza kuachana na wazo la kuinyima Tanzania msaada kwa sababu Tanzania haitakubali ushoga achilia mbali watu wa jinsia moja kufunga na kufungishwa ndoa.

Wakati huohuo, vyama vya siasa nchini hapa na vile vya Uingereza vianzishe vuguvugu la kudai demokrasia katika utoaji misaada na kuheshimiwa kwa haki za nchi maskini katika kulinda utu wa watu wake na mila na utamaduni wao.

Enzi za Uingereza na Marekani kutoa masharti ya kisenge na kiudhalimu kwa Waafrika ninaamini zimepita. Hivi sasa Afrika ina nafasi ya kuchagua na kukataa masharti ya kijinga na yanyochimbua mizizi na kuusambaratisha mashina yake ya utu na utamaduni wake bila sababu ya msingi. Kufuatia ujibari, jeuri na kiburi cha Marekani na Wayahudi, ingekuwa jambo zuri kama nchi za BRIC na marafiki wengine tajiri wa Afrika, zingeingilia kati na kuliziba pengo la bajeti ya UNESCO, kama Marekani itajitoa kuifadhili UNESCO eti kwa sababu Palestina imekubalika kama mwananchi kamili.

Kama mataifa haya makubwa yanaamini kweli katika demokrasia hayawezi kuwalazimisha viongozi wetu kufanya maamuzi kwa niaba yetu. Maana kufanya hivyo ni kuwafunza udikteta viongozi wetu.

Isitoshe baadhi yetu katiba zetu tayari hazikubali ushoga. Je, kwa masharti hayo ya Waingereza hawaoni moja kwa moja kwamba sio tu wanataka kuingilia sheria na katiba yetu, bali pia wanaonyesha dharau kwa serikali na watu wetu ya hali ya juu kabisa.

Wanachostahili kufanya mabwana hawa ni kuwezesha nchi zetu kuwapa fursa wananchi wao kupiga kura ya kukubali au kupinga kuingizwa au kulazimishwa kuufanya halali ushoga nchini mwao.

Kwa jinsi serikali yetu inavyojikuta mchafukoge katika masuala kama ya mkorogo katika suala la huduama za umeme, maji, afya na tiba, ustawi wa jamii na usafi; migodi na madini; ufisadi, EPA na wenzake; mawakala wanavyotumbua na kadhalika na tunavyoambiwa kuwa wanaCCM wenyewe hawaoni mtu wa kupambana na ufisadi ndani ya chama hicho hatujui ni kwa kiasi gani tunaweza kuwa na viongozi watakaoendelea kuonyesha ubabe na ufidhuli kwa wale wanaotutaka tuwe mashoga na wasenge katika dunia hii ieleekeayo kwenye maangamizi ya Sodom na Gomorrah.