KAMA jiji hili ambalo ndilo lenye Ikulu na wizara na idara zote muhimu nchini linataka liondokane na uchafu, harufu mbaya mpaka misikitini na makanisani, kinyesi kinachozibuliwa wakati wa mvua barabarani na mandhari za kuchukiza sasa ni wakati wa kuirudisha kazi ya usafi wa jiji kwa wanajamii kwa kiasi fulani badala ya kutoa tenda na kukodisha mchakato wote kwa watu wasio na uwezo na wasiokidhi mahitaji na matakwa ya usafi wa jiji hili.
Serikali kuu na serikali za mitaa zitatakiwa kutoa ushirikiano maalum ili kufanikisha azma hii.
Tofauti na mambo mengine, ningelipendekeza kazi hii ipewe umuhimu wa juu hata machoni kwa watu wa nje wanaotaka kuisadia nchi yetu katika masuala ya utunzaji mazingira na usafi.
Kinachopendekezwa hapa ni kuachana na utitiri wa magari na matrekta mabovu katika kazi ya kukusanya na kusomba taka kuzipeleka huko zinakotupwa. Badala yake kutoa ajira pana na za kudumu kwa kina vijana wetu wenye matoroli, maguta, pikipiki, vipawatila, bajaji, mikokoteni na wilibaroo kufanya kazi ya kukusanya taka mitaani na kwenda kutupwa kwenye eneo maalum litakalokuwa na shimo kubwa la kutupwa taka zilizotenganishwa kiaina na kiufundi na kisha kuchakatwa hadi kuzalishwa bidhaa mpya inayoweza kutumika majumbani, viwandani na mashambani.
Umuhimu wa serikali kuu na serikali za mitaa ni katika kupatikana kwa maeneo maalum ya kuchimbwa mashimo hayo mitaani au kwenye kata; ujenzi wa miundo mbinu rahisi ya kukokotosha taka kuwa bidhaa hitajika; kuwaandaa vijana kimafunzo tayari kwa kazi za kutenganisha taka na kuzibeba kwenda kwenye maeneo husika; na kuhakikisha bajeti ya usafi toka serikalini na misaada ya wafadhili inaelekezwa kwenye mambo haya badala ya kuliwa na wajanja wachache huko walipo.
Italazimu pia kwa viongozi na maofisa wote wa jiji na katika wizara husika, ambao wameomba kupewa hisa na chochote na wawekezaji katika miradi mipya tarajiwa ya kurejelea taka kupewa ruhusa maalum na serikali kuu ya kuwekeza kwenye makampuni bila kutoa chochote !
Aidha wanajamii kwa kushirikiana na serikali kuu na za mitaa watapaswa kuwa na kisima cha maji kilichochimbwa kwenye eneo au kina ambacho maji hayakauki kamwe ili kuhakikisha mji unakuwa na mandhari nzuri na ya kuvutia wakati wote. Maji hayo pia yatatumika kusaidia kazi za kupooza na kulainisha bidhaa katika kituo kikuu cha kubadili taka kuwa mali na utajiri. Ndoto ya kuwa na mifumo mizuri ya kuvuna mvua itakuwa ziada ambayo si mbovu katika hili.
Kila nyumba italazimika kupatiwa pipa pacha nne au kwa maneno mengine pipa ambalo lina sehemu nne: moja kwa ajili ya kutupwa chupa na glasi: la pili kwa ajili ya kutupwa karatasi: la tatu kwa ajili ya kutupwa mabaki ya vyakula na la mwisho kwa ajili ya kutupwa taka ambazo ni hatari kwa afya ya binadamu na taka mchanganyiko nje ya hizo hapo juu.
Vijana wakusanyaji watafunzwa jinsi ya kuzihamisha taka hizo toka mapipa hayo kwenda mifuko maalum ambayo itachukua taka kwa mpangilio huo huo huo na kuzipeleka kwenye kituo kikuu cha taka kwenye mtaa au kata kwa ajili ya kurejelewa upya kuzalisha kinachowezekana kuzalishwa.
Zitakapofikishwa kituoni hapo taka zitakuwa tayari zimetenganishwa kwa utaratibu huo hapo juu na hivyo kuingizwa kwenye moja kwa moja kwenye eneo zitakazofanyiwa kazi ili kuzalisha umeme au kutoa bidhaa fulani itakayotumika kama bidhaa mpya tena madukani au sokoni. Mabaki ya vyakula yanatarajiwa kutengenezwa kuwa mbolea asili isiyo na dawa yoyote ambayo itauzwa kwenye mifuko maalum kwa wakulima na watunza bustani.
Watumishi wizara ya ardhi wataaswa kwamba ili kuleta uwiano kati ya klutenda dhambai na mema- nchini ni muhimu kwao pamoja na kuuza maeneo wazi kwa mabwanyenye wetu wapya, sasa kutoa maeneo kwa ajili ya uchimbaji mashimo makubwa ya uhifadhi wa taka zitakazochakatwa na kuwa bidhaa mpya au kuzalisha umeme kwa ajili ya faida ya wakazi walio wengi jijini.
Wataalamu wa vyama vya siasa vyenye vijiwe mjini wataombwa wautumie utaalamu huo ili kugeuza vijana wetu toka 'majoblesi alwatani', wababaishaji na kupe wenye sifa za kimataifa kubadilika kwa kukopeshwa mitaji ya kununua toroli, maguta na vifaa kama hivyo ili kuwa wakusanyaji na wabebaji taka watakaoipa heshima mpya jiji la Dar es salaam.
Wataalamu wa kupiga raia mabomu, kuvunja maandamano na mikutano wataombwa kuutumia utaalamu wao ili kuhamasisha kazi ya usombaji taka kila wakati ili pasiwe na taka hata moja mahala popote jijini kwa kasi ile ile ya upigaji mabomu ya machozi wakati wa maandamano ya upinzani, wafuasi wa dini fulani au wafanyakazi au wanafunzi.
Mameneja wa migodi wataaombwa kuazimisha magreda na makatapila kuja kuchimba mashimo hayo katika mitaa au kata mbalimbali jijini kama walivyofanikisha zoezi la uchimbaji mashimo huko Geita, North Mara na Bulyanhulu,kutegemeana na kiwango cha uzalishaji taka katika maeneo husika.
Badala ya kuwa na magari mabovu yanayosafiri umbali mrefu kuokota na kutupa taka sasa vitoroli, mikokoteni, bajaji, guta na pikipiki zitatengenezwa kwa njia ambayo kwazo zitakuwa zikipeleka taka kwenye maeneo hayo yenye mashimo na miundo mbinu maalum ya kupokea taka zilizotenganishwa na kuanza kuzifanyia mchakato ili zitoe bidhaa za aina mbalimbali na kuzalisha umeme na vitu vingine vitakavyowezekanika.
Taka zinazohitaji kutupwa mbali zitachukuliwa na magari makubwa maalum machache lakini yenye kiwango cha kimataifa kwenda kutupwa mbali kabisa na makazi ya watu na wakati mwingine hata kwenda kufukia mashimo yaliyotokana na kuchimbwa madini yetu katika mikoa ya kaskazini na kusini.
Ukiutazama mtiririko huu mzima utagundua kuwa pendekezo hili lina shabaha ya kugeuza taka kuwa mali kwa namna kadhaa. Kwanza, vijana ambao wana tatizola ajira itabidi sasa wakimbie ajira wao wenyewe. Taka zitageuka fumba na kufumbua mali, maana kila mzigo kutegemeana na aina yake utakuwa ukilipwa fedha nzuri tu mara ukifika kwenye kituo kikuu cha kuchakata taka kwenye mtaa au kata.
Aidha magari mabovu ya kusomba taka amabyo wakati mwingine badala ya kusafisha mji huuchafua yatatoweka. Takataka hizo zitazaa bidhaa ambazo wafanyabiashara na wanunuzi watanufaika kwani zina uwezekano mkubwa wa kuwa za bei rahisi zaidi kuliko nyinginezo. Kisha mbolea itakayozalishwa itakwenda kuzistawisha bustani za Ikulu na Mnazi mmoja na maeneo mengine mjini na hivyo kulipa jiji mandhari ya kukata na shoka kwa uzuri wake. Hali kadhalika, sio tu tatizo la kukatikakatika umeme jijini litakuwa historia bali mradi huu utahakikisha hata nyumba mbavu za mbwa zilizo mabondeni zinapata umeme wa kutosha na wa uhakika kila siku.
Vilevile visima vitakavyoendana na mradi huu vitawahakikishia wakazi wa kila mtaa na kata upatikanaji maji masafi ya uhakika wakati wote, wakati wanasubiri maajabu yatakayofanywa na DAWASCO miaka mitano au kumi ijayo kama bado wako hai. Hili linawezekana, cheza nafasi yako na timiza wajibu wako. Miaka hamsini baada ya uhuru hutakiwi kushindwa na jambo hili.
Wakati ninaandika makala haya watafiti wanaonisaidia wameleta habari kwamba kuna watu tayari wameanza kujituma wenyewe na kuanzisha miradi kama hii. Kama hili ni kweli basi wilaya, mkoa na wizara husika zichangamkie mara moja jambo hili. NIna hakika likipata kuungwa mkono nao ni kitu kinachowezekana na kitakalolifanya jiji la Dar es salaam kuwa jiji la kuigwa na miji mingine sio tu Tanzania bali Afrika nzima.
lle tabia ya kujifanya kuwa serikali inaweza kufanya kila kitu si kitu kizuri. Na katika miaka hii ni kitu kilichopitwa na wakati na kuwazaini wananchi huku tukijua fika tunasema uongo. Kweli Watanzania hawana fedha, yaani, ni maskini. Lakini Watanzania wana kitu kimoja ambcho thamani yake wakati mwingine ni kubwa kuliko fedha. Kitu hicho sio kingine ila akili na nguvu zao. Pakiwa na uongozi unaoona mbali na mbele na unaojua kutumia akili na nguvu hizo na kuwekeza fedha kidogo Watanzania kama watu wengine wana nafasi ya kufanya maajabu mbalimbali duniani.
Friday, November 25, 2011
Thursday, November 17, 2011
Muswada wa katiba na hatima ya nchi yetu...
AKIZUNGUMZIA uwezekano wa kuandikwa katiba mpya ya Tanzania kwa mara yake ya kwanza, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye pia ni Mwenyekiti na mwanachama wa Chama kimojawapo cha siasa nchini Tanzania, CCM, Bwana Jakaya Kikwete pamoja na mambo mengine alionesha kutamani sana kwamba katiba itakayoandikwa iweze kutufaa kwa miaka 50 kama sio 100. Hata hivyo, kile kilichowasilishwa na Waziri wake wa katiba hakikufanana kabisa na matamanio mema yake hayo.
Tofauti na msimamo huu wa mheshimiwa Rais, muswada wa serikali yake kwa bunge la Jamhuri ulidhihirisha nia ya serikali ya Chama cha Mapinduzi kuitumia fursa hiyo ili iweze kujikita vyema zaidi nchini kwa halali au haramu kisiasa kwa kuwatumia wabunge wao ambao ilionekana kama walishapewa mafunzo maalum kuhusu kinachotegemewa kutoka kwao.
Pamoja na spika wa bunge hilo kudai kwamba wanaharakati, wapinzani na waandishi wa habari wanapotosha kilicho mezani mwa wabunge, kazi nzuri ya uchambuzi wa kina iliyofanywa na Mheshimiwa Tundu Lissu (CHADEMA) ilionesha kulikuwa na uwezekano mkubwa wa wabunge wa CCM kutokuwa wameusoma muswada huo na Tundu akawa anapigia gitaa mbuzi.
Pengine wabunge wa CCM walishaambiwa kwamba ni lazima upite kama ulivyo na hakuna aliyesumbuka kuusoma kikwelikweli, lakini baadaye ilidhihirika waziwazi kwamba muswada huo ulikuwa na udhaifu mkubwa na kasoro nyingi za kimaudhui, kisheria, kisiasa na kikanuni kikatiba ambao kwa watunga sheria makini lazima wangelihitaji muda wa ziada wa kuufanyia kazi na sio kama wenzetu walivyoanza kuchangia wakiwa na uelewa 'finyu kiuzalendo' kwa kazi iliyokwa mbele yao.
Sio siri kwamba CCM inachokitaka pengine ni kujihakikishia uzima wa milele. Kitu ambacho hakiwezekani. Na haitawezekana kwa sababu hizi si zama za Nyerere, Mkapa na Mwinyi na chochote kinaweza kutokea kwa watu ambao hali ya uchumi inawawia ngumu kila kukichwa, mali asili zao zinatwaliwa bure, watu wanauawa na kubakwa migodini na wakubwa wanapora fedha, wanyama pori, miti, ardhi na rasilimali nyingine kwa jinsi wanavyotaka. Na wasichonacho wananyang'anywa hata kile kidogo walicho nacho, wakati wenye nacho wanazidi kuongezewa kila siku.
Watanzania hawatakaa wasahau kwamba kunako mwezi Novemba, mwaka 2011 baadhi ya wabunge wao kupitia CCM walipoteza fursa ya kipekee katika kuutanguliza Utanzania mbele ya nafsi na uchama wao. Matokeo ya ubinafsi na uchama wao yakawapotezea fursa hii adhimu ambayo ingeliwaweka pazuri sana katika historia ya nchi yao na watu wake.
Kilichotokea ni kwa wabunge hao wa CCM-CUF kuonesha dhahiri kuwa ni mbwa-mwitu (wawakilishi wa chama na serikali) waliovaa ngozi ya kondoo (wawakilishi wa wananchi). Kipaumbele siku hiyo hakikupewa wananchi na vizazi vyao vijavyo bali chama, matashi yake na ubinafsi wa wabunge hata kama Watanzania kwa ujumla wao watapoteza kikubwa zaidi siku zijazo.
UCCM na UCUF kwa kiasi fulani katika hili umewafanya wengi waamini kuwa wabunge wa vyama hivyo wanastahili kupata shahada ya udaktari katika uchama, usisi, umimi na katika mapambano ya maslahi na maendeleo ya wabunge binafsi.
Kwa maneno mengine, wabunge wa CCM na CUF walikuwa wakituambia kwamba vyama vyao na uongozi wa chama chao ni muhimu kuliko Utanzania wetu au utaifa wetu, watu wetu na vizazi vyetu vijavyo.
Kubwa zaidi ni lile la spika, muwakilishaji muswada na wabunge wa CCM waliochangia muswada huo kusingizia eti kuna urongo, uzushi, upotoshaji na tafsiri mbovu ya kile kilichotakiwa kuwakilishwa. Haraka aliyokuwa nayo spika, wabunge wa CCM kuchangia na mwasilisha muswada na wenzake kuliacha maswali mengi kuliko majibu. Mwisho wa siku kilio cha spika, muwasilisha mada na wabunge wa CCM na CUF kilifanana na kile kilio cha mchunga kondoo aliyekuwa akisumbua wanakijiji wenzake kwa kupiga mayowe ya MBWA MWITU, MBWA MWITU kumbe yote ilikuwa ni mzaha kama sio urongo.
Uzaini wa CCM wa kujionesha eti wana CCM na viongozi wao wanaipenda na wana uchungu sana na Tanzania kuliko watu wengine umewafanya jamaa hao kuangukia pua katika siku ambayo wengi wao hawataiashau na wao wenyewe wameamua kujizika kihistoria.
CCM na wakewenza Unguja
Baya zaidi ni lile la muswada huo kudiriki kuifanya Zanzibar kuwa sawasawa na Tanganyika isiyopo katika kuamua hatima ya nchi yetu na watu wake. Hiki ni kitendo cha waendesha utumwa, kikoloni, kibabe, kihuni na cha kidhalimu ambacho hakistahili kukubalika.
Kwani nia ya kuwapa ukubwa huu Wazanzibari wasiostahili kuupata ni kurahisisha siasa ndani ya CCM kati ya Wazanzibari na Wabara. Kwa maneno mengine, CCM imediriki kuwauza Watanganyika kwa Wazanzibari, kama walivyouza migodi ya dhahabu, ili mradi tu mambo yao yawe safi.
Ukewenza Zanzibar na Serikali ya JMT, unatuweka pabaya kitamathali na kiuyakinifu kwa kiasi cha eti watu asilimia 2 Tanzania kuamua hatima ya asilimia 98 iliyobakia.
Kwa maneno mengine, muswada huo unawageuza Wazanzibar wakoloni na Watanganyika watawaliwa katika nchi yao wenyewe. Sijui hata kama muswada huo utapita kama hili litakaa likubalike kesho na keshokutwa.
Hadhi ya Zanzibar kiukweli haina tofauti na ya mkoa wowote bara. Tofauti tu ni kuwa mikoa inabanwa kuwa huru kisiasa, kijamii na kiuchumi kwa mafaniko yake makubwa na haraka zaidi. Kilichokosekana ni uamsho kwa wakazi mikoani na uadilifu kwa serikali kuipa mikoa serikali huru zinazosimamiwa na waziri mkuu wa mkoa, baraza la mawaziri wa mkoa na wawakilishi wa mkoa na mikoa mingi tu ingeiacha Zanzibar nyuma kimaendeleo, bila ya visiwa hivyo kuona hata indiketa za mikoa hiyo kwenye mbio za ustawi wa jamii na maendeleo ya mkoa.
Itakuwa ni jambo la fedheha kama wabunge na serikali yetu baada ya kushindwa kuafikiana na wapinzani wa kweli ndani ya bunge itakuja kufanza hivyo kwa kupata shinikizo toka Marekani na EU. Jambo hili litaonesha kwamba viongozi wetu hawajaiva wala kukomaa na hakika hawastahili kuiongoza nchi hii kama kweli tunataka kuendelea na umoja na amani tuliyo nayo hivi leo. Kinachoonekana hapa ni kwamba kuna Watanzania wenye akili na uwezo mkubwa tu lakini kwa kukosa uongozi adilifu na mzuri wanashindwa kuwatumia.
Viongozi wa dini
Viongozi wa dini kama ilivyokuwa kwa wenzetu nchini Kenya wana mchango mkubwa katika kuhakikisha Tanzania inakuwa na katiba nzuri na safi na itakayowafaa Watanzania kwa muda mrefu kuliko hii ya kupandikizwa ilivyotsukuma sukuma.
Yapo mambo kadhaa ambayo viongozi wa dini wanaowatakia Watanzania na vizazi vyao amani na umoja wanaweza kuhoji na kutoa mwongozo yaende vipi kwa faida ya watu wote. Mathalani, hivi leo kanisa katoliki linafanya vizuri sana katika elimu na sekta ya afya, lakini siasa za uziwi na upofu zinaweza kuhujumu haya yote kama katiba isipohifadhi sheria na haki muhimu za kulinda kanisa, mali zake na viongozi wake. Misikiti na Makanisa yakikaa nyuma, viongozi wa dini wasije anza kulalama baadaye kwamba katiba imewapendelea hawa, au kuwaonea hawa.
Makampuni na taasisi na katiba
Makampuni na taasisi kisheria ni sawa na mtu au raia. Makampuni na taasisi zikikaa nyuma na kutokushiriki kwenye mchakato wa katiba mpya yapo masuala mengi yanayoweza kuja kuzuka baadaye kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiutamaduni yakaya kuwa ni kwa hasara kubwa kwa upande wao.
Katika suala hili lal katiba mpya sisi sote ni wadau na washiriki na hakuna anayestahili kubakia kuwa mtazamaji tu au juu ya wenzake kwa namna yoyote ile.
Muswada huu kama ilivyokuwa kwa miswaada mingine dhaifu, inayovuja na dhalimu kwa wananchi na vizazi vijavyo, imedhirisha mapungugu mengi mengine katika muundo, mifumo na taratibu zetu za uongozi na uendeshaji nchi. Baadhi ya kasoro hizi ni pamoja na hatari ya kuwa na wabunge wa kuteuliwa badala ya kuchaguliwa kwenye bunge la kiwakilishi; jinsi ambavyo serikali iliyoko madarakani inaweza ikapora mamlaka na madaraka ya wananchi na kufanya mapinduzi ya kikatiba bila kuwajibishwa ipasavyo; muungano unavyozidi kuonekana kukosa maana kwa Watanganyika na kuwa mzigo usiobebeka; na ule ukweli kuwa nchi bado imo kizani na haijajaliwa kuwa na kiongozi na wanasiasa wanaoweza kututoa kwenye shimo refu la giza ambalo tumejikuta tumo leo.
Pepe: sammy.makilla@columnist.com
Tofauti na msimamo huu wa mheshimiwa Rais, muswada wa serikali yake kwa bunge la Jamhuri ulidhihirisha nia ya serikali ya Chama cha Mapinduzi kuitumia fursa hiyo ili iweze kujikita vyema zaidi nchini kwa halali au haramu kisiasa kwa kuwatumia wabunge wao ambao ilionekana kama walishapewa mafunzo maalum kuhusu kinachotegemewa kutoka kwao.
Pamoja na spika wa bunge hilo kudai kwamba wanaharakati, wapinzani na waandishi wa habari wanapotosha kilicho mezani mwa wabunge, kazi nzuri ya uchambuzi wa kina iliyofanywa na Mheshimiwa Tundu Lissu (CHADEMA) ilionesha kulikuwa na uwezekano mkubwa wa wabunge wa CCM kutokuwa wameusoma muswada huo na Tundu akawa anapigia gitaa mbuzi.
Pengine wabunge wa CCM walishaambiwa kwamba ni lazima upite kama ulivyo na hakuna aliyesumbuka kuusoma kikwelikweli, lakini baadaye ilidhihirika waziwazi kwamba muswada huo ulikuwa na udhaifu mkubwa na kasoro nyingi za kimaudhui, kisheria, kisiasa na kikanuni kikatiba ambao kwa watunga sheria makini lazima wangelihitaji muda wa ziada wa kuufanyia kazi na sio kama wenzetu walivyoanza kuchangia wakiwa na uelewa 'finyu kiuzalendo' kwa kazi iliyokwa mbele yao.
Sio siri kwamba CCM inachokitaka pengine ni kujihakikishia uzima wa milele. Kitu ambacho hakiwezekani. Na haitawezekana kwa sababu hizi si zama za Nyerere, Mkapa na Mwinyi na chochote kinaweza kutokea kwa watu ambao hali ya uchumi inawawia ngumu kila kukichwa, mali asili zao zinatwaliwa bure, watu wanauawa na kubakwa migodini na wakubwa wanapora fedha, wanyama pori, miti, ardhi na rasilimali nyingine kwa jinsi wanavyotaka. Na wasichonacho wananyang'anywa hata kile kidogo walicho nacho, wakati wenye nacho wanazidi kuongezewa kila siku.
Watanzania hawatakaa wasahau kwamba kunako mwezi Novemba, mwaka 2011 baadhi ya wabunge wao kupitia CCM walipoteza fursa ya kipekee katika kuutanguliza Utanzania mbele ya nafsi na uchama wao. Matokeo ya ubinafsi na uchama wao yakawapotezea fursa hii adhimu ambayo ingeliwaweka pazuri sana katika historia ya nchi yao na watu wake.
Kilichotokea ni kwa wabunge hao wa CCM-CUF kuonesha dhahiri kuwa ni mbwa-mwitu (wawakilishi wa chama na serikali) waliovaa ngozi ya kondoo (wawakilishi wa wananchi). Kipaumbele siku hiyo hakikupewa wananchi na vizazi vyao vijavyo bali chama, matashi yake na ubinafsi wa wabunge hata kama Watanzania kwa ujumla wao watapoteza kikubwa zaidi siku zijazo.
UCCM na UCUF kwa kiasi fulani katika hili umewafanya wengi waamini kuwa wabunge wa vyama hivyo wanastahili kupata shahada ya udaktari katika uchama, usisi, umimi na katika mapambano ya maslahi na maendeleo ya wabunge binafsi.
Kwa maneno mengine, wabunge wa CCM na CUF walikuwa wakituambia kwamba vyama vyao na uongozi wa chama chao ni muhimu kuliko Utanzania wetu au utaifa wetu, watu wetu na vizazi vyetu vijavyo.
Kubwa zaidi ni lile la spika, muwakilishaji muswada na wabunge wa CCM waliochangia muswada huo kusingizia eti kuna urongo, uzushi, upotoshaji na tafsiri mbovu ya kile kilichotakiwa kuwakilishwa. Haraka aliyokuwa nayo spika, wabunge wa CCM kuchangia na mwasilisha muswada na wenzake kuliacha maswali mengi kuliko majibu. Mwisho wa siku kilio cha spika, muwasilisha mada na wabunge wa CCM na CUF kilifanana na kile kilio cha mchunga kondoo aliyekuwa akisumbua wanakijiji wenzake kwa kupiga mayowe ya MBWA MWITU, MBWA MWITU kumbe yote ilikuwa ni mzaha kama sio urongo.
Uzaini wa CCM wa kujionesha eti wana CCM na viongozi wao wanaipenda na wana uchungu sana na Tanzania kuliko watu wengine umewafanya jamaa hao kuangukia pua katika siku ambayo wengi wao hawataiashau na wao wenyewe wameamua kujizika kihistoria.
CCM na wakewenza Unguja
Baya zaidi ni lile la muswada huo kudiriki kuifanya Zanzibar kuwa sawasawa na Tanganyika isiyopo katika kuamua hatima ya nchi yetu na watu wake. Hiki ni kitendo cha waendesha utumwa, kikoloni, kibabe, kihuni na cha kidhalimu ambacho hakistahili kukubalika.
Kwani nia ya kuwapa ukubwa huu Wazanzibari wasiostahili kuupata ni kurahisisha siasa ndani ya CCM kati ya Wazanzibari na Wabara. Kwa maneno mengine, CCM imediriki kuwauza Watanganyika kwa Wazanzibari, kama walivyouza migodi ya dhahabu, ili mradi tu mambo yao yawe safi.
Ukewenza Zanzibar na Serikali ya JMT, unatuweka pabaya kitamathali na kiuyakinifu kwa kiasi cha eti watu asilimia 2 Tanzania kuamua hatima ya asilimia 98 iliyobakia.
Kwa maneno mengine, muswada huo unawageuza Wazanzibar wakoloni na Watanganyika watawaliwa katika nchi yao wenyewe. Sijui hata kama muswada huo utapita kama hili litakaa likubalike kesho na keshokutwa.
Hadhi ya Zanzibar kiukweli haina tofauti na ya mkoa wowote bara. Tofauti tu ni kuwa mikoa inabanwa kuwa huru kisiasa, kijamii na kiuchumi kwa mafaniko yake makubwa na haraka zaidi. Kilichokosekana ni uamsho kwa wakazi mikoani na uadilifu kwa serikali kuipa mikoa serikali huru zinazosimamiwa na waziri mkuu wa mkoa, baraza la mawaziri wa mkoa na wawakilishi wa mkoa na mikoa mingi tu ingeiacha Zanzibar nyuma kimaendeleo, bila ya visiwa hivyo kuona hata indiketa za mikoa hiyo kwenye mbio za ustawi wa jamii na maendeleo ya mkoa.
Itakuwa ni jambo la fedheha kama wabunge na serikali yetu baada ya kushindwa kuafikiana na wapinzani wa kweli ndani ya bunge itakuja kufanza hivyo kwa kupata shinikizo toka Marekani na EU. Jambo hili litaonesha kwamba viongozi wetu hawajaiva wala kukomaa na hakika hawastahili kuiongoza nchi hii kama kweli tunataka kuendelea na umoja na amani tuliyo nayo hivi leo. Kinachoonekana hapa ni kwamba kuna Watanzania wenye akili na uwezo mkubwa tu lakini kwa kukosa uongozi adilifu na mzuri wanashindwa kuwatumia.
Viongozi wa dini
Viongozi wa dini kama ilivyokuwa kwa wenzetu nchini Kenya wana mchango mkubwa katika kuhakikisha Tanzania inakuwa na katiba nzuri na safi na itakayowafaa Watanzania kwa muda mrefu kuliko hii ya kupandikizwa ilivyotsukuma sukuma.
Yapo mambo kadhaa ambayo viongozi wa dini wanaowatakia Watanzania na vizazi vyao amani na umoja wanaweza kuhoji na kutoa mwongozo yaende vipi kwa faida ya watu wote. Mathalani, hivi leo kanisa katoliki linafanya vizuri sana katika elimu na sekta ya afya, lakini siasa za uziwi na upofu zinaweza kuhujumu haya yote kama katiba isipohifadhi sheria na haki muhimu za kulinda kanisa, mali zake na viongozi wake. Misikiti na Makanisa yakikaa nyuma, viongozi wa dini wasije anza kulalama baadaye kwamba katiba imewapendelea hawa, au kuwaonea hawa.
Makampuni na taasisi na katiba
Makampuni na taasisi kisheria ni sawa na mtu au raia. Makampuni na taasisi zikikaa nyuma na kutokushiriki kwenye mchakato wa katiba mpya yapo masuala mengi yanayoweza kuja kuzuka baadaye kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiutamaduni yakaya kuwa ni kwa hasara kubwa kwa upande wao.
Katika suala hili lal katiba mpya sisi sote ni wadau na washiriki na hakuna anayestahili kubakia kuwa mtazamaji tu au juu ya wenzake kwa namna yoyote ile.
Muswada huu kama ilivyokuwa kwa miswaada mingine dhaifu, inayovuja na dhalimu kwa wananchi na vizazi vijavyo, imedhirisha mapungugu mengi mengine katika muundo, mifumo na taratibu zetu za uongozi na uendeshaji nchi. Baadhi ya kasoro hizi ni pamoja na hatari ya kuwa na wabunge wa kuteuliwa badala ya kuchaguliwa kwenye bunge la kiwakilishi; jinsi ambavyo serikali iliyoko madarakani inaweza ikapora mamlaka na madaraka ya wananchi na kufanya mapinduzi ya kikatiba bila kuwajibishwa ipasavyo; muungano unavyozidi kuonekana kukosa maana kwa Watanganyika na kuwa mzigo usiobebeka; na ule ukweli kuwa nchi bado imo kizani na haijajaliwa kuwa na kiongozi na wanasiasa wanaoweza kututoa kwenye shimo refu la giza ambalo tumejikuta tumo leo.
Pepe: sammy.makilla@columnist.com
Tuesday, November 8, 2011
Ndoa isiyo na tija
Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Hili sio la kutamba, lataka funga mkaja,
Na wengine hulichamba, wasiache kubwabwaja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Wanandoa hujisomba, wakuja na wasokuja,
Utadhani ni mtumba, hujui aliyeufuja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ndoa ni kitu cha namba, kukua si rejareja,
Yataka mengi kuumba, na sio kwishia moja,
Yataka kujenga nyumba, na pengine kwenda hija,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ndoa sio kama gamba, kuvua halina haja,
Utaonwa ni mshamba, ukabakia mseja,
Ndoa kuvuta kamba, lenu wote kuwa moja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ndoa tamu ya kulamba, ikiwa rojo vioja,
Yataka hali kuvimba, ovyo vitu kutofuja,
Yataka kuvuta kamba, mbele mkajikongoja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Akiba anayekomba, upesi kumvua koja,
Na mtaji anayefuja, ni kumshusha daraja,
Maisha yataka gomba, haikubali harija,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Huhasiri na unyumba, pasiwepo na umoja,
Japo mwafunga vilemba, nje watu hawana haja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Hili sio la kutamba, lataka funga mkaja,
Na wengine hulichamba, wasiache kubwabwaja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Wanandoa hujisomba, wakuja na wasokuja,
Utadhani ni mtumba, hujui aliyeufuja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ndoa ni kitu cha namba, kukua si rejareja,
Yataka mengi kuumba, na sio kwishia moja,
Yataka kujenga nyumba, na pengine kwenda hija,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ndoa sio kama gamba, kuvua halina haja,
Utaonwa ni mshamba, ukabakia mseja,
Ndoa kuvuta kamba, lenu wote kuwa moja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ndoa tamu ya kulamba, ikiwa rojo vioja,
Yataka hali kuvimba, ovyo vitu kutofuja,
Yataka kuvuta kamba, mbele mkajikongoja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Akiba anayekomba, upesi kumvua koja,
Na mtaji anayefuja, ni kumshusha daraja,
Maisha yataka gomba, haikubali harija,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Huhasiri na unyumba, pasiwepo na umoja,
Japo mwafunga vilemba, nje watu hawana haja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.
Sasa vuta nikuvute
Lazima nchi itwete, na kujakauka mate,
Watajatembea viwete, zikijageuka kete,
Na watu lazima mtote, kwa jasho pia matete,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Hali hii sasa tete, mambo vuta nikuvute,
Watu wataka wapate, si skuzote waote,
Ndoto wazitema mate, na hawataki mfute,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Ahadi kwao uwete, hungoja usiwakute,
Ni puya wazipepete, nafaka wasipukute,
Wengine msinifate, uoga jadi ya wote,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Nakukumbuka Mnete, Ujerumani usinate,
Njoo tuhidi viwete, hata kidogo waokote,
Na neema uilete, misada waipate,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Kila mtu ana kete, ataka naye apate,
Hatoishi kwa mkate, mtu anataka vyote,
Kwa hili msimsute, suteni nafsi zote,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Mtapoenda popote, chunguzeni na mtete,
Ili amani iote, fanaka iwe kwa wote,
Watu lisiwakerekete, la kukosa wao mkate,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Na hata vipi mnyate, gizani vyenu mng'ate,
Bado hudondoka mate, usingizini waote,
Kuteketea si lolote, na umauti ni wa wote,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Naomba yasinikute, nilapo wote niite,
Hata kidogo nipate, tutagawana na wote,
Na Rabana asisite, kichache aje avute,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Utupe leo mkate, peke yetu tusifute,
Na wenzetu waupate, slensi isiwapite,
Baadaye nisijute, kwa ubinafsi nisutwe,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Watajatembea viwete, zikijageuka kete,
Na watu lazima mtote, kwa jasho pia matete,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Hali hii sasa tete, mambo vuta nikuvute,
Watu wataka wapate, si skuzote waote,
Ndoto wazitema mate, na hawataki mfute,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Ahadi kwao uwete, hungoja usiwakute,
Ni puya wazipepete, nafaka wasipukute,
Wengine msinifate, uoga jadi ya wote,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Nakukumbuka Mnete, Ujerumani usinate,
Njoo tuhidi viwete, hata kidogo waokote,
Na neema uilete, misada waipate,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Kila mtu ana kete, ataka naye apate,
Hatoishi kwa mkate, mtu anataka vyote,
Kwa hili msimsute, suteni nafsi zote,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Mtapoenda popote, chunguzeni na mtete,
Ili amani iote, fanaka iwe kwa wote,
Watu lisiwakerekete, la kukosa wao mkate,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Na hata vipi mnyate, gizani vyenu mng'ate,
Bado hudondoka mate, usingizini waote,
Kuteketea si lolote, na umauti ni wa wote,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Naomba yasinikute, nilapo wote niite,
Hata kidogo nipate, tutagawana na wote,
Na Rabana asisite, kichache aje avute,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Utupe leo mkate, peke yetu tusifute,
Na wenzetu waupate, slensi isiwapite,
Baadaye nisijute, kwa ubinafsi nisutwe,
Sasa vuta nikuvute, mtu ataka apate!
Mwvi kamwambia....
Naishangaa dunia, kuja kuumwa mwiibiwa,
Mifuko kanipekua, na mbwa kasakazia,
Mwizi ananiibia, ataka nimalizia?
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Tukio lilipotokea, wala usingedhania,
Jizi kunishambulia, na mbwawe kunivamia,
Ah, jamani ninalia, haki inshakupotea,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Shilingi kazichukua, maumivu kunachia,
Simu nayo kaizoa, na yangu dhahabu saa,
Kila nikifikiria, nazidi kuchanganyikiwa,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Mtu hakujatokea, mie kunisadia,
Kufurukuta haikua, mbwa kuning'atua,
Amtii na kumsikia, chakula anayempatia,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Hii ndiyo yetu dunia, na hizi zake hatua,
Haki viumbe wajua, sasa waweza nunua,
Wenye haki wanagwaya, ndani huja wakatiwa,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Mwivi huru anakua, na kutamba hukutambia,
Hujui utanijua, mpini nashikilia,
Mikono yako nchani, nikivuta hatarini,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Mifuko kanipekua, na mbwa kasakazia,
Mwizi ananiibia, ataka nimalizia?
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Tukio lilipotokea, wala usingedhania,
Jizi kunishambulia, na mbwawe kunivamia,
Ah, jamani ninalia, haki inshakupotea,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Shilingi kazichukua, maumivu kunachia,
Simu nayo kaizoa, na yangu dhahabu saa,
Kila nikifikiria, nazidi kuchanganyikiwa,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Mtu hakujatokea, mie kunisadia,
Kufurukuta haikua, mbwa kuning'atua,
Amtii na kumsikia, chakula anayempatia,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Hii ndiyo yetu dunia, na hizi zake hatua,
Haki viumbe wajua, sasa waweza nunua,
Wenye haki wanagwaya, ndani huja wakatiwa,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Mwivi huru anakua, na kutamba hukutambia,
Hujui utanijua, mpini nashikilia,
Mikono yako nchani, nikivuta hatarini,
Mwivi kamwambia mbwawe, ankamate, antafune!
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
NYIE hawatawafunga, mkifunga wapinzani,
Mbona mnayabananga,hamjui mwajizaini,
Dunia geuzi anga,wajinga hawabaini,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Kutesa kwa zamu ringa, ila ujue yakini,
Wafunge watakufunga, kama haki hukuauni,
Usiombee kimbunga,kikukute mtaani,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Hujatengwa na mtenga, wajua Raskazoni,
Mpingwa huja kupinga, ikawa abautani,
Mgongwa huja kugonga, ujikute hatarini,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Sheria ukizipanga, jua na wewe undani,
Na kanuni ukitunga, jione nawe mpinzani,
Ujapoivaa khanga, usilisahau gauni,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Ukiuchonga mzinga, na nyuki wabaini,
Asali ukenda kinga, kubali na yake faini,
Porini ukenda chunga, simba usiwaamini,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Hukungwa naye mkunga, uzazi hauna dini,
Na mfungwa huja kufunga, Mandela hili aamini,
Ila sidhani kwa mwanga, iweje kuwangiwani?
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Hutwanga mtwanga unga, na hili asibaini,
Nchi yataka waganga, haitaki majinuni,
Nchi yataka kuunga, nyie vipi mwabanduani?
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Mbona mnayabananga,hamjui mwajizaini,
Dunia geuzi anga,wajinga hawabaini,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Kutesa kwa zamu ringa, ila ujue yakini,
Wafunge watakufunga, kama haki hukuauni,
Usiombee kimbunga,kikukute mtaani,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Hujatengwa na mtenga, wajua Raskazoni,
Mpingwa huja kupinga, ikawa abautani,
Mgongwa huja kugonga, ujikute hatarini,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Sheria ukizipanga, jua na wewe undani,
Na kanuni ukitunga, jione nawe mpinzani,
Ujapoivaa khanga, usilisahau gauni,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Ukiuchonga mzinga, na nyuki wabaini,
Asali ukenda kinga, kubali na yake faini,
Porini ukenda chunga, simba usiwaamini,
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Hukungwa naye mkunga, uzazi hauna dini,
Na mfungwa huja kufunga, Mandela hili aamini,
Ila sidhani kwa mwanga, iweje kuwangiwani?
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Hutwanga mtwanga unga, na hili asibaini,
Nchi yataka waganga, haitaki majinuni,
Nchi yataka kuunga, nyie vipi mwabanduani?
Mkiwafunga wapinzani, nao hawatawafunga?
Waziri mkuu wa mkoa....
Nchi haitoendelea, bila mkoa huru kuwa,
Maamuzi kujifanyia, bila ya mtu kungojea,
Na awe nayo raia, sauti ya kusikiwa,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Arusha yasingetokea, leo yanayotokea,
Mkoa unatawaliwa, na chama chenye izaya,
Wajanja walipokwapua, kile wasichojivunia,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Mbeya ukiangalia, chama fulani chafaa,
Kuutawala mkoa, zingeliisha ghasia,
Uchumi wadidimia, king'ang'anizi kung'ang'ania,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Na Mwanzo nako pia, kama haya yatokea,
Uhuru wanalilia, wakazi wake mkoa,
Mambo yao kimkoa, wao wenyewe kuamua,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Wamechoka kuwekewa, viongozi wasofaa,
Na tena sio wazawa, uchungu nao hawajawa,
Angelikuwa mwana kaya, uchumi angelipaua,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Ardhi wanachukua, wa mkoa wasokuwa,
Juu walikokalia, wawekezaji wauzia,
Sasa wanagombania, ardhi kujilindia,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Mali asili tambua, ni ya wakazi wa mkoa,
Haijawa, haitakuwa, ya hao wanaopewa,
Tutaambiana ubaya, haya yakija tokea,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Tuacheni kusinzia, haja za watu kujua,
Muda usijepotea, mabaya kujatokea,
Ama chelewa chelewa, mwana hutomkumbatia!
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Maamuzi kujifanyia, bila ya mtu kungojea,
Na awe nayo raia, sauti ya kusikiwa,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Arusha yasingetokea, leo yanayotokea,
Mkoa unatawaliwa, na chama chenye izaya,
Wajanja walipokwapua, kile wasichojivunia,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Mbeya ukiangalia, chama fulani chafaa,
Kuutawala mkoa, zingeliisha ghasia,
Uchumi wadidimia, king'ang'anizi kung'ang'ania,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Na Mwanzo nako pia, kama haya yatokea,
Uhuru wanalilia, wakazi wake mkoa,
Mambo yao kimkoa, wao wenyewe kuamua,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Wamechoka kuwekewa, viongozi wasofaa,
Na tena sio wazawa, uchungu nao hawajawa,
Angelikuwa mwana kaya, uchumi angelipaua,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Ardhi wanachukua, wa mkoa wasokuwa,
Juu walikokalia, wawekezaji wauzia,
Sasa wanagombania, ardhi kujilindia,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Mali asili tambua, ni ya wakazi wa mkoa,
Haijawa, haitakuwa, ya hao wanaopewa,
Tutaambiana ubaya, haya yakija tokea,
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Tuacheni kusinzia, haja za watu kujua,
Muda usijepotea, mabaya kujatokea,
Ama chelewa chelewa, mwana hutomkumbatia!
Mkoa lazima uwe, na waziri mkuu wake.
Subscribe to:
Posts (Atom)
