SISHANGAI kwanini baadhi ya wabunge hawajagutukia mtego uliopo katika kashikashi ya posho iwepo au isiwepo. Kwa tunaojaribu kuangali mbali na kuona mbele tunatambua kwamba tatizo hapa sio POSHO bali ni ile hali ya umaskini wa kutisha aliyonayo Mtanzania wa kawaida.
Kwa bahati mbaya waheshimiwa wabunge wetu wanachokiona ni kutaka kuporwa na pengine na wale 'walioneemeka kwa njia nyingine' hata kile ambacho bado wao wanakiona ni kidogo.
Wale waliokwishazunguka mijini na vijijini baada ya kubaini kwamba wanaweza kutumia matatizo na dhiki mbalimbali za wananchi kama mtaji wa kisiasa hawajachelewa kufanya hivyo.
Na wale wanaokurupuka na majibu ya haraka haraka bila shaka watajikuta wanajiumbua wenyewe na kubaki wameshangaa ni kitu gani kinachoendelea.
Wenzetu wasingelikuwa wanasumbuliwa na ule ugonjwa niliowahi kuusilimisha kwa jina la 'ndivyotunavyofikir' wangekuwa wajanja kidogo tu, wangelitambua wanaowawakilisha wanauliza na wanataka majibu ya ni nini taifa hili linalovuna na kinachovunwa kinagawanywa vipi ?
Ni vigumu kuandika makala kama hii bila kuegemea upande wa walalahoi na wasiofaidika na mfumo uliopo lakini nitajaribu kutokupendelea upande wowote kwa mara ya kwanza.
Mlipuko wa mawasiliano rahisi kati ya mtu na mtu kupitia simu za mkononi, redio, televisheni, tovuti, blogi, twitter na facebook mijini na vijijini vinawaarifu wananchi mambo mengi kupita hata uwezo wao wa kuyatafakari na kuyachambua. Lakini, kila mmoja akihabarika kiasi cha kuanza kuuuliza je hicho kinachovunwa na taifa ni
nani anayekipata, yuko wapi hapa nchini, anakipata wakati gani, na kwanini anapata yeye na sio wengine ?
Dakika moja tu inatosha kwa mtoto wa mkulima kule kijijini kufahamu kutoka kwa mwanawe kwamba senti anazomtumia inabidi zipungue kwa sababu uwezo wake wa kifedha sasa umeterereka. Gharama mbalimbali zimepanda na wa kulaumiwa ni serikali na chama tawala. Kwa maneno mengine, kazi ya kuwaumbua, kuwasingizia, kuwapakazia na kulaumu viongozi na serikali imekuwa rahisi kufikishwa hadi kijijini -ambako watu kwa kawaida walikuwa wamelala na wasioamin kwamba serikali inaweza kuwa na nia mbaya na wanachi wake achilia mbali kuwafanyia ubaya huku ikijua inawafanyia ubaya.
Je, kuna usawa na haki katika kile kinachopatikana kwa maana wananchi wote wana fursa sawa, wako huru kukifanya au kuna wanaojichagua na kufaidi wao tu. Na kama kuna matatizo, je, kuna wanaoyashughulikia matatizo hayo kwa wakati na kwa manufaa ya jamii husika.
Au kila kiongozi toka ngazi ya chini hadi juu yuko 'bize' na mambo mengine lakini sio matatizo ya wananchi. Na je, wale wanaotumwa kwenda kuwawakilisha wananchi je wanafanya hivyo au wanawakilisha watu au taasisi nyingine ?
Je, mfumo na miundo ya kiuchumi na kijamii iliyopo inaonesha kuwa na uwezekano wa kuwapa wananchi fursa ya kutatua matatizo yao na kujiendeleza wao wenyewe bila kuhadaiwa na siasa au wanasiasa au watu wengine ?
Hii ni miaka ambayo wananchi watakuwa wanauliza maswali yaliyokuwa hayaulizwi sana huko nyuma. Mathalani, wanaweza kuuliza je, hao wanaopata kilicho kikubwa na zaidi ya wengine kutoka kwenye keki ya taifa wanastahili kupata wanachokipata. Au wanakipata kitu wasichokitolea jasho, yaani, wasichokistahili kwa uhalali kabisa, kwa maana kuwepo kwao ni mzigo tu kwa wananchi na watu hao hawasaidii wananchi kuapta unafuu wowote katika maisha yao ?
Yaani, wanaopata zaidi wanakula haramu na jasho la wananchi bue kwa kupata zaidi au wanapendelewa au wanajipendelea bila kuwa na sababu yoyote ya kuridhisha? Utakumbuka wale tulioikuwa tunasoma sekondari za kulala au hata za siku ambazo kuna chakaula cha mchana au jioni. Katika dhambi kubwa niliyowahi kujisikia ni ile ya kujimegea mimi binafsi wali mwingi na mboga nyingi kuliko wanafunzi wenzangu tuliokuwa tunakula kwenye meza moja. Nilifanya hivyo baada ya kuguswa na kosa nililolifanya. Nikaugawa tena wali wangu kwa kuwapunguzia wenzangu na mimi kubakiwa na kiasi kidogo kuliko wao. Kuanzia hapo, palikuwa hapana swali ni nani anastahili kugawa chakula katika meza yetu.
Swali dada na hili ni lile la nani wanaopata kidogo au wanaokosa kabisa ? Na kama kukosa kwao kunatokana na wao kuwa duni, wajinga, wavivu na wasiojituma kwa kiasi hicho au kwa kuwa wamezidiwa tu ujanja na uelewa na wale waliotangulia kupata mitaji na wanaowaongoza?
Kwanini wanakosa ? Kwanini hawatosheki, hawaridhiki na hawashibi kwa yale mazuri viongozi na wanasiasa wanayoamini tayari wamekwishawafanyia toka kuwepo kwao madarkaani?
Na je, mfumo mapokeo tuliourithi na tulio nao hadi leona uloanzia toka tukiwa na watu milioni 9 (1960) unafaa baada ya miaka 50 ambako tunakadiriwa kuwa watu milioni 50 ? Au kwa maneno mengine, kama Karl Marx alivyohoji, je, mahesabu yetu ya 'production' na 'reproduction' na 'redistribution' ya mapato ya taifa yapo sawa na sio yameachiwa huru mno kiasi ambacho tunachezea bomu la tofauti kubwa ya kipato kati ya walionacho na wasionacho?
Tanzania inafikisha miaka 50 ya Uhuru wa benderea ikiwa na tofauti kubwa kati ya mtu wa kipato cha chini na yule wa kipato cha juu pengine kwa uwiano wa 1: 10,000. Hii sio tu ni hatari bali ni aibu na fedheha kwa nchi ambayo Mungu na kiongozi wake wa mwanzo alishawaonyesha ubaya wa tofauti kubwa namna hii kati ya walionacho na wasio nacho.
Na kama Wahenga walivyosema,' Mwenye shibe, hamjui mwenye njaa', jambo hilo sasa, yaani walionacho kushindwa kujua kwanini kuna umasikini na kwanini watu hawana fedha mifukoni mwao na majumbani mwao, limefikia hadi kwenye ngazi za juu za uongozi wetu? Majemadari wanaotakiwa kuwatoa Watanzania toka kwenye umasikini hawajui upana, urefu na kina cha umasikini nchini mwao na miongoni mwa watu wao!!
Upo uwezekano mkubwa kwa nchi hii na viongozi kujiabisha kuhusu hali ya maisha ya Mtanzania kutokana na kulewa na sifa za viongozi wa nje na wale wanaowatumia kisiasa kwa faida zao wanazozijua wao wenyewe.
Katika kupanga tufanye nini wakati wa kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru tuwe waangalifu sana ili sherehe hizo zisiwe chanzo cha kujiaibisha na kujifedhehesha badala ya nafasi nzuri ya kurekebisha makosa yaliyopo na kuifanya siku hiyo siku ya kuzindua yale yatakayowapa wananchi matumaini na faraja.
Ni wakati muafaka kwa hiyo kuoanisha suala la 'posho ya wabunge' na lile la 'riziki ya kila siku ya mwananchi wa kawaida' na wawakilishi wetu kujiuliza kama hakuna uhusiano kati yake na hali halisi ya yule wanayemwakilisha bila kuzingatia dhiki na umaskini wake huko bungeni na kulipa hilo uzito unaostahili bila kuburuzwa na mtu au taasisi yoyote ambayo imeamua kufumbia macho jambo hili ?
Au kuna wanaowafunga macho kwa kitambaa cha khaki tena khaki nyeusi katika usiku mweusi wa hali halisi ya kiuchumi ya Mtanzania?
Je tunaweza kuongeza kinachovunwa? Kwa njia gani na mbinu zipi na mikakati ipi ya chapchapu ? Na hivi ukiwauliza Watanzania kwanini wao ni masikini na wewe una wajibu wa kuwatoa toka kwenye umaskini je, unawajibika kweli na je, unawatendea haki Watanzania masikini? Je, Taasisi ya Utafiti kuhusu umaskini hapa nchini imefikia wapi na yale ambayo imekwishayatafiti hadi wa leo yamefanyiwa kazi kiasi gani? Kwa maneno mengine, je, taasisi hiyo imekuwa na manufaa yaliyokusudiwa kwa Watanzania masikini au imewashibisha tu waliomo katika taasisi hiyo na nyingine kama hizo?
Na, je, ukiritimba katika masuala ya uongozi wa kijamii na uchumi ndio utakaotusaidia kutoka kwenye umasikini na matatizo yetu au tunaung'ang'ania tu kwa sababu ya mazoea na uoga wa kujaribu kilicho kipya?
Maana kuna wanaoamini kwamba serikali kuu inapswa kugawa madaraka ya maamuzi na utekelezaji sio tu kwa mikoa, wilaya, vyama vya kisiasa, mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali, makundi mbalimbali ya kijamii na watu mmoja mmoja kushiriki na kuchangia kikamilifu katika kuziona na kuzitumia fursa za kiuchumi na kijamii zilizopo nchini kuliko tulivyowahi kufanza huko siku za nyuma na vilevile kuyatafakari matatizo mbalimbali yanayowakabili Watanzania na kisha kuweka mkakati unaosadikisha kwamba 'utatuaji matatizo kila sekta, katika kila jamii' kila kona nchini ndiyo ajenda yetu ya kwanza kwa kila mpango tulionao na tutakaokuwa nao.
Tuiaminishe pia jamii yetu kwamba tukijipanga upya, kimkakati, kiakili na kwa hekina na busara zaidi tunaweza kupatia ufumbuzi sisi wenyewe matatizo na changamoto nyingi zinazotukabili.
Na pale msaada wa serikali, sekta binafsi na wasamaria wema inapohitajika inakuwa ni pale ambapo hatuna ujanja kwani kiakili, kiteknolojia na kirasilimali nyinginezo tumekwama na hatuna ujanja.
Nguvu na akili-jamii na ujasiriamali-kijamii ndio njia pekee ya kuinua ubora wa maisha ya Mtanzania.
Serikali yetu lazima ifike siku irudie maneno ya Mwalimu Nyerere kwamba, 'Serikali na Watanzania hatuna fedha. Na fedha na mtaji wetu ni akili, nguvu, maarifa, juhudi na bidii zetu wenyewe katika kutatua matatizo na changamoto mbalimbali zinazotukabili.'
Serikali ikiendelea kujifanya ndio bwana mkubwa, tajiri, ina mali, ina uwezo, ina nguvu na inaweza kila kitu na haishindwi na chochote lazima kuna siku tataibika na tutakwama.
Ninaamini ni Watanzania ndio wanaostahili kuwa BWANA MKUBWA, MATAJIRI, MFANO WA MUKTADIRI, KWA MAPENZI NA BARAKA ZA MWENYEZI MUNGU WANAWEZA KILA JAMBO, HAWASHINDWI NA LOLOTE na wingi, nguvu, matakwa na maslahi yao ndiyo yanayopasa kutawala na kuendesha nchi hii na sio vinginevyo. Demokrasia kwanza, mengine ni mazungumzo baada ya habari.
Tunaweza kumlaumu Mtanzania kuwa chanzo cha kukosa mahitaji yake ya msingi, maradhi, ujinga na umaskini wake lakini tusisahau kwamba upo uwezekano pia ikawa ni mundo na mifumo tuliyo nayo na ukiritimba wa serikali katika mipango, maamuzi na utekelezaji wake vikawa ndio sababu ya umasikini wa Mtanzania.
Katiba, wabunge na posho...
LABDA wabunge wanaotaka wasilipwe posho wameaona kile wanachokula hakilingani na kazi wanayowafanyia masikini wa Kitanzania katika jitihada zao za kutuondoa na umaskini, ujinga na maradhi.
Wametangulia Katiba katika kuleta mabadiliko ya kimsingi yanayohitajika, kwa maana ya kwamba, kipato cha kila kiongozi wa Kitanzania kwanza, kinatakiwa kinaoanishwa na mchango wake katika kupiga vita umaskini, ujinga na maradhi awali ya yote. Na kwa upande mwingine ipo haja kujenga miundo na mifumo inayomsaidia mwananchi kuondakana na umaskini badala ya miundo inayomwingiza mwananchi kwenye umaskini zaidi.
Wakati tunasubiri ujio wa Katiba mpya na namna itakayolishughulikia suala la keki ya taifa na inavyostahili kugawanywa kwa namna ambayo kila Mtanzania anakuwa na arri na motisha ya juu kuiondoa nchi hii kwenye daraja la tatu na umaskini mkubwa kwenda kwenye daraja la pili la kiuchumi kidunia lenye nafuu, utu na ubinadamu zaidi.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment