UDIKTETA au ukiritimba kwa mtu mmoja kuhodhi mamlaka yote peke yake, iwe kisiasa au kiuchumi au kijamii huashiria kuwpo mtu au kikundi cha watu wasiojiamini na wasiokuwa na uhakika wa kile wanaschostahili wanachokifanya. Aghalabu watu wa namna hii huwa hawajui wanakotoka wala wanakokwenda. Kihistoria na kimustakabali ni muflisi. Ni mwanzo wa ufichaji maovu mengi kwa kuonesha mazuri machache ambayo pengine hayana manufaa kwa binadamu. Udikteta una tabia ya kuwageuza watu wote wajinga, mazezeta na wakorofi na wachache walioko madarakani kuwa ndio watu bora, wanaojua kila kitu wastaarabu na wazalendo wa kweli. Hata hivyo, jambo hili pia huwa na tabia ya kujichimbia kaburi lake yenyewe. Huanza kwa kutoamini wengine lakini huishia kwa kutojiamini wenyewe na kutoaminiana wenyewe kwa wenyewe na kuishia kwa wao wenyewe kujichanganya na kujimaliza.
Udikteta huweza kuundwa na mtu mmoja au kikundi cha watu. Udikteta uliopo Tanzania hivi leo ni ule wa kichama. Udikteta unaokifanya chama kimoja kujiona kimeokoka na kitakatifu zaidi kuliko vyama vingine. Eti peke yake na wanasiasa wake tu ndio wanaoweza kufanya mema na mazuri kwa nchi. Udikteta unaotaka kuwaaminisha watu eti kwamba chama kinachotawala peke yake ndicho kinachotaka kudumisha amani, umoja na mshikamano nchini na vyama vingine ni hatari na tishio kwa umoja na amani yetu. Jambo ambalo si kweli bali unafiki na danganya toto ya wale wanaotaka kula nchi bila kubughudhiwa. Na haya tumeyaona huko Tunisia, Misri na yakingali yanaendelea Libya, Bahrain, Oman, Yemen na kadhalika.
Udikteta huu unajidhirisha kwa chama hicho kutaka kuwa na watu na sauti katika kila jambo hata yale yasiyokihusu- kwa mfano, dini, utamaduni, mila na desturi, mawasiliano, maendeleo ya watu na jamii zao, ushirika, uzalishaji mali na majumuiko mengine ya kijamii kwa hofu hii au ile.
Katika miaka hii kila mkoa utakuwa ukijiuliza sisi kama mkoa tunapata NINI, tunapata toka kwa NANI, tunakipata LINI, tunapata kwa ajili ya NANI na KWANINI tunapata kitu tunachopata HIVI SASA, ni NANI anayetupa, yuko WAPI, NA ANATUPA KWA SABABU gani na kwa NAMNA GANI ILI YEYE NA SISI TUPATE nini kwa ajili ya nini NA KINA NANI ? Na tunachopewa ni SAMAKI au ni NDOANA au nyavu za sisi wenyewe KUVUA?
Na je kwa mpango huu tutapata maendeleo baada ya miaka michache au baada ya miongo kama sio karne? Maana wakishaingia madarakani viongozi wa Kiafrika hudhani wananchi wameuimbwa kuwa wavumilivu hata katika yale mambo yanayopaswa kutekelezwa ndani ya juma au mwezi tu! Ili mradi wao wanaishi na kula vizuri, wanapanda helikopta na ndege na hakuna wanachokosa msamiati wenye maneno kama haraka na dharura kwao hamna. Uvumilivu kama huo utakuwa ni vigumu kupatikana huko tunakokwenda.
Kwa kuwa wanasiasa waliopo wanaamini hawawezi kuitawala nchi bila ya kulazimisha mikoa, wilaya, vijiji na mitaa kuwa chini ya chama tawala basi miundo, kanuni na mifumo ya kisiasa inayoundwa sio ile ya kufanya maeneo hayo kuwa huru bali maeneo hayo kutawaliwa moja kwa moja au kimzunguko na chama tawala na viongozi wake.
Ni dhahiri basi madaraka mikoani au kuwa na mikoa huru kiuchumi na kijamii sio jambo linaloweza kufanywa na wanasiasa wa chama tawala. Hili ni jambo linalostahili kuwemo kwenye katiba na sheria za nchi kama sehemu moja ya kupanua na kuongeza kina cha watu kujitawala, kujiamulia mambo yao wenyewe na demokrasia kiujumla.
Chama tawala kina unafiki mkubwa ambao ni muhimu kuutambua na kuubainisha kwa wadau wa katiba. Kwa kuwa kinatambua nguvu yake inatokana na ujinga, umaskini na magonjwa mbalimbali ya watawaliwa basi kinaelewa fika kuwa kupiga vita mambo hayo ni lazima wanajamii washirikiane ili kufanikiwa. Lakini, ushirikiano wa wananchi kijamii na kiuchumi kutawapa pia wanajamii nguvu na sauti sawa au zaidi ya wanasiasa. Kwa mantiki hii chama cha siasa kinachokubali makundi ya jamii au watu kuwa huru zaidi kiuchumi na kisisasa katika ngazi ya mtaa, kata, wilaya na mkoa huhofia pia kujimaliza kisiasa. Kwa sababu hii, maamuzi yote yanayohusiana na kuyapa makundi ya kijamii nguvu na uwezo zaidi hufanywa polepole mno. Jambo la siku moja huchukua mwezi; la mwezi, mwaka; la mwaka muongo; la muongo karne kama sio zaidi!
Hata hivyo, ili nchi na watu wake wapate maendeleo hakuna njia ya mkato. Njia ni moja tu. Nayo ni ushirikishwaji wananchi na umilikaji wananchi uchumi wa nchi katika uundwaji wa katiba na sheria za nchi zinazoendana na wakati tuliomo; ushirikishwaji watu katika maamuzi, mipango, uongozi, utekelezwaji na udhibiti wa masuala yote ya maendeleo na ustawi wa jamii husika ikiwemo kuwa na mikoa huru kiuchumi inayokuwa chini ya viongozi waliochaguliwa na wananchi au wakazi wa mkoa husika.
Kwa kifupi kuna mambo kadhaa yanayoonesha wazi kwamba ili serikali yoyote ifanikiwe ni lazima wananchi wake washiriki na wawe na sauti katika uongozi wa nchi:
. Kukubalika, heshima na uwezo wa serikali kuu huanza kwenye mitaa na jamii mikoani;
. Maendeleo ya kweli ya mkoa yanatokana na kile wananchi wake wanachozalisha na kumiliki na sio vitu vya wageni;
. Serikali zenye nguvu na uwezo za mikoa na mitaa hufanya kazi ya kulinda hazina ya mkoa na mali asili za eneo husika kwa faida ya wakazi wake na nchi nzima;
. Uongozi wa kitaifa hutekeleza miradi ya mikoa aghalabu nusu nusu na bila udhibiti wa kutosha kutokana na kukurupuka na kwenda kuzima moto unaowaka mkoa mwingine, hivyo kuhamisha fedha kwa ajili ya mkoa mmoja kwenda kuufaa mkoa mwingine isivyo haki;
. Serikali huru za mikoa ni shule au chuo pekee kitakachowafundisha viongozi wa baadaye wa kitaifa kwa vitendo huko huko waliko mikoani.
Migogoro ya kisiasa inayotokea Afrika na hususan Tanzania kwa kiasi kikubwa ni kati ya wale wamanaoamini:
* Wanasiasa wanaoamini kwamba Watanzania ni waoga na wasiokubali tofauti kati yao na migogoro na wale wanaoamini Watanzana ni mashujaa na kuwa tofatui na migogoro ya kisiasa, kijamii, kiuchumi, kiteknolojia na kiutamaduni ni sehemu ya maisha ya kawaida ya nchi na wananchi na lazima ikubalike na itumiwe kwa faida ya kunusuru nchi na watu wake;
* wanasiasa kazi yao ni kutawala na wananchi ni kutawaliwa tu dhidi ya wale wanaoamini wananchi wanastahili kujitawala wenyewe;
* Wanasiasa wanaoamini viongozi wetu wanastahili kuishi kifahari na wale wanaoamini ni lazima wanasiasa wajishushe kwanza na kuwanyanyua watu wao kabla ya wao wenyewe kuwa na maisha mazuri na bora;
* Wanasiasa wanaodhani kuwa kazi ya vyombo vya habari vya umma na vile vya chama tawala ni kufumua na kuharibu ukweli na kisha kufuma na kusambaza urongo na wale wanaoamini hakuna mwenye haki ya kutengeneza na kuuzia wananchi uongo Afrika;
* wanasiasa wanastahili maisha mazuri na bora kuliko raia wengine na wale wanaoamini wananchi wanastahili maisha bora na mazuri kuliko ya wanasiasa;
* wanasiasa wetu wanastahili kuwanyenyekea na kuwafuata wale wanasiasa matajiri kwa kila jambo wanalolisema au kutushauri hata likiwa halina maslahi kwa watu wetu na wale wanaoamini wakati umefika kwa wanasiasa wetu kusimama kwa miguu yao wenyewe;
* wanasiasa wanastahili kuwatumia polisi na pengine jeshi ili kuwasaga wananchi waende kule wao wanakotaka waende dhidi ya wale wanaoamini polisi na jeshi wanastahili kudhibiti wanasiasa kwenda kule katiba na wananchi wanakotaka nchi iende;
* wanasiasa wanahitaji kubaki madarakani milele ili walete maendeleo na wale wanaoshani wanastahili kubaki tu madarakani kama wanaweza kuongeza thamani na ubora wa miasha ya mwananchi;
* wanasiasa wanaoamini wananchi wakielimishwa na wakiondokana na ujinga na umasikini itakuwa vigumu wao kutawala dhidi ya wale wanaoamini itakuwa rahisi zaidi kwao kutawala;
* Wanasiasa wanaoamini wananchi ni wajinga na wao wanasiasa ni wajanja na wale wanaodhani hakuna kitu kama hicho na jambo hilo linategemea watu binafsi na mitazamo na makusudio yao;
* wanasiasa wanaoamini ni wanachama wa chama fulani tu wanaostahili kuwa na sauti na kuwa makundi mengine katika jamii hayastahili kuwezeshwa wala kuwa na nguvu iwe ya kisiasa, kijamii au kiuchumi na kadhalika;
* wanasiasa wa chama tawala ndio tu wapewe uongozi hata kama hawawezi kazi na wale wanaodhani wanaostahili kuongoza wananchi lazima wachaguliwe na wananchi wa eneo husika.
Afrika imebadilika, na Afrika ya leo si ya jana. Wale wote wenye fikra hasi pacha za kwanza hawana tena nafasi katika Afrika mpya. Kizungumkuti kinachokuja kitawafagia pembeni hadi kwenye majaa kama ilivyofanyika huko Maghreb na kuwajaribu wala wenye fikra mbadala chanya pacha hapo juu.
Na njia sahihi ya kuifuata ni kuhakikisha kuwa kuanzia sasa tunakubali na tunahamasisha kupeleka madaraka kwa wananchi sio tu mikoani bali mpaka vijijini na kwenye kila kata na mtaa.
Mikoa Huru ya Ujerumani:
Kwa mfano mikoa ya Ujerumani ni pamoja na Baden-Württemberg, Bavaria (Bayern), Berlin,Brandenburg na Bremen. Kahalika kuna Hamburg, Hesse
(Hessen), Mecklenburg-Vorpommern, Lower Saxony (Niedersachsen), North Rhine-Westphalia (Nordrhein-Westfalen), Rhineland-Palatinate (Rheinland-Pfalz), Saarland, Saxony (Sachsen), Saxony-Anhalt (Sachsen-Anhalt), Schleswig-Holstein na Thuringia (Thüringen).
Mikoa yote hii isipokuwa kwa mkoa mmoja tu ina serikali za pamoja/mseto kati ya vyama viwili au zaidi. KIla mkoa una waziri wake mkuu, baraza lake la mawaziri, wawakilishi wake na taasisi zake na inakuwa huru kwa kiasi kikubwa kwenye masuala yote ya kiuchumi na kijamii. Yale ya ulinzi, usalama, fedha na siasa za nje hushughulikiwa zaidi na serikali ya kitaifa yenye makao yake makuu hivi leo Berlin. Mikoa hii imewezesha kuwa na ushindani wa ndani kwa ndani na hivyo kuipa nguvu Ujerumani katika utandawazi na ushindani wa nje kwa kujikita tu kwenye maeneo inayoamini hakuna anayeweza kuwapita. Wao si watu wa kufanya na kujaribu kila kitu kwa kubahatisha. Hutafuta uhakika kwanza kabla hawajawekeza kwenye jambo fulani.
Jiografia ya nchi na rasilimali
Baadhi ya mambo yanayofanyika nchini hivi leo hayaashirii mshikamano na umoja wa nchi.
Kwa mfano, badala ya kujenga vyuo vikuu vidogo kila mkoa serikali iliyopo madarakani ina mkakati wa kujenga vyuo vikuu vikubwa katika mikoa michache iliyochaguliwa kwa sababu zisizofahamika. Hili linafanyika ikidhihirika kuwa bado hatujawa na rasilimali watu timilifu kusimamia vyuo vikubwa vyenye wanafunzi zaidi ya elfu tano tu. Hali kadhalika, hili linatokea wakati kila mkoa unajenga hisia ya kupendelewa au kutopendelewa katika kupata taasisi kama hizi. Je, huko mbele tunakokwenda hakuna mikoa itakayokuja kugeuka na kudai vyuo vikuu vilivyopo mkoani vyake ni vyake na sio vya kitaifa. HIvi tumejifunza nini toka Yugoslavia na Urussi ya zamani na yaliyotokea huko? Aidha, mkoa kukosa kabisa angalau chuo kikuu kimoja ni dhuluma ya hali ya juu ya kielimu kwa wakazi wa mkoa husika. Kwa maneno mengine kama Tanganyika ilivyoanza na Chuo KIkuu chenye chini ya wanafunzi mia moja basi ni haki ya kila mkoa kuanzisha chuo kikuu chake hata ikiwa ni kuanza na wanafunzi ishirini tu. Kitaongozwa vyema. Kitakuwa. Kitaendelea na mkoa utajivuna pia kuwa na chuo kikuu chao.
Hili limerahisishwa tayari na Chuo Kikuu huria cha Tanzania (CKT) kinachotakiwa ni kukisaidia chuo hicho sasa kugeuza matawi yake mikoani kuwa k.m. Chuo KIkuu Huria cha Arusha au Manyara au Mbeya au Ruvuma au Pwani na kadhalika.
Sunday, March 6, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment