Thursday, December 22, 2011

Dar kimaafa ni bomu litakalolipuka wakati wowote

NI DHAHIRI suala la kuishi au kuhama mabondeni, hususan Jangwani, ni
suala 'lililosiasaishwa' na haiwezekani chama kilichoko madarakani na
serikali kuwahamisha wakazi wa maeneo haya kwa nguvu kama nguvu
inavyotumika sehemu zingine kutokana na kuhitajika kwa mtaji wa kisiasa.

Haiwezekani pia kidira, kisera, kifedha, kiteknolojia na kiuwezo kwa Dar es
salaam ambayo ni pua na mdomo na bahari kuwa na miundo mbinu
itakaloliwezesha jiji litapike maji yote ya mvua yaende baharini kama tu
imeshidwa kutapisha maji taka na ya matumizi ya kawaida kwenda baharini.
Ugumu wa hili umedhirishwa na kauli zinazopingana juu ya kuhama au
kutokuhama mabondeni zinazotolewa na viongozi wa serikali na chama
tawala. Haiwezekani katika muda mfupi na siamini kama suala hilo limo
katika kipaumbele cha serikali. Je, kiuhalisia kinachobakia kushauri ni kitu
gani ? Nitajaribu ingawa ninajua ni mtihani mkubwa kufanya hivyo katika
makala yangu leo. Ila kama kawaida tutarajie amri zisizotekelezeka na ahadi zisizotimizwa.

Kipindi cha pili cha awamu ya nne kilianza kwa bishara njemba katika
angalau za masula ya nyumba na makazi, lakini kadri muda unavyokwenda
imedhihirika kuwa hizo zilikuwa ni nguvu za soda tu.

Biashara hizo zilitokana kwanza na kuteuliwa kwa mwanamke aliyeswahi
kushika wadhifa wa juu katika shilrika la masula ya nyumba na makazi na
kauli zake za mwanzo ambazo zilionekana kama angelikuwa na uhuru wa
kufanya yale anayofikiria kichwani kwake leo angalau tungelianza angalau
kuona ishara za kuwa na mipngo miji katika nchi ambayo kwa mapana na
marefu na kwa ujumla yake ilikwishazika kabisa suala la mipango miji na
ujenzi uaoangalia na kutahadhari na yanayoweza kutokea kesho na kesho
kutwa.

Jambo moja linalochangia udhaifu katika utawala na menejimenti yetu ya
nyumba na makazi ni sheria za kubembelezana na kuvumiliana. Na siku hizi
umezuka mtindo kuwa pakijengwa kijiwe cha chama tawala mahala fulani,
basi mahala hapo panahesabika kuwa sehemu ambayo hata kama sheria
zimevunjwa, hazikuvunjwa!

Hizi ni siasa za kutafuta kupendwa na umaarufu, huku mtu akijua fika kwa
kuruhusu kinachofanyika kiendelee kufanyika basi mwisho wake ni zahama,
dhiki na vifo kwa wale wanouhurumiwa na kvumililiwa. Ninaamini wakati
umefika kwa nchi yetu kujenga heshima ya kuwa na utawala wa kisheria
ambao haushawishiwi vinginevyo na wanasiasa kwa malengo yao binafsi.

Pamoja na ujenzi wa nyumba mabondeni ipo mifano mingi ya kimaafa
maafa tu inayosubiri cheche moja tu, moto au bomu kulipuka.

Mifano hiyo ni pamoja na vituo vya zima moto na upatikanaji maji kuwa mbali
na maeneo ambayo janga la moto linaweza likazuka.

Manispaa mbalimbali za maji zimeruhusu au kuachia watu kujenga kuta au
vizuizi vya aina mbalimbali ambavyo vinaweza vikachangia si haba ukubwa
wa maafa na hasa yale ya maji na mafuriko.

Tembelea sehemu mbalimbali za jiji la Dar es salaam na utakuta makumi
kama sio mamia ya vituo vya petroli ambavyo vimejenga kando ya masoko
au ndani ya makazi ya watu.

Watalii mbalimbali hivi sasa wanahofia kuja Tanzania kutokana na
kukosekana usalama wa kutosha mabarabarani . Jambo linalosababishwa
na malori, daladala, bajaji, pikipiki, mikokoteni na vyombo vingine vya
uchukuzi kutofuata sheria zilizopo na kukosa uungwana na ustaarabu katika
maingiliano ya watu njiani.

Aidha, kumekuwa na kauli kadhaa za kisheria zisizotekelezwa juu ya hili au
lile, mojawapo likiwa ni amri inayokataza watu kuishi mabondeni toka zama
za Mzee Makamba alipokuwa mkuu wa mkoa wa jijimkoa.

Nchi haiwezi kamwe kujengwa kwa siasa za kujipendekeza, kutaka
kuonekana wema na wazuri na wengine wabaya na unafiki mwingine kama
huo. Ni lazima tufike mahala ambapo sheria zetu zinalinda na kutunza roho
za watu, kisha utamaduni, imani na mali za watu . Mengine ni uzandiki wa
kisiasa ulio na melngo binafsi dhidi ya yale yanayostahili kuwa ya umma.
Ninaamini, wakati tunatoa michango yetu kuhusu katiba yetu mpya itulinde
vipi tokana na wale tunaowapa ukubwa tutahakikisha kuwa ulinzi na
usalama wa roho za watu, utamaduni na mali zao unapewa uzito
unaostahili.

Kama azma yetu basi itakuwa ni hivyo ni dhahiri kubainisha hapa kwamba
huwezi ukalinda na kuthamini maisha ya wananchi wako kama wewe kama
serikali na mkusanyaji mkuu wa kodi na mirabaha unashindwa kuwapatia
wananchi unaowaongoza mahitaji yao ya msingi. Mahitaji hayo ya msingi ni
pmoja na nyumba na makazi bora na salama.


Nyumba kama hitaji la msingi

Kichekesho kwa wazungu na wageni wengi wanaotembelea nchi hii ni pale
wanapokuta kuwa kila Mtanzania ana mradi wa kujenga nyumba. Pengine
hawaelewi umasikini na kudunduliza kwetu na jinsi tunavyozaliana kwa
wingi, lakini bado ukweli unabakia pale pale wengi wanatushangaa
wanapoona badala ya kujenga vitu vya kututajirisha tunajenga vitu vya
kutumasikinisha.

Ukiweka siasa pembeni, nyumba ni hitaji la msingi la kila mwanadamu.
Inasemekana baada ya chakula na maji basi nyumba ni muhimu kuliko kitu
kingine. Kutokana na ukweli huu, serikali iliyokuwa makini haiwezi
kulichukulia suala hili kimzahaha mzaha au kuliona ni mzigo na kulisukuma
ili libebwe na watu wengine. Bila watu kuwa na nyumba bora na salama hata
kama watajishughulisha na mengi mazuri katika uzalishaji na ujenzi wa
nchi, fumba na kufumbua, siku moja vyote vinaweza kuoshwa au kufagiliwa
mbali na maafa ya aina hii au ile.

Serikali inayoona mbali na mbele, kwa hiyo, huwa inachukulia suala la
mipango na mikakati ya nyumba na makazi kama jiwe la msingi la
maendeleo la taifa na watu husika. Inafanya hivyo, kwa kuzingatia kuwa vita
vyote vingine vinavyokabili watu wake vikiwemo vile vya ujinga, njaa, maradhi
na umaskini ni vita vitakavyokuwa rahisi sana kuibuka kidedea kama
washindi wasioshindika.

Katika muktadha huu, hoja yangu hapa ni kwamba tusianze kumwaga
machozi ya mamba huku tukijua fika kwamba siasa zetu za kujipendekeza
zimechangia si haba kuwapotezea Watanzania wenzetu ambao kama sheria
zingelikuwa zinawalinda na rasilimali za nchi zinatumika kuwanufaisha wao
na sio vinginevyo hivi leo wasingelikuwa marehemu.

Ninasema hivyo, kwa kudhihirisha kuwa ulegevu na urojorojo wa seriikali
yetu ambayo kwa kushangaza sana inakuwa na nguvu ya kupambana na
waandamanaji toka vyama vya upinzani au wafuasi wa dini fulani
wanapotaka kuandamana au kuwasekwa ndani na kuwashtaki waandishi wa
habari kwa kutumia sheria za kidhalimu na kikoloni na zilizopitwa na wakati
kwa sababu tu waandishi hao wa habari wameandika kisichowafurahisha
wanasiasa walioko madarakani unachangia si haba nchi hii kuwa na
matatizo ya kila namna, kutokuendelea na kupiga maktaimu wakati watawala
wakidanganywa na takwimu na taarfifa za wapambe wao kwamba mambo ni
saaafii.


Mradi wa kuondokana na makazi ya mabondeni

Mathalani, kama serikali yetu ingelikuwa haifanyi kazi kisanii, basi mara tu
baada ya kutangaza marufuku ya kujenga na kuishi mabondeni
nilichotegemea kuona ni serikali hiyo kujenga nyumba za angalau chumba
kimoja na ukumbi kwa familia husika katika maeneo mengine na kisha
kupitia benki na taasisi nyingine za fedha, misaada na ukopeshaji kurejesha
gharama zake kwa kuwalipisha wananchi masikini kwa kiwango
wanachoweza kulipa hadi deni lao liishe. Je, tunakumbuka mikopo ya miaka
25 hadi 50 ya Benki ya Dunia kwa watanzania miaka ya huko nyumba.
Serikali yetu kwa kutumia utajiri, madini, mali asili zetu na kodi zetu hivi
inashindwa kufanya jambo kama hili au haina nafasi na watu wake ambao ni
maskini? Utaratibu huu utaendana hata na matarajio ya katiba ya kiutawala iliyopo na
utaanza kujenga kutoa fursa sawa kiustawi ili kuleta uwiano na usawa wa
kimaendeleo miongoni mwa Watanzania.

Hitaji la nyumba na makazi kama hitaji la msingi likishatoshelezwa, kinachobakia ni kwa wananchi kujiingiza katika ushindani mbalimbali wa kujiendeleza kielimu, kikazi, kibiashara, kihuduma, kisanaa, kimichezo na kadhalika na kuwa bora zaidi nchini na
duniani.

Kwa maneno mengine, safari ya kweli na dhati kuelekea kwenye
maendeleo ya Watanzania inakuwa ndio imeanza na sio vinginevyo.

Nyumba zilizo kwenye maeneo safi, bora na salama zitachangia sio haba
kuwapa mamilioni ya Watanzania utulivu wa akili na kiroho. Ni kitu
kitakachorahisisha miingiliano ya kijamii na kupatikana kwa huduma za
utumaji na upokeaji barua kupitia makasha nyumbani na sio ofisi za posta
mbali na waishipo watu. Hali kadhalika, kuishi kwenye makazi salama, mandhari nzuri

na yanayopendeza vitawapa Watanzania moyo wa amani, utu, huruma na mapenzi zaidi.


Na kubwa zaidi litawapa Watanzania nafasi kubwa zaidi ya kujiheshimu na
kujithamini na sio kujiona wao sio lolote sio chochote.

Nyumba bora na salama zitawapa watoto wa kimaskini nafasi ya kusoma
katika mazingira bora zaidi na kufanya vizuri zaidi katika shule na vyuo.

Nyumba bora na salama na zenye nafasi zitawapa watoto wa makini fursa
ya kuwa watundu, wenye kujaribu na wazua ujasiriamali wa kila aina siku
zote daima.

Nyumba bora, salama katika miji ambayo utawala wa kisheria sio tu
unasemekana kuwepo bali kufuatwa kwa herufi na silabi na zenye
kuhudumiwa ipasavyo na huduma zote muhimu za kijaami unaweza
kuifanya Tanzania fumba na kufumbua kuwa chaguo la watalii duniani na
mapato ya utalii peke yake yakatuwezesha kujivua nguo za mitumba ya
umaskini na kuvaa nguo mpya za raia wanaoheshimiwa, kujiheshimu na
kutoa mchango wao muhimu katika maendeleo ya dunia yao na wakati wao.

Kubwa zaidi ni lile la kwamba kuanzia hapo hayo hapo juu
yatakapozingatiwa watu wetu sio tu itakuwa ni rahisi kupata huduma zote
muhimu binadamu anazohitaji, bali kubwa zaidi maisha na mali zao
zitakuwa salama wakati wote.

Friday, December 16, 2011

CUF na hatima ya upinzani Tanzania...

WATANZANIA mnamo mwaka 1990 waliupokea mfumo wa vyama vingi kwa matumaini makubwa ya mageuzi na mabadiliko chanya katika mfumo wao wa kisiasa, kijamii na kiuchumi. Awali CUF kilihofiwa kuwa chama chenye udini, akheri, ni dhahiri inaweza kuwa au isiwe hivyo, ila kilicho wazi ni kuwa CUF baada ya muafaka ni chama cha Kizanzibari zaidi na sio cha Kitanzania, achilia mbali kuwa cha Kitanganyika.


Watu wengi waliamini mfumo wa vyama vingi utaleta ushindani wa kweli katika siasa, uchumi, teknolojia, utamaduni na rasilimali ziendazo kwa wanajamii ili kila mtu na kila jamii ipate kilicho bora kabisa na sio kitu hafifu, dhaifu na vilivyochakachuliwa.

Hata hivyo, ushindani katika sekta nyingine ulitegemea sana kuwepo na mafanikio ya ushindani wa dhati na wa kweli katika siasa. Ushindani huo katika siasa hadi hivi wa leo haujafika, haujaonekana na kwa siasa zilizopo ndani na nje ya chama tawala haionekani kama utapatikana kwenye awamu hii.

La kusikitisha ni kuwa siasa za mfumo wa vyama vingi Tanzania zimeiga neno kwa neno siasa za Kimarekani zinazotawaliwa na wenye fedha, na wasio na fedha kuwa wasindikizaji kama sio wanunuliwaji. Na kinachopandwa hakiashirii mema kwa nchi hii na watu wake hapo baadaye.

Kubwa tunalojifunza hapa ni kwamba kutokana na kukwamishwa kuwepo kwa ushindani wa kweli wa kisiasa ndani na nje ya bunge, viongozi wetu wanawapotezea wananchi muda na nafasi nyingi na nyinginezo za kuondokana na umaskini wao kwa kutumia fursa na changamoto ambazo aghalabu huzaliwa tu katika mfumo wenye ushindani wa kweli kisiasa. Hili linapaswa lionekane na lieleweke na wote, waliomo kwenye upinzani na wanaoongoza chama tawala hivi sasa ili maamuzi yanayofaa yafanywe kwa faida ya nchi na watu wake.


Ilitegemewa kuwa vyama vya upinzani vingekuwa vingi, lakini kuna viwili au vitatu vitakavyoungana na kukipa changamoto ya kutosha chama tawala. Kiasi ambacho chama tawala kisingeweza kufanya maamuzi yoyote ya maana kiurahisi bila ushirikiano na vyama vingine na kuwaelimisha na kuwaridhisha wabunge au wawakilishi wake kwenye mazungumzo mbalimbali.

Kinachoonekana leo, hata hivyo, ni kuongezeka vyama vya siasa visivyo na kichwa wala miguu, huku vile vilivyokuwepo vikizidi kudhoofika kwa njia moja au nyingine.

Zipo sababu mbalimbali zinazotolewa kuhusu udhaifu wa upinzani. Baadhi ya viongozi wa vyama tawala wanaamini kwamba vyama hivyo vimeanzishwa kwa shinikizo la IMF na Benki ya dunia, na hili pengine linaathiri mahusiano ya chama tawala na vyama hivyo kwa chama tawala kuona ndicho pekee chenye ridhaa na uhalali kwa wananchi lakini sio vya upinzani.

Aidha, vyama vingi vya upinzani pamoja na sheria ya kuvilazimisha kuwa na wanachama angalau 200 katika angalau mikoa 10 ni vyama vilivyokosa mizizi ya kweli mijini na vijijini na vinaishi kwa kubangaizabangaiza tu. Wakati hili linatokea chama tawala kwa kushika funguo za hazina na kuwa katika nafasi ya kufanya maamuzi kadhaa kwa manufaa yake, hakina dhiki kama hiyo, ila pale kinapoingizwa mkenge kama ilivyotokea kwenye suala la rada.

Kutokana na chama tawala na viongozi wake kuwa na uwezo wa kifedha (ambao hatuna uhakika na chimbuko lake, maana hakionekani kuwa na miradi ya maana ya kukiingizia kipato na wanachama wake wengi sio walipa ada wala watoa michango mikubwa) kimetumia njaa na umaskini wa vyama vya upinzani kwa manufaa yake kwa njia mbalimbali, ambazo hatuna sababu ya kuingilia kwa undani zaidi hapa. Pamoja na hayo kutokana na siasa kuitwa mchezo mchafu tumeshuhudia mambo ambayo yanatia mashaka kuhusu ukweli na uhalali wake katika maeneo mbalimbali ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kimaendeleo kwa ujumla.

Kisiasa kwa mfano tumeona baadhi ya vyama vikisingizia vingine udini, wakati ndivyo vinavyolea udini kwa mlango wa nyuma; tumeona uoza na ufisadi ukiswafishwa na kuitwa utakatifu; tumeona wabunge wakizomewa na kukashifiwa kwa kuwa na msimamo fulani; tumeona wabunge wakitumiwa kwa manufaa ya chama na serikali na siyo ya wananchi; tumeona watu wakisingiziwa uongo na wengine kujiita na kutaka kuonekana watakatifu na kadhalika; na juu ya yote tumewaona wanafiki na wasioitakia nchi yetu mema wakijifanya wao ndio wenye uchungu mkubwa kabisa na nchi yetu kuliko watu wengine.

CUF na Zanzibar....

Baada ya kukerwa na ugomvi wa ndugu wa Unguja na Pemba, sisi sote tulivuta pumzi na kushukuru Mungu na tukafata wahenga waliyosema: ' Ndugu wakigombana, chukua kisegerema chako uende kulima; na ndugu wanapopatana, chukua kapu lake ukavune!'

Hebu turudi nyuma kidogo, hata hivyo, je, CUF kiliundwa makusudi na mahsusi kwa ajili ya muafaka wa Zanzibar? Au nini kilichotokea?

Pamoja na ukweli kwamba cham hicho kilistahili kuwa na wanachama 200 katika kila mkoa angalau kwa mikoa 10 Tanzania bara na visiwani ni vipi chama hicho kikamezwa kabisa na Wazanzibari? Kiasi kwamba kama chama hicho hakikuhusiswa na Uzanzibari na Upemba kilikuwa kikihusishwa na Uislamu kwa heri au shari ?

Je, katika hali ambayo tunayo leo, yaani, kuwepo sio tu muafaka bali pia serikali ya Umoja wa Kizanzibari, ukweli hauonekani kwamba chama cha CUF hakikuwa chama cha Tanzania bali cha Kizanzibari?

Iweje baada ya viongozi wa Kizanzibari kupewa ubunge na vyeo mbalimbali katika serikali yao ya Umoja wa kitaifa harakati zao za kisiasa kama upinzani unaotarajiwa kuwa imara katika kuikabili CCM bara kudhoofu na kuwa hoi bin taabani?

Katika matukio ya kitaifa na hususan Bungeni, tumeona watunga sheria wa CUF kwa heri au shari wakiunga mkono au kupinga moja kwa moja lolote lile ambalo Chama tawala liliunga mkono au kupinga ?

Na hivi Hazina, Tume ya Uchaguzi na Msajili wa vyama vya siasa wanastahili kulipa CUF na CCM kama chama kimoja au vyama viwili kwa hali kama hii?

Wamasheria wanasemaje kuhusu CUF hapa Tanzania kama ni chama cha Upinzani au chama tawala au chama kilicho katikati ya hayo ?


Na Watanzania waliohadaiwa na wapanda mabasi ya muafaka wakidhani wanapelekwa kwenye upinzani imara na wa kweli wana kila haki ya kushuka na kupanda basi jengine.

Vijana wa chama ambacho kimefikia kuwauza bila wao wenyewe kujua wanauzwa ili viongozi wachache wa chama hicho wapate ukubwa na sio maendeleo ya watu na nchi yao sio laiki yao kukaa kimya labda wakose kiongozi wa kuwafungua macho na kuwaongoza kwenda kule wanakosatahili kuelekea na sio vinginevyo.

Maana ya kuwa na upinzani nchini haiwezi kubadilika. Upinzani unahitajika kama njia muhimu ya kisiasa kwa wanasiasa wa mrengo fulani kupimwa kiuwezo, kufuatiliwa, kudhibitiwa na kutathminiwa kimatendo na kimatokeo kama na wanasiasa wenzao na wananchi kwa ujumla kama wanaweza au hawawezi kazi waliyoiomba.

Huu ni mfumo ambao ukiutumia vibaya unaweza ukairuhusu nchi kutawaliwa na kuendeshwa na chuya na pumba wakati nafaka zimetupwa jalalani. Au kwa upande mwingine mfumo wa vyama vingi ni mfumo unaoweza pia kuchangia sio haba nchi kuwa na viongozi safi, wenye uwezo, wenye nia ya kujenga nchi na watu wao na wenye mitazamo na dira za kimaendeleo zinazohitajika kufikisha nchi na watu wake kule wanakotaka kwenda.

Upinzani hauwezi kustawi kama katika nchi husika bado watu wana wasiwasi kwamba upinzani ni uasi, vita na uhaini. Ni lazima watu na hasa vijijini waliko wananchi wengi wakubali kwamba mfumo wa vyama vingi ni kitu kizuri na anayeutega au kudhoofisha ni adui wa nchi na watu wake. Na kwamba upinzani si ubaya, si uasi na sio vita wala uhaini. Na kwamba vita na uhaini hutokea pale demokrasia inapohujumiwa na wale walioko madarakani kukataa kushindwa na kuwanyima washindi haki yao kwa njia halali au haramu.

Juu ya yote upinzani hauwezi kujengwa na wazee ambao daima wanalilia kupewa nishani ili watambuliwe kwa kile kisichotambulika wala kueleweka. Upinzani wa kweli utajengwa na vijana waliofunguka macho na wanaotambua kwamba nchi hii haiwezi kujengwa kwa kuigeuza shamba la bibi kama sio la nyanya, ila kwa mikoa na wilaya za nchi hii kujiendesha kama makampuni huru yenye visheni na misheni ya kile kinachostahili kuzalishwa, kuundwa au kuhudumiwa kwa ufanifu na ufanisi wa hali ya juu kwa kasi ambayo itatuwezesha kuuaga ulimwengu wa tatu kwa haraka zaidi kuliko tunavyotarajia.

Tusipoangalia demokrasia yetu inaweza kuwa wizi….

SI MTU mwingine ila baba wa ukomunisti, Karl Marx ambaye miaka zaidi ya 120 alitahadharisha kwamba demokrasia kama ilivyokuwa katika nchi za Magharibi ni mfumo wenye udhaifu, mapungufu na kasoro nyingi.

Alionya kwamba demokrasia isipodhibitiwa na wananchi wenyewe ikaachiwa kwa wajanja wachache katika jamii inaweza kugeuka wizi wa mchana kweupe na wa kutisha ambao umehalalishwa na una nguvu za kisheria.

Kiasi ambacho jambo likishaamuliwa huwezi kulipinga kwa kutumia sheria ila kwa njia nyingine.

Alidai wale wanaoitwa wawakilishi wa wananchi wanaweza kuamua kupiga kura ya 'ndiyo' ili kuifagia na kuisafisha hazina au Benki Kuu ya nchi ikawa nyeupe na isibakiwe hata na shilingi moja kwa ajili ya matumizi yao binafsi.

Nina wasiwasi kama huko sio kwa mfumo tulionao leo, wa demokrasia ya chama kimoja iliyojificha ndani ya mfumo wa vyama vingi kama sio tunakokwenda.

Hakuna anayepinga wabunge kupata posho na maslahi zaidi na hata kufanya israfu na kufuru ndogondogo. Kwa mfano, wabunge wenzao wa Kenya wameidhinisha bunge lao kununua viti vipya vya bunge kwa mabilioni ya fedha za Kenya. Kiti kimoja kitakuwa chanunuliwa kwa takriban shilingi milioni tatu. Piga hesabu kwa viti zaidi ya mia tatu bungeni uone mambo hayo. Tofauti na Tanzania viti hivyo havitoki nje vitatoka magereza ya Kenya ambako kuna maseremala wenye hadhi ya kimataifa. Lakini huu ni uwakilishi wa walio nacho kuwawakilisha wasio nacho, ambao wanaamini ili kufanya kazi zao vizuri na kwa starehe lazima anasa na starehe nazo ziingizwe hadi bungeni kwa namna moja au nyingine. Na matajiri kumbukeni hawatopenda wawakilishi wenu waonekane kuteseka au kuwa na maisha ya dhiki au kufanya kazi katika mazingira magumu, kwa hiyo mkiwaruhusu au msipowaruhusu wao watawafadhili bila shida. Ili kuepukana na aibu hii na fedheha ya kufadhiliwa na wenye pesa basi gharama hizo huonekana ni za lazima na zisizoepukika.



Maswali ya kujiuliza

Swali kuu la kujiuliza ni kigezo au vigezo gani vinavyotumika kihistoria na kimapokeo na katika mazingira na hali halisi au muktadha uliopo hivi leo ? Swali hili linazaa maswali yafuatayo:

. Wabunge wetu wana umuhimu na utakatifu gani wa kustahili kulipwa vizuri kuliko madaktari, wahadhiri, wahandisi, walimu, manesi na watu wengine kama hao?
. Hivi kweli hiki tunachokiona katika luninga, yaani, bunge la kusifia na kujisifia na kujipalilia na bunge la NDIIIIYO.... ndicho Watanzania watakachokubali kwacho wabunge kulipwa kihalali na sio kidhulumati ?
. Hivi bunge letu kazi yake ni kutatua matatizo ya wananchi na kuwawezesha wananchi wetu au kazi yake ni kuwapatia fursa wabunge ya kutumbua na kutanua?
. Je, badala ya kuwa na bunge moja tukawa pia na bunge la makundi ya kimaslahi, yaani, bunge la pili muda wa vikao hautafupishwa kiasi wabunge wakashughulikia matatizo yetu badala ya swahifa na swahifa za maneno na porojo?
. Hivi kila mkoa ukiwa na waziri wake mkuu, mawaziri na wawakishi wake nao wakashughulikia moja kwa moja mipango na bajeti zao bunge au mabunge ya kitaifa hayatahitaji tu wiki moja kila baada ya miezi mitatu kuzungumzia mambo makubwa ya kitaifa badala ya utaratibu wa sasa unaotudumaza badala ya kutukuza?
. Hivi na wanaopiga porojo, wanaolala, wanaozomea na kupiga vigelegele nao wanastahili posho hii?

. Mfumo wetu wa bunge hivi unalandana na ule wa kikoloni au kibepari ambao umejengwa katika hoja kuwa watu ni matajiri na sio masikini au vipi?

. Huko Malasyia viongozi wakiwemo wabunge walijipa miaka kadhaa ili kwanza wawatoe wananchi kutoka kwenye umaskini wa kutisha na kisha ndio wabunge wakaanza kulipwa vizuri na kutanua, je, wabunge wetu wanapoanza kwa kutanua kuna uwezekano wowote kweli kwa sisi kukombolewa kiuchumi na kijamii? Wanakubaliana na falsafa ya wabunge wa Malaysia au hawajaona ndani? Ukizingatia hulka au saikolojia ya binadamu, tuna ubavu wa kuifikia Malaysia hata 2100 kwa namna za posho kama hizi za wabunge wetu ?
. Kuna uwiano gani kati ya kile wabunge wanachofanikisha kiuchumi na kijamii kwa wananchi na kile wanacholipwa ?
. Je, uwezo wetu wa kukusanya kodi na kipato chetu cha kila mwaka unaturuhusu kulipa posho hii?
. Je, mabilioni ya fedha yatakayolipwa kwa namna hii hayawezi kuwekezwa kwanza katika mradi utakaozalisha ili posho hiyo itokane na kinachozalishwa na sio kuiingizia hazina shimo jipya la kuchotwa fedha kila mwaka? Hivi wabunge wetu wana akili za uwekezaji au wanazisikia tu na wanataka wawe nazo wananchi lakini si wao wenyewe?
. Je, kwanini mhadhiri, mwalimu, polisi, daktari na nesi nao wasipate posho kama hii? Hasa ukizingatia mazingira magumu wanayofanya kazi na majukumu watumishi hawa waliyonayo kwa wananchi wenzao ?
. Je, uwezo wetu wa kiakili unatufanya tujali faida au manufaa makubwa zaidi kwa idadi iliyo kubwa zaidi au kinyume cha hayo?
. Ni miradi mingapi mbadala ambayo ingesaidia watu wenye kipato cha chini kuondokana na umaskini inakwamishwa kwa hatua hii?

Sababu za baadhi ya wabunge kuridhika na hili

Wabunge nao ni binadamu na mahitaji yao yanaongezeka kutokana na ukubwa walio nao na tamaa zao za kifahari licha ya umaskini wa watu wao; wanataka kulimbikiza ili kushinda uchaguzi ujao; uwakilishi unakuwa fursa ya wao kunyanyuka kiuchumi kama sio kutajirika kirahisi zaidi na mfumo uliopo unatumika kuwanunua bila kujua ili wawasaliti wanaowawakilisha na kutetea walioko mamlakani hata katika yale yanayowahujumu wawakilishwa wao. Aidha katika mfumo ambao wizi wa kura umehalalishwa kinyemela na mbunge hachaguliwi ila kwa kugawa fedha kwanza, wawakilishi hulazimika baadaye kulipa madeni ya watu au kudunduliza tena kile kilichokuwa akiba yao walichokitumia ili wapate kura za wananchi.

Kwanini wabunge wanajisahau
. Wabunge ni binadamu na katika mfumo unaostawi kwa ubinafsi wa kichama na umimi, ubinafsi hauonekani ni kitu kibaya;
. Wabunge walio wengi hawaingii bungeni kutetea maslahi ya wengine ila kulinda na kuendeleza maslahi yao binafsi na jamaa zao;
. Katika mfumo ambao umekwaza na unakinza fani na tasnia nyingine (k.m. mishahara njiwa kwa wahadhiri, walimu, manesi na madaktari ) kimshahara au kiujira, kimasurufu na kimaslahi matokeo yake ni wengi kukimbilia siasa hata kama hawapendi siasa na wanaziona ni uchafu kwa sababu ya fedha au kipato na siyo kwa sababu ya wito;
. Wabunge hawachaguliwi tena kama wawakilishi na watetezi wa wanajamii fulani bali kama watumishi wa chama fulani;
. Mawasiliano kati ya wanaowawakilisha na wabunge huisha mara baada ya mbunge kuchaguliwa;
. Mbunge hafanyi kazi zake ili wananchi wake waneemeke na kutajirika bali kukisaidia chama chake kurudi tena madarakani;
. Nguvu ya serikali na vyombo vya serikali hutumika kukijenga chama tawala na kuvidhoofisha vyama vingine na kutokana na udhaifu wa vyama vingi wabunge kuamini kuwepo kwao kisiasa kunategemea chama tawala kushinda;
. Baadhi ya vyama vingine nyongeza ya posho inapotolewa asilimia kubwa haiendi mfukoni kwa mwakilishi bali kwa chama husika, yaani, nyongeza ya posho ni mlango mzuri wa kustawisha udokozi wa vilivyo vya serikali ili kuwajenga wanasiasa na vyama vyao, na;
. Wawakilishi walio wengi hawaujui umaskini wa wanaowawakilisha. Na wengi huishi katika ukale badala ya kuangalia hali halisi iliyopo hivi leo majimboni mwao.
Majibu ya maswali hayo hapo juu na mengine kama hayo nina hakika ndiyo yatakayoamua hatima ya wabunge na wanasiasa wetu na mustakabali wa nchi yetu bila kujali masuala ya itikadi, msimamo, mtazamo, chama na serikali iliyopo madarakani.


Tanzania tuitakayo

Tanzania tuitakayo haiwezi kupatikana kwa kuwa na wabunge walioshiba na wasiyemjua mwenye njaa, na wakuu wa mikoa wanaokokota badala ya kuongoza mikoa; kwani wao bado waamini wana njaa pia; kwa kutanguliza mbele ubinafsi badala ya jamii; na bwabwaja wa kuzungumza lakini wachache wa vitendo; na vyama na wanasiasa ambao wanajilinganisha na matajiri na kuishi kama wao kama sio kuwapita; na wanaotetea maslahi ya chama au serikali badala ya wananchi wao; na wenye fedha wanaoingia bungeni ili kutajirika zaidi na sio kuwanyanyua wanaowawaklisha; na watu wanaokubali kutumiwa na wengine kwa manufaa ya wengine na sio ya watu wao; na watu wasiojua nchi ilipo na inapotakiwa kwenda.

Ninaelewa maswali hayo hapo juu sio rahisi kuyajibu achilia mbali kuyajibu kwa haraka sana. Ila yanadhihirisha kitu kimoja, muswaada wa katiba si 'blue' wala 'green' wala 'white' paper ya serikali unahitaji muda na wasaa kuusoma na kuutafakari. Na kwamba kama wanaharakati, kazi yetu moja kubwa ni kuitumia katiba ama kuondoa vipengele vyote vinavyowapendelea kiujira na kimaslahi wale wasiozalisha na kuwakamua wanaozalisha kwa upande mmoja na kuviingiza vipengele vipya vyote vinavyohitajika ili kuondokana na dhuluma hii ya kiujira na kimapato ilioyoanzishwa na wakoloni, kulelewa na watawala wetu wa jana na sasa na likachukuliwa kama msahafu au biblia na lisilogusika au kurekebishwa na watawala wetu wa leo. Muktadha huu si msahafu, si biblia na mapinduzi hayaepukiki ili tuwe na Tanzania yenye usawa, haki, utu na ubinadamu zaidi. Tanzania mtu anayelipwa kwa kigezo cha kile alichokisomea na kuhitimu na sio kwa kubebwa kisiasa bila hoja na sababu za msingi. Mungu tusaidie!

Tusipoangalia demokrasia yetu inaweza kuwa wizi….

SI MTU mwingine ila baba wa ukomunisti, Karl Marx ambaye miaka zaidi ya 120 alitahadharisha kwamba demokrasia kama ilivyokuwa katika nchi za Magharibi ni mfumo wenye udhaifu, mapungufu na kasoro nyingi.

Alionya kwamba demokrasia isipodhibitiwa na wananchi wenyewe ikaachiwa kwa wajanja wachache katika jamii inaweza kugeuka wizi wa mchana kweupe na wa kutisha ambao umehalalishwa na una nguvu za kisheria.

Kiasi ambacho jambo likishaamuliwa huwezi kulipinga kwa kutumia sheria ila kwa njia nyingine.

Alidai wale wanaoitwa wawakilishi wa wananchi wanaweza kuamua kupiga kura ya 'ndiyo' ili kuifagia na kuisafisha hazina au Benki Kuu ya nchi ikawa nyeupe na isibakiwe hata na shilingi moja kwa ajili ya matumizi yao binafsi.

Nina wasiwasi kama huko sio kwa mfumo tulionao leo, wa demokrasia ya chama kimoja iliyojificha ndani ya mfumo wa vyama vingi kama sio tunakokwenda.

Hakuna anayepinga wabunge kupata posho na maslahi zaidi na hata kufanya israfu na kufuru ndogondogo. Kwa mfano, wabunge wenzao wa Kenya wameidhinisha bunge lao kununua viti vipya vya bunge kwa mabilioni ya fedha za Kenya. Kiti kimoja kitakuwa chanunuliwa kwa takriban shilingi milioni tatu. Piga hesabu kwa viti zaidi ya mia tatu bungeni uone mambo hayo. Tofauti na Tanzania viti hivyo havitoki nje vitatoka magereza ya Kenya ambako kuna maseremala wenye hadhi ya kimataifa. Lakini huu ni uwakilishi wa walio nacho kuwawakilisha wasio nacho, ambao wanaamini ili kufanya kazi zao vizuri na kwa starehe lazima anasa na starehe nazo ziingizwe hadi bungeni kwa namna moja au nyingine. Na matajiri kumbukeni hawatopenda wawakilishi wenu waonekane kuteseka au kuwa na maisha ya dhiki au kufanya kazi katika mazingira magumu, kwa hiyo mkiwaruhusu au msipowaruhusu wao watawafadhili bila shida. Ili kuepukana na aibu hii na fedheha ya kufadhiliwa na wenye pesa basi gharama hizo huonekana ni za lazima na zisizoepukika.



Maswali ya kujiuliza

Swali kuu la kujiuliza ni kigezo au vigezo gani vinavyotumika kihistoria na kimapokeo na katika mazingira na hali halisi au muktadha uliopo hivi leo ? Swali hili linazaa maswali yafuatayo:

. Wabunge wetu wana umuhimu na utakatifu gani wa kustahili kulipwa vizuri kuliko madaktari, wahadhiri, wahandisi, walimu, manesi na watu wengine kama hao?
. Hivi kweli hiki tunachokiona katika luninga, yaani, bunge la kusifia na kujisifia na kujipalilia na bunge la NDIIIIYO.... ndicho Watanzania watakachokubali kwacho wabunge kulipwa kihalali na sio kidhulumati ?
. Hivi bunge letu kazi yake ni kutatua matatizo ya wananchi na kuwawezesha wananchi wetu au kazi yake ni kuwapatia fursa wabunge ya kutumbua na kutanua?
. Je, badala ya kuwa na bunge moja tukawa pia na bunge la makundi ya kimaslahi, yaani, bunge la pili muda wa vikao hautafupishwa kiasi wabunge wakashughulikia matatizo yetu badala ya swahifa na swahifa za maneno na porojo?
. Hivi kila mkoa ukiwa na waziri wake mkuu, mawaziri na wawakishi wake nao wakashughulikia moja kwa moja mipango na bajeti zao bunge au mabunge ya kitaifa hayatahitaji tu wiki moja kila baada ya miezi mitatu kuzungumzia mambo makubwa ya kitaifa badala ya utaratibu wa sasa unaotudumaza badala ya kutukuza?
. Hivi na wanaopiga porojo, wanaolala, wanaozomea na kupiga vigelegele nao wanastahili posho hii?

. Mfumo wetu wa bunge hivi unalandana na ule wa kikoloni au kibepari ambao umejengwa katika hoja kuwa watu ni matajiri na sio masikini au vipi?

. Huko Malasyia viongozi wakiwemo wabunge walijipa miaka kadhaa ili kwanza wawatoe wananchi kutoka kwenye umaskini wa kutisha na kisha ndio wabunge wakaanza kulipwa vizuri na kutanua, je, wabunge wetu wanapoanza kwa kutanua kuna uwezekano wowote kweli kwa sisi kukombolewa kiuchumi na kijamii? Wanakubaliana na falsafa ya wabunge wa Malaysia au hawajaona ndani? Ukizingatia hulka au saikolojia ya binadamu, tuna ubavu wa kuifikia Malaysia hata 2100 kwa namna za posho kama hizi za wabunge wetu ?
. Kuna uwiano gani kati ya kile wabunge wanachofanikisha kiuchumi na kijamii kwa wananchi na kile wanacholipwa ?
. Je, uwezo wetu wa kukusanya kodi na kipato chetu cha kila mwaka unaturuhusu kulipa posho hii?
. Je, mabilioni ya fedha yatakayolipwa kwa namna hii hayawezi kuwekezwa kwanza katika mradi utakaozalisha ili posho hiyo itokane na kinachozalishwa na sio kuiingizia hazina shimo jipya la kuchotwa fedha kila mwaka? Hivi wabunge wetu wana akili za uwekezaji au wanazisikia tu na wanataka wawe nazo wananchi lakini si wao wenyewe?
. Je, kwanini mhadhiri, mwalimu, polisi, daktari na nesi nao wasipate posho kama hii? Hasa ukizingatia mazingira magumu wanayofanya kazi na majukumu watumishi hawa waliyonayo kwa wananchi wenzao ?
. Je, uwezo wetu wa kiakili unatufanya tujali faida au manufaa makubwa zaidi kwa idadi iliyo kubwa zaidi au kinyume cha hayo?
. Ni miradi mingapi mbadala ambayo ingesaidia watu wenye kipato cha chini kuondokana na umaskini inakwamishwa kwa hatua hii?

Sababu za baadhi ya wabunge kuridhika na hili

Wabunge nao ni binadamu na mahitaji yao yanaongezeka kutokana na ukubwa walio nao na tamaa zao za kifahari licha ya umaskini wa watu wao; wanataka kulimbikiza ili kushinda uchaguzi ujao; uwakilishi unakuwa fursa ya wao kunyanyuka kiuchumi kama sio kutajirika kirahisi zaidi na mfumo uliopo unatumika kuwanunua bila kujua ili wawasaliti wanaowawakilisha na kutetea walioko mamlakani hata katika yale yanayowahujumu wawakilishwa wao. Aidha katika mfumo ambao wizi wa kura umehalalishwa kinyemela na mbunge hachaguliwi ila kwa kugawa fedha kwanza, wawakilishi hulazimika baadaye kulipa madeni ya watu au kudunduliza tena kile kilichokuwa akiba yao walichokitumia ili wapate kura za wananchi.

Kwanini wabunge wanajisahau
. Wabunge ni binadamu na katika mfumo unaostawi kwa ubinafsi wa kichama na umimi, ubinafsi hauonekani ni kitu kibaya;
. Wabunge walio wengi hawaingii bungeni kutetea maslahi ya wengine ila kulinda na kuendeleza maslahi yao binafsi na jamaa zao;
. Katika mfumo ambao umekwaza na unakinza fani na tasnia nyingine (k.m. mishahara njiwa kwa wahadhiri, walimu, manesi na madaktari ) kimshahara au kiujira, kimasurufu na kimaslahi matokeo yake ni wengi kukimbilia siasa hata kama hawapendi siasa na wanaziona ni uchafu kwa sababu ya fedha au kipato na siyo kwa sababu ya wito;
. Wabunge hawachaguliwi tena kama wawakilishi na watetezi wa wanajamii fulani bali kama watumishi wa chama fulani;
. Mawasiliano kati ya wanaowawakilisha na wabunge huisha mara baada ya mbunge kuchaguliwa;
. Mbunge hafanyi kazi zake ili wananchi wake waneemeke na kutajirika bali kukisaidia chama chake kurudi tena madarakani;
. Nguvu ya serikali na vyombo vya serikali hutumika kukijenga chama tawala na kuvidhoofisha vyama vingine na kutokana na udhaifu wa vyama vingi wabunge kuamini kuwepo kwao kisiasa kunategemea chama tawala kushinda;
. Baadhi ya vyama vingine nyongeza ya posho inapotolewa asilimia kubwa haiendi mfukoni kwa mwakilishi bali kwa chama husika, yaani, nyongeza ya posho ni mlango mzuri wa kustawisha udokozi wa vilivyo vya serikali ili kuwajenga wanasiasa na vyama vyao, na;
. Wawakilishi walio wengi hawaujui umaskini wa wanaowawakilisha. Na wengi huishi katika ukale badala ya kuangalia hali halisi iliyopo hivi leo majimboni mwao.
Majibu ya maswali hayo hapo juu na mengine kama hayo nina hakika ndiyo yatakayoamua hatima ya wabunge na wanasiasa wetu na mustakabali wa nchi yetu bila kujali masuala ya itikadi, msimamo, mtazamo, chama na serikali iliyopo madarakani.


Tanzania tuitakayo

Tanzania tuitakayo haiwezi kupatikana kwa kuwa na wabunge walioshiba na wasiyemjua mwenye njaa, na wakuu wa mikoa wanaokokota badala ya kuongoza mikoa; kwani wao bado waamini wana njaa pia; kwa kutanguliza mbele ubinafsi badala ya jamii; na bwabwaja wa kuzungumza lakini wachache wa vitendo; na vyama na wanasiasa ambao wanajilinganisha na matajiri na kuishi kama wao kama sio kuwapita; na wanaotetea maslahi ya chama au serikali badala ya wananchi wao; na wenye fedha wanaoingia bungeni ili kutajirika zaidi na sio kuwanyanyua wanaowawaklisha; na watu wanaokubali kutumiwa na wengine kwa manufaa ya wengine na sio ya watu wao; na watu wasiojua nchi ilipo na inapotakiwa kwenda.

Ninaelewa maswali hayo hapo juu sio rahisi kuyajibu achilia mbali kuyajibu kwa haraka sana. Ila yanadhihirisha kitu kimoja, muswaada wa katiba si 'blue' wala 'green' wala 'white' paper ya serikali unahitaji muda na wasaa kuusoma na kuutafakari. Na kwamba kama wanaharakati, kazi yetu moja kubwa ni kuitumia katiba ama kuondoa vipengele vyote vinavyowapendelea kiujira na kimaslahi wale wasiozalisha na kuwakamua wanaozalisha kwa upande mmoja na kuviingiza vipengele vipya vyote vinavyohitajika ili kuondokana na dhuluma hii ya kiujira na kimapato ilioyoanzishwa na wakoloni, kulelewa na watawala wetu wa jana na sasa na likachukuliwa kama msahafu au biblia na lisilogusika au kurekebishwa na watawala wetu wa leo. Muktadha huu si msahafu, si biblia na mapinduzi hayaepukiki ili tuwe na Tanzania yenye usawa, haki, utu na ubinadamu zaidi. Tanzania mtu anayelipwa kwa kigezo cha kile alichokisomea na kuhitimu na sio kwa kubebwa kisiasa bila hoja na sababu za msingi. Mungu tusaidie!