Thursday, February 21, 2013

Elimu, Mitaala na Utatuaji Matatizo ya Watu na Nchi


Nia na madhumuni ya insha hii ni kujaribu kuwashawishi Watanzania kuona kwamba elimu yetu sasa hivi inaendeshwa kwa namna ambayo haina uhusiano kabisa na matatizo yanayokabili nchi na watu wetu.
                Ninavyoelewa mimi sababu kubwa ya kuwepo kwa elimu ni kusaidia kudumisha daraja la maarifa, nadharia, ujuzi na uzoefu wa waliotangulia na wanaowafatia katika jamii fulani.
                Jamii isiyoweza kurithisha toka kizazi kimoja kwenda kingine maarifa, elimu, teknolojia, mila, desturi na utamaduni wake kiujumla inayozikusanya muongo baada ya muongo sio jamii yenye uhakika wa kuwepo na kuendelea kuwepo katika siku zijazo.
                Urithishaji huu unajumlisha pia urithishwaji wa kizazi kimoja na kingine mbinu, njia na mikakati ya kushughulikia matatizo makubwa na madogo yanayokabili mtu mmoja mmoja na jamii nzima kwa ujumla.
                Inaaminika kwamba nusu ya matatizo ya jamii fulani huhesabika yamekwisha au yameishatatuliwa kama jamii hiyo itakuwa inawafunza vijana wake pamoja na elimu nyinginezo elimu ya kutafuta ufumbuzi wa matatizo yanayoikablili jamii husika.
                Mafunzo  haya hutolewa sio tu kinadharia bali pia kwa vitendo.  Unapotenganisha nadharia na vitndo katika elimu, basi jamii husika huwa inapoteza jambo muhimu sana katika wakati muafaka na sio rahisi kulipata jambo hilo tena katika siku zijazo.
                Kuna wanaoamini kwamba nusu ya matatizo ya Tanzania yanaweza kwisha kwa kuwa na mitaala inayolenga kutatua matatizo yake ya kijamii na kiuchumi.    
Matatizo ya kimaendeleo yanayowakabili Watanzania walio wengi ni pamoja na uadimu kama sio ukosefu wa maji, chakula na nyumba. Aidha kuna udhaifu katika elimu, tiba na afya kiasi kwamba watoto wa Kitanzania wanaendelea bado kusomeshwa nchi jirani na Ulaya au Asia; wakati huo huo wagonjwa wa Kitanzania wanaendelea kutibiwa
nje.
                Kuna tatizo la kukosa matunzo kwa wazee,  mayatima na watoto wa mitaani.      Vilevile yapo matatizo ya kiulinzi na usalama, uhalifu yanayotishia sio tu usalama wa raia mmoja mmoja bali amani na utulivu katika jamii ikiwemo kuongezeka kwa vitendo vya wivi na ubakaji pamoja na kuwa na sheria kali dhidi ya vitendo hivyo.
                Aidha yapo matatizo katika ujenzi na upanuzi au ujengaji upya wa barabara, reli, madaraja, uchimbaji madini, bandari, viwanja vya ndege na ujenzi wa uendelezaji wa miundombinu mingine.
                Kiutamaduni na Kiteknolojia tuna matatizo ya kuoanisha maendeleo ya teknolojia na mila na desturi zetu ili kupunguza gharama na kurahisisha ufanifu na ufanisi katika maeneo mengineyo ya maisha, kazi, sanaa, utunzi wa vitabu, filamu, michezo na burudani.
                Kijamii na kiuchumi matatizo makubwa ni katika ujasiriamali, mikopo na urudishaji wake, mipango, uratibu, uongozi, usimamizi na udhibiti wa mambo kiutawala, kimaandishi na kiteknolojia.  Hali kadhalika kuna masuala ya menejimenti na uendeshaji bora wa michezo, sanaa na uchumiwa utoaji au uuzaji huduma. Aidha kuna changamoto katika uchimbaji na utunzaji au uangalizi wa visima vya maji, bomba, pampu, mashamba ya kisasa, uvuvi na ufugaji wa kisasa, utunzaji na ulinzi wa wanyama pori, nege na viumbe wengine, matumizi bora na makubwa zaidi ya rasilimali nchi kavu, rasilimali kwenye baharini na kwenye maji kwa faida ya wengi na sio wachache.
                Elimu yetu kwa mapana na marefu sasa hivi imeelekezwa katika kujifunza vitu kama historia, sayansi kama sayansi, uraia, jiografia, hesabu, lugha na mambo kama hayo. Kwa maoni yangu masomo yote yanayotolewa hivi sasa iwe kwa shule za msingi au sekondari yanaweza kuangukia ndani ya masomo matatu makubwa: Maarifa ya Namba na Takwimu; Maarifa ya Kunadika na Mawasiliano na Maarifa ya Maisha, Sayansi na Mazingira.
                Fani hizo hapo juu zikipata msukumo wa kuwekwa kwenye mtandao kwa lugha ya Kiswahili na Kiingereza kama itakavyoandikwa na Watanzania wenyewe ni maeneo yanayoweza kutawaliwa kielimu vyema na mwanafunzi yeyote awaye.
                Hayo kwa upande wangu ndiyo yangelikuwa masomo ya msingi kuanzia chekechea hadi sekondari na yakawa ni lazima kuwepo kwenye kila mchepuo kwenye maeneo hayo.
                Masomo yanayotakiwa kupangwa kama ziada itakayotofautisha kati ya mchepuo wa mweleko fulani na mwingine ni mtatizo yalioorodheshwa hapo juu.
                Kwa mpangilio huo mwanafunzi, mathalani,  katika kundi la kwanza la matatizo ya uadimu na ughali wa maji, chakula, nyumba na kadhalika atakuwa akijishughulisha na kujifunza jinsi ambavyo matatizo hayo yanaweza kupunguzwa au kumalizwa nchini. Ni elimu inayomhakikisha kijana nafasi ya kujiajiri au kuajiriwa kwa sababu elimu hiyo itakazia nguvu zaidi katika vitendo na sio nadharia tu.
                Mchepuo mwingine unaweza ukaelekeza nguvu zake katika kujifunza na kurahisisha kuelewa matatizo ya elimu (elimu nayo pia huwa tatizo na lazima kufunzwa na kufanyiwa tafiti dahari ili kuboreshwa mara kwa mara),  tiba na afya  wataanza kugangana na mbinu, stadi na maarifa za ualimu au ufundishaji na uangalizi au utabibu mahospitalini na katika zahanati mbalimbali nzhini zisizo na watumishi wa kutosha.
                Wanafunzi wengine na hususan katika shule za msingi wataelekezwa kutokan na mapenzi na mwelekeo wao katika kujifunza na kulielewa tatizo la matunzo kwa wazee, wajane, mayatima na watoto wa mitaani ili waje kubobea sio tu katika nadharia bali vitendo vya kulipunguza au kuondosha kabisa tatizo hilo.
                Wale wanaopendelea mambo ya ujenzi na miundombinu wataanza kupigwa msasa toka shule za msingi kwa kujifunza juu ya umuhimu, kazi na faida za  nyumba, barabara, reli, madaraja, visima, bandari na viwanja vya ndege, vituo vya kisasa mipakani na usafiri na uchukuzi kiujumla. Kwa namna hii, mtoto hata akimaliza darasa la saba anaweza kuanza kufanya kazi katika eneo hilo na akawa anajiendeleza katika fani yake pasipokuwa na wasiwasi wa kuchanganya kimasomo au kimitaala. Maana elimu hapa inakuwa ikishughulika na tatizo lilipo, linaloeleweka na linaonekana na kila mtu katika jamii.
                Mcherpuo mmoja muhimu utakuwa ule wa kuwapa watoto kuanzia chekechea fursa ya kuonyesha vipaji vyao katika nyanja za sanaa, kuimba, kucheza ngoma na kukatika viuno, kuigiza, kuchekesha, uchezaji mpira wa vikapu na michezo mingine na mambo kama hayo. Kwa kuwa mtoto anaelekezwa kulekule anakokutaka inakuwa ni rahisi kijana wa Kitanzania kuanza kuonyesha vitu vyake akingali bado mdogo na hivyo kumpa nafasi ya kufanza makubwa zaidi hapo baadaye.
                Mabadiliko ya mitaala katika miaka hii pia lazima iwe na mchepuo wa uongozi, utawala, biashara na menejimenti ya vitu hivyo. Ni vizuri hili likaanzia shule za msingi kiasi kwamba mtoto wa Kitanzania akimaliza darasa la saba anakuwa sawa na mtoto wa Kimarekani aliyesomea B.B.A. au hata M.B.A. (unacheka?) nina hakika hili linawezekana kwa kuwa watoto wa Kitanzania kutokana na mzingira yao magumu wanaisoma na kuilewa dunia haraka kuliko watu wa nje katika hili.
                Mwanafunzi anayemaliza masomo katika mchepuo huu atakuwa na uwezo wa kusimamia biashara ya wazazi wake kwa namna bora zaidi kuliko wazazi  hao, na upo uwezekano mkubwa wa mchepuo huu kuzalisha viongozi bora zaidi kwa vyama, vijiji na taasisi nyingine kuliko hali ilivyo hivi sasa.
                Ninakubaliana na wale wote wanaodai kwamba ilikuwa ni makosa kuondoa elimu  ya ujamaa na kujitegemea mashuleni. Lakini kama ikirudishwa, ninashauri ingerudishwa kwa mapana na kina zaidi kwa kuzingatia ulazima wa kuoanisha matatizo ya jamii leo na elimu inayowapatia watu wake.
                Nionavyo mimi, Vyuo vya VETA vinastahili kuitia makali au kuinoa zaidi elimu vijana wetu watakayoipata shule za msingi na sio kuwa mahala pa kuanzia tu vitu vipya kwao. Nikiwa na maana kwamba shule zetu zote za msingi zinahitaji maabara na karakana za useremala, uashi, umakenika na ufundi mwingine ili ziwe kamili na sio nusunusu kama zilivyo leo. Hali ingelikuwa hivyo, leo tusingekuwa na shule za msingi zisizokuwa na madawati na vyoo vya kutosha, na zenye madarasa na majengo mengine yasiyofikia viwango.
Copyright © 2013 Sammy W.I. Makilla. All Rights Reserved.

No comments:

Post a Comment