AMANI na umoja hapa Tanzania una kila sababu ya kuendele
kuwepo ili mradi tu mambo yafuatayo yanaheshimiwa, hayawi tu sera bali yanakuwa vitendo vya kila
siku na wote kwa pamoja tukawa tunakataa kwenda kinyume na kauli na ahadi za
kitaifa kuhusu masuala husika.
Kwanza
viongozi na raia lazima kujiheshimu, kuheshimu wengine na kuheshimiana. Huwezi
ukaendelea kuwadhalilisha wengine au kufanya vitendo vinavyohalalisha
kudhalilishwa wengine na wewe ukaamini kuwa utaendelea kuheshimika. Kiongozi
yeyote wa Tanzania atakayekubali Mtanzania yeyote kudhalilishwa ndani au nje ya
nchi na yeyote yule awaye basi huwa mchangiaji katika hatima ya uvunjikaji
amani na umoja wa nchi.
Mtu
mmoja mmoja, vikundi vya watu, wapangaji, wenye nyumba, wenye mji, wanamtaa,
wanakijiji na wanamji kwa ujumla wao ni sehemu ya Tanzania. Kila mmoja wao ana
wajibu na ana haki zake. Kitendo chochote kinachoruhusu au kuendelea kuruhusu
mtu au watu fulani kununua na kuuza haki za wengine ni kitendo kinachonuiwa na
kinachodhamiria kuvunja amani na umoja wetu. Kisikubalike
Uhuru
wa kweli kwa mtu mmoja mmoja na makundi au jumuiya ya watu pasina uhuru huo
kuingilia uhuru wa wengine. Uhuru ndicho kitu kinachompa uwezo mwananchi au
raia awaye kufanya maamuzi kwa kuangalia maslahi yake na kikundi chake bila ya
kurubuniwa, kuzainiwa, kununuliwa au kushawishiwa kufanza hivyo kwa pesa au
upendeleo wowote uwao. Nchi huru hujengwa na watu huru haijengwi na watu wa kununuliwa au watumwa wa
mtu fulani.
Kama
nchi, Tanzania tunapwaya mno katika medani za ukweli na uaminifu kama watu
binafsi na dhamana tunazopewa kutunza na wenzeu. UOngo haujengi nchi, aghalabu
uongo hubomoa na kausambaratisha watu, vyama na nchi. Ni muhimu katika
uandikaji wa katiba yetu tukarejea suala la kuwa na maadili muhimu ya kitaifa.
Maadili hayo pamoja na mambo mengine yahusu: ukweli kama tabia inayokubalika na wote; uaminifu;
usafi wa mazingira, miili na mioyo yetu; uchapakazi na uwajibikaji wa kiwango
cha juu; tabia ya kujisomea na kujiendeleza baada ya kumaliza shule/vyuo;
kujitolea kusaidia wengine; kujitegemea kama jamii kama hali inaruhusu na ndio
njia peikee ya kutatua tatizo la kijamii na kujitahidi kuongoza kwa vitendo na
sio porojo na maneno.
Hali
ilivyo hivi sasa ni kwamba kuna matajiri na wakubwa wengine wanaojiweka juu ya
sheria na wengi wengine kuwa chini ya sheria. Amani na umoja wetu lazima kufa
kama hapatakuwa na usawa mbele ya sheria kwa wote viongozi kwa raia.
Tusikubali
visingizio vya kihaki za kibinadamu na kisheria kukwamisha mapambano dhidi ya
rushwa. Kwa vigezo na bishara zote mla rushwa na fisadi huonekana maili kumi
toka pale alipo na wala sio siri. Tukiidharau rushwa na kukubali itutawale sisi
kama taifa na sio sisi kuitawala rushwa tutakuwa tumeshindwa katika safari ya
ustawi na maendeleo ya watu wetu kabla hata ya kuanza safari yenyewe.
Kujilinda na kuwa na maofisa habari na mawasiliano pia
wahariri wa habari na waandishi ambao pamoja na
uchanga wao wanajifanya ni
watakatifu na wanajua kilicho bora zaidi kwa nchi na watu wake. Hali katika
kufanya hivyo wakawa ndio wanaopanda
mbegu za ushetani na balaa kwa nchi na watu
wake .
-Kupigwa vita rushwa na ufisadi
Kama
hatutaenzi ahadi na amri mbalimbali ambazo ni sahihi na za haki basi kitaifa
tutakuwa tunabomoa msingi wa amani na umoja wetu. Baada ya kusema hivyo, ni
lazima kwa wakubwa wetu sio tu kuchungua mambo pale tatizo linapotokea bali pia
kuchungua kwa makini, kina na mapana malalamiko yoyote nchini ambayo yanaashiria
kuwepo tatizo kati ya mtu na mtu au watu na watu. Mambo haya yakichukuliwa
kijuujuu yatatufiksha pabaya, kwani yana uwezekano mkubwa wa kuweka umoja na
amani yetu rehani katika mikono ya wachache kwa wema au ila.
Huko
nyuma Watanzania walikuwa wepesi wa kuitana ndugu au komredi. Kuzuka na kukua kwa matabaka kati yetu
kumeanza kunyemelea na kuuharibu udugu na ujamaa huo. Ni muhimu kuangalia kwa
kutumia njia zozote ziwezekanazo tunarudisha
upendo na kukubalika kwa makundi mbalimbali katika jamii na sio kama
hivi sasa ambapo baadhi ya watumishi wa
umma wameanza kuonekana kama maadui na aghalabu wako juu ya sheria za nchi na
maeneo mbalimbali. Udugu na mahusiano mema huzaa kile kinachoitwa mtaji wa
kijamii. Mtaji huu usipokuweko mbio za manendeleo kwa jamii yoyote iwayo hatima
yake ni kuishia sakafuni.
Tuepuke
tabia ya kuwadharau , kuwashusha h adhi na kuwakwaza wengine hadharani pasina
sababu ya msingi ila kwa mtu kujipendekeza na kujionyesha kwa wenzake kwamba
yeye ni mkereketwa na anayewashwa zaidi kuliko wenzako na hasa katika jambo
muktalifuni na lisilokubalika ukweli
wake na watu alimu na wenye uadilifu. Tabia ya kuikweza na kujionyesha wewe
safi na bora kuliko wengine hujenga
chuki na inda isiyo na tija. Aghalabu anayejikweza na kukwaza wenzake
huonekana mbaya, mbinafsi, adui na huchukiwa na wenigi hata na wale anaodhania
wanamshabikia na kumpenda. Maana leo ni yule, kesho aweza wageukia wao.
Kumezuka
tabia ya baadhi ya wanasiasa na matajiri kuwanunua Watanzania wengine kwa sababu moja au
nyingine. Jambo hili sio tu linarudisha
uhadimu kwa watu wetu kupitia mlango wa nyuma bali ni sababu moja kubwa
inayochangia kuua na kuumaliza udugu na umoja wetu, kwa kuwa watu wanaonunuliwa
ni rahisi sana kutumika kufanya lolote lile liwalo, liwe jema au baya mradi
wanalipa deni lao.
Katika
miaka hii ya kugundulika kwa rasilimali mbalimbali nchini upo umuhimu wa kuwa
na fomula ya kitaifa itakayogawa rasilimali na mapato yanayotokana nazo kwa
namna ambayo kule inakopatikana wanaona wanastahili kupata wanachopata na
wengine kugawiwa au kunufaika na kile kinachobakia, ikiwemo serikali na vyombo
vyake pia.
Upo
uwezekano mkubwa wa amani na umoja wetu kudumu kama mambo niliyoorodhoshea hapo
juu yatafanyiwa maamuzi sio kiimla bali kwa kuwashirikisha wahusika au wabia
katika masuala mbalimbali na kufikia maamuzi ambayo yanachangia wote kujiona ni
washindi na hakuna mshindwa.
Kwenye
jamii ya mpito kama ilivyo yetu aghalabu umoja hujengwa kwa kuwa na madaraja
kati ya walionacho na wasio nacho. Aidha kila kinachoonekana kuwa ni kizuizi
katika ukombozi wa wasionacho huwa kinang'olewa haraka kwa faida ya wote.
Rasilimali
zetu ni nyingi na za kutosha. Kinachokosekana ni uongozi, utu na ubinadamu wa kuweza kutumia akili na maarifa
tuliyopewa na Mola ili rasilimali hizo ziweze kutufaa sote bila ya wengine
kutengwa na kusahauliwa. Hii ina maana katika sifa kubwa amabyo viongozi wetu
kuanzia vijijini hadi kitaifa wangepaswa kuwa nayo ni ile ya kukosa kabisa
ubainafsi wenye uharibifu.
Hatuwezi
kuwapata kina Nyerere wengine (watu waliokuwa wanajisahau wao wenywe na familia
zao na kumtanguliza mbele Mtanzania kwanza) lakini tukiwa na maadili bora,
kupata viongozi wenye kudhibiti ubinafsi wao kwa masalahi ya walio wengii ni
kitu kinachowezekana kabisa. Kuna mifano mingi duniani inayoonesha kwamba nchi
zilizochipukia na kuwa tajiri katika miaka ya hivi karibuni ziliongozwa na
viongozi walionyima wao na kuwanufaisha watu wao kwanza, na sio waliowanyima na
kuwakwaza watu wao ili wao wajinufaishe kwanza.
Tanzania katika nchi nyingi za Kiafrika ipo katika nafasi ya
kipekee kuendelea kudumisha amani na umoja wa watu wake kama isipofuata
msaragambo na kuiga yanayotokea katika nchi nyingine za Kiafrika na kwingineko
duniani kwa kuwa na utaratibu wa wazi na usio na usiri katika kuzungumzia mambo
mbalimbali yanayoonekana kuwa ni chanzo cha mtafaruku na maelewano kati ya
Watanzania katika siku zijazo.
Tabia
ya mbuni haifai kwa nchi kama yetu, yaani, kuingiza kichwa chetu kwenye
mchanga, kisha tukajifanya kama vile kwa kuwa hatuoni hatari inayokuja, basi
tukifijificha hatari hiyo haitatugusa na eti tukabakia salama. Athari, hatari
na matishio mbalimbali kwa amani na
umoja wetu lazima tupambane navyo ana kwa ana.
No comments:
Post a Comment