USAFIRI na UCHUKUZI Tanzania uwe wa barabarani, angani au majini umezungukwa na kila aina ya mapungufu na kukosa ukaguzi na udhibiti wa kutosha.
Aghalabu tunakuwa na akili pale balaa linapotokea na roho zinapopotea. Wakubwa na mamlaka zao wamekaa zaidi mkao wa kufurahia ukubwa na vyeo vyao na wala sio kutekeleza kile ukubwa au cheo husika kinachowataka kutekeleza. Na hakuna anayewasema wala kuwachukulia hatua, maana pengine na wakubwa nao wamekaa mkao huohuo.
Maafa kama yaliyotokea mkondo wa Nungwi ni kitu kilichokuwa kikisubiriwa tu kitoke na Mungu aepushilie mbali yapo mengine kama hayo yanayotusubiri kwenye maziwa na bahari zetu, barabarani na angani kama tusipozinduka na kuanza kudhibiti kila kazi inayogusa maisha ya watu hapa nchini, ili kuwe na uhakika na usalama wa maisha ya watu na mali zao.
Ilivyo hivi leo ni kwamba mtu akiwa na fedha au cheo anaweza akafanya lolote hata kama kwa kufanya analolifanya anahatarisha maisha ya maelfu ya Watanzania wasio na kosa. Na sheria zilizopo ni sheria bibi au sheria nyanya ambazo hazimsaidii mzawa kwa lolote zaidi ya mamba kumwaga machozi yao na huruma za kisiasa ili watu wahurumiwe kwa kuonekana wana huruma wakati huruma yao ilikuwa inatakiwa ionekane kwa kuona mbali na mbele, kupanga na tathadhari kuchukuliwa kabla ya janga husika. Ambayo hii kwa hakika ndiyo kazi ya uongozi, yaani, kazi ya uongozi ni kuona mbali na mbele na kuwaepusha wananchi na matatizo yanayoweza kutokea aidha kutokana na uzembe wa watu au amri ya Mwenyezi Mungu.
Hakuna tume itakayoundwa na ikamsaidia mtu yeyote kama serikali na waendeshaji wake wasipojichunguza na kuangalia utendaji wao na kwa kiasi gani unakidhi changamoto za usalama na ulinzi wa raia na mali zao.
Wataalamu wanadhihirisha Watanzania ni wazuri sana kwa mipango na kupanga lakini ni wabovu katika utekelezaji wa kila jambo kwa sababu udhibiti, ukaguzi na ufuatiliaji mambo husika haupo au upo kwa kiwango cha chini sana.
Ieleweke kwamba, hatumlaumu yeyote kwa sasa lakini tukubaliane kwamba 'uswahili', yaani, ubabaishaji au kufanya kazi tu mkubwa anapokuwepo au kwa kubebembelezwa, au kule kufanya mambo kama vile mtu hutaki au kuamini kwamba kitakachotokea ni amri ya Mungu na huwezi kukizuia, sio tu utatugharimu maisha na mali nyingi sisi wenyewe bali utawafukuza pia watalii na wawekezaji watakapoona umezidi na hauvumiliki. Ni lazima tubadilike.
Ingelifaa sote, pamoja na tume husika tujiulize maswali yafuatayo:
.Je ni kweli au si kweli kwamba meli zilizo katika bahari ya Hindi na katika maziwa ya Tanganyika, Victoria na Nyasa ni chakavu na zimeshapita muda wake wa kuishi lakini tunazilazimisha kuendelea kubeba abiria?
.Je ni kweli au si kweli kwamba meli nyingi zinazosafiri kwenye bahari na Hindi pamoja na kuwepo kwa SUMATRA na maofisa bahari na forodha bado zinasafiri bila kuwa na vifaa tosha kama 'lifejackets' kuokoa maisha ya watu meli inapozama? Na kwamba ukaguzi na udhibiti kwa hili ni mdogo mno au sawa na haupo?
.Je ni kweli au si kweli kwamba moto ukitokea katika migodi, nyumba, shule, hospitali, meli, basi au treni ni watu wachache sana watakaonusurika kwa sababu hatua zinazolazimisha kuwepo na vizimia moto vya dharura haziheshimiwi na hazionekani kama ni muhimu. Na Uswahili unatawala kuliko utawala wa kisheria?
.Je ni kweli au si kweli, kwamba barabarani ukishakuwa tajiri au na cheo kikubwa unaweza ukavunja sheria na usifanzwe lolote?
.Je ni kweli au si kweli kwamba wenye mali au vyeo au wapambe wao wanamiliki magari mabovu yanayobeba kama mende mizigo usiku na hayaachi kufa njiani kila siku katikati ya barabara na kuua mamia ya Watanzania wanaoshtukizia wameshaingia nyuma yao.
.Je ni kweli au si kweli, kwamba mamia ya daladala jijini ni mbovu na hazifai kubeba abiria lakini kwa kuwa zinamilikiwa na wakubwa au jamaa zao zipo na zinaendelea kufanya kazi bila kubughudhiwa na mtu?
.Je ni kweli au si kweli, au reli zetu zimeoza na zinafaa kung'olewa na kuwekwa mpya ila kuhakikisha usalama wa wanaozitumia?
.Je ni kweli au si kweli kwamba balaa la maji au mafuriko au gharika ikitokea tutaangaza angaza macho tu kuiongojea nusura ya Mwenyezi Mungu na serikali yetu na tunaowalipa kodi hawataweza kutusaida kwa lolote!
.Je ni kweli au si kweli kwamba Tsunami ikitokea kwenye pwani Pemba, Unguja au Mrima kitakuwa ndio kiama kwa wakazi wengi wa maeneo ya huko maana hatuna lolote kitahadhari tulilowahi kulifanya huko wala tunalolifikiria kufanya hivi sasa?
.Je ni kweli au si kweli kwamba tufani au upepo mkubwa vikiikamia Tanzania hakuna miti wala zana maalum za kupunguza makali ya balaa litakalotuangukia?
.Je ni kweli au si kweli kwamba migodi na machimbo yetu mengi hayana usalama wa kutosha na waliomo humo wanapona tu kwa kudra ya Mwenyezi Mungu?
.Je ni kweli au si kweli kwamba baadhi ya vyakaula na vinywaji vinavyoruhusiwa kuingia nchini toka nchi za nje ni hatari kwa uzima na afya ya Watanzania?
.Je ni kweli au si kweli kwamba maji, vyakula na viliwa vingine katika mahoteli yetu uswahilini yasiyo na vyoo wala vilinda afya na siha havina tofauti na kula sumu. Na kwamba pakiwa na viwango vinavyodhibtiwa sio tu afya na usalama wa walaji vitahakikishwa bali tutajijengea heshima mbele ya watalii, wawekezaji na wageni kwa ujumla?
Katika miaka hii ya utandawazi, hatuna muda wa kupoteza. Ni muhimu kubadilika mara moja. Kazi kubwa kuliko nyingine zote za serikali ni kuhakikisha kuwa maisha na mali ya raia zake inalindwa. Serikali ikiterereka katika hili huo unakuwa ni mtihani mkubwa kwetu sote!
Na je ni kweli au si kweli kwamba ubabe na uzembe wa wenye vyombo vya usafiri na uchukuzi hapa nchini unatokana na thamani ya Mtanzania kuonekana ndogo kuliko ya ng'ombe au punda na fidia ya maisha ya Mtanzania anayepoteza kufa maisha kuwa vijisenti tuchache tu? Na kwamba fidia hiyo ingekuwa kubwa kiasi cha kumfilisi mmiliki wa chombo ajali ZINGEPUNGUA SAAANA!!!
Saturday, September 10, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment