Sunday, November 4, 2012

JKT karne ya 22 inatakiwa iwe vipi ?




Watanzania  wanatarajia kwamba hadi inafikia mida hii ambayo JKT litayari kufungua milango yake kwa wanaJKT wa kizazi kipya kwamba kuna mipnago dhahiri ya muda mfupi na mrefu kuhusu uendeshaji wake; kuna mikakati-mipango sadifu, kuna sera tambuzi na shirikishi na kuna masahihisho kadhaa yaliyofanzwa ili kuoanisha  malengo mapya katika nyakati mpya kwa uendeshwaji wa JKT ijayo. Na kwamba JKT ikisaidina na majeshi yetu mengine itakuwa ndio kichwa cha garimoshi au injini ya kuiendesha Tanzania mpya itakayokuwa inatengeneza na kujenga karibu kila kitu kwa kutegemea rasilimali zetu wenyewe ikiwemo rasilimali watu.
                Kufanya hili lazima pawepo na mpango wa uendeshaji wa mwaka mmoja; mpango wa miaka mitatu - mitano (hususan kuhusu rasilimali mbalimbali)  na mpango wa muda mrefu wa miaka 25-50 inayolenga kuingiza nchi kwenye mabadiliko makubwa kila baada ya muongo mmoja.
                Mipango hii itarahisisha kufahamu ni kwa namna gani JKT itaoanisha matumizi na mapato yake katika uendeshaji wake. Lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa inakuwa ni taasisi inayojiendesha yenyewe bila kutegemea ufadhili toka nje au ndani ya nchi.
                JKT ikiweza kujiendesha yenyewe bila ufadhili na kwa  hiyo kujitegemea itazalisha vijana wanaoweza kujiajiri wenyewe na kujitegemea bila kutegemea kuajiriwa kama njia ya mtu kujipatia riziki yake ya kila siku.
                Mpango-mkakati ni muhimu kwa kuwa mpango huu ndio unaoisadia taasisi yoyote ile iwayo kujua mahala ilipo na inakotaka iwe baada ya miakafulani.
                Ili kufanikisha hili ni lazima tubainishe wazi malengo ya JKT. Bila shaka katika mustakabali wa sasa lengo moja litakuwa ni kuwaunganisha vijana  wenye itikadi tofauti na wanaounga mkono vyama tofauti vya kisiasa kujenga utamaduni wa ushindani-shirikishi, ushindani unaojenga badala ya kubomoa kwa kuheshimu misingi ya haki na usawa kwa kila Mtanzania. Na kwamba vijana wa Kitanzania kuanzia sasa hawatatiwa upofu wa kuchagua kilichooza na kuacha kilicho bora kwa namna yoyote ile.                  Na juu ya yote mtu yeyote mwenye kupiga vita mfumo wa vyama vingi na demokrasia ni adui na sio rafiki wa Watanzania. Na kwamba mtu yeyote anayetumia hila, hadaa, rushwa, fedha na ujanja wowote ule uwao ili kupata cheo au uongozi ni mtu wa kutliwa mashaka makubwa katika safu za uongozi wa taasisi na maeneo mbalimbali nchini.
                Tofauti na huko nyuma katika miaka hii ya upasho na uamsho upo umuhimu wa makambi ya JKT mpya kuheshimu imani  za wanakambi na uhuru wa watu kuabudu na kufuata maamrisho ya dini zao bila kukwazwa na kitu au mtu. Hili likifanyika litawaondoa wazazi hofu kuwa watoto wao wanaweza kwenda kuharibiwa au kupotoshwa JKT.
                Ninategemea pia kuwa JKT itafafanua dhana ya uzalendo iwe pana na wazi zaidi na ianyoendana na wakati. Kwangu mimi Uzalendo sio kukubali kuwa kondoo na kutii au kuridhia kila jambo linaloanzishwa au kuamriwa na wakubwa hata kama ni kosa au uovu; na wala uzalendo sio mavazi, ulimbwende na mapambo yenye rangi za bendera ya taifa.
                Uzalendo ninavyouelewa mimi ni hali ya juu ya utu na ubinadamu inayofikiwa katika nchi fulani. Uzalendo ni juu ya familia, urafiki, ukoo, kabila, imani, uchama na uwana- kikundi wowote ulekatika jamii husika. Mzalendo kwa maneno mengine ni mtu aliye juu ya mambo yake binafsi na ya kifamilia, juu ya masuala ya ukoo na ukabila, juu ya dini au imani yake na ni juu ya siasa za kichama pale utaifa unapohitajika kuwa juu ya kitu kingine chochote.             Aidha, mzalendo ni mtu anayefahamu katiba na sheria za nchi yake na ni mwepesi wa kuhoji na kuuliza ili kupata majibu sahihi kabla ya ya kufanya maamuzi yoyote ya kisiasa, kijamii au kiuchumi, aghalabu, akiliweka taifa lake na utaifa wake mbele ya mtu au kitu chochote kile kiwacho.
                Ili kudadavua na kuibua melengo yanayofaa ni kitu muhimu tuanze kwa kuangalia matatizo au changamoto zinazowakabili Watanzania mijini na vijijini.
                Changamoto hizo ni pamoja na umaskini unaotufanya tushindwe kulipa ujira unaokidhi mahitaji ya wafanyakazi mbalimbali na hivyo kuzusha matatizo ya rushwa, migomo, mitafutano na mengine kama hayo; aibu ya watu wetu kukosa nyumba, maji na umeme na mahitaji mengine ya msingi katika karne hii; mbinu duni katika kilimo na uzalishaji na biashara ya chakula;  kushindwa kutumia bahari, kushindwa kuunda vyombo vya kisasa ili kutajirika na rasilimali bahari na rasilimali kwa ujumla;  kukosa uwezo wa kuchimba na kuuza madini yetu sisi wenyewe na hivyo kuachia wageni kutuibia mali asili zetu kushoto na kulia; ushirikishwaji duni wa Watanzania katika maamuzi na uendeshaji wa nchi yao na mambo yake; kuweza kuwa na mashirika ya umma lakini tukashindwa kuwawezesha Watanzania wengi zaidi na hususan vijijini kumiliki kampuni, biashara a miradi yao yenye kuingiza kipato cha uhakika; kufulia kiteknolojia na  kiviwanda na hivyo kusababisha  kununuliwa kwa kila zana au kifaa toka nchi za nje;  Kushindwa kuitumia teknohama na mifumo ya kidijito kuharakisha maendeleo ya nchi kwa kasi kubwa zaidi;  kushindwa kutoa matunzo na  malezi kwa wazee, masikini, watoto wa mitaani na wajane;  kushindwa kuendeleza miundombinu na mahitajio mengine ambayo yangeweza kumuwezesha kijana wa Kitanzania kung'aa katika soka, riadha, michezo mbalimbali, filamu, maigizo, muziki na sanaa mbalimbali.
                Pasina ushirikishwaji wa dhati na uhakika wa masikini nchini ambao ndio idadi kubwa ya watu wetu hatutakwenda popote.                                Lazima JKT mpya iwe na kitengo mahsusi kinachokaa, kufikiri na kutekeleza hatua mbalimbali zitakazochangia kupiga vita umaskini nchini kwa vitendo na sio kwa nadharia na maneno.
                Kuna wakati JKT iliwakawaka katika kilimo. Nina hakika hali hii inaweza kurejeshwa pakiwa na ushirikiano kati ya JKT, vijiji na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi hasa kilimo na uzalishaji wake kitakapolenga matakwa ya wahitaji binafsi na kile wanachoagiza kikazalishwa kwa viwando vinavyokubalika.
                Ili mapinduzi ya kilimo yafanikiwe JKT inastahili kuzalisha zana mbalimbali za kilimo ikiwemo matrekta, kombaini havesta, malori na mitambo ya kuhifadhi na kusindika vyakula. Ni aibu miaka 50 baada ya uhuru kushindwa kutengeneza vitu kama hivyo sisi wenyewe.
                Aidha, katika mikoa inayopakana na bahari, maziwa na mito mikubwa nitategemea kuiona JKT katiika maeneo hayo sio tu ikijiingiza katika uvuvi na uvunaji rasilimali maji bali pia ikiunda vyombo vinavyohitajika na sekta hiyo ili kuisasaisha au kuifanya ya kileo zaidi.  
                Katika maeneo yenye madini ninatarajia kuona vitengo ndani ya JKT vinavyoharakisha kuwawezesha vijana wa Kitanzania kuwa wachimbaji madini na waendeshaji na wasimamizi wa migodi yetu ili tuonokane na kuibiwa waziwazi.
                Ninaamini makambi mbalimbali ya JKT yatakuwa na vyuo kwa vitendo vitakavyowafundisha vijana sio tu ujasiriamali bali taaluma zote za uongozi na utawala ikiwa ni pamoja na ubingwa wa kupanga, kusimamia rasilimali, kudhibiti mambo, kutafuta masoko na uzalishaji na uuzaji wa kile kinachozalishwa. Chuo hicho kwa kufanya mambo yake kwa vitendo ninakitarajia kuwa kitakuwa ndio eneo la  kupanda mbegu za kuzlisha makampuni ya kijamii kwa watu wa maeneo mbalimbali nchini.           
                JKT ijayo haiwezi kukwepa kuwa na kitendo cha teknolojia na teknohama ili kuiwezesha nchi na hususan vijana kwenda na wakati. Nitategemea watu hodari katika masuala ya kompyuta, simu, tovuti na mawasiliano watakuwa vijana waliopitia na kusomea mambo haya kwa vitendo na sio nadharia tu. JKT kwa maneno mengine itakuwa wadi ya uzalishaji miradi mbalimbali ya kiteknolojia na kiteknohama itakayochangia kuharakisha maendeleo ya Tanzania. Hususan katika matumizi ya tovuti yatakayosaidia kuwakutanisha watu kiteknohama toka Ulaya, Asia, Amerika na kwingineko Afrika wakaanzisha na kuendesha mradi hapa nchini.
                JKT ijayo lazima iwe na kitengo cha ustawi wa Jamii na kufanya kazi ambayo wizara ya afya na ustawi wa jamii meshindwa kwa kiasi kikubwa kuifanya inavyostahili.
                Kama ilivyo kwa makundi hayo hapo juu wanamichezo na wasanii wa Tanzania nao wamejikuta ni mayatima. Ninaamini JKT tena kwa faida kubwa sana inaweza kuingilia kati katika hili na kugeuza hali ya mambo ilivyo leo na Tanzania ikaanza kunufaika vilivyo na vipaji vya vijana wake.
                Hayo hapo juu yana maana kwamba JKT inastahili kuwa na mafunzo ya muda mfupi katika masuala ya matumizi sahihi ya silaha, ulinzi na uasktari (pengine miezi mitatu tu) na kisha vijana wakagawanywa katika idara mbalimbali  zenye majukumu ya kutekeleza changamoto hizo hapo juu (kwa miezi sita -tisa au hata zaidi)  kwa ufanifu na ufanisi mkubwa kila mwaka kuanzia pale itakapoanza rasmi.

No comments:

Post a Comment