Sunday, November 4, 2012

Tuna Uhuru wa Bendera, bado Uhuru wa Aina Zingine…


NCHI nyingi za Kiafrika zitakuwa zinafikisha nusu karne mwaka huu au mwaka ujao kama nchi huru. Uhuru huo wa kisiasa au uhuru wa  bendera au uhuru kutoka kutawaliwa na mgeni na kutawaliwa na mwenyeji ni mchakato wa asili kama vile watoto wa kiume au wakike wanapofikia umri wa kuoa au kuolewa na wanavyotoka nyumbani kuanzisha nyumba yao mpya.
                Bila shaka wengi wanajiuliza je, uhuru tuliopigania ulikuwa ni uhuru mmoja au uhuru wa aina nyingi? Jibu lake ni wazi hapa litakuwa kwamba uhuru tuliopigania sio uhuru wa aina moja, bali uhuru wa aina nyingi. Hapa tunachukulia neno uhuru kuwa ni pamoja na staha, heshima, kiwango stahilivu, uwazi na uwajibikaji wanaopewa majukumu mbalimbali kieneo na kitaifa.
                Watu wanajiuliza je, hivi, Watanzania na Waafrika kwa ujumla wakipata uhuru wa kujifunza na kuelewa na hata kuigeuza nadharia kuwa vitendo katika elimu na maarifa mbalimbali  ya dunia ikiwemo kujifahamu na kufanyia kazi kwa vitendo lugha yao ya asili, katiba na sheria za nchi yao ?
                Je, nini kitakachotokea ikiwa kama Watanzania na Waafrika watapata uhuru na demokrasia pana, kiasi cha kuwa na uhuru wa kukichagua chama chochote cha kisiasa kuingia madarakani na pale kinapoboronga iwe rahisi kukiondoa kama walivyokichagua bila mikwara kutoka vyombo vya dola vikiwemo vile vya usalama ? Tutakwenda mbele kijamii na kiuchumi au tutarudi nyuma ?
                Je, hivi hapa Afrika viongozi na watawala wetu wanaridhia, kuchangia na kusaidia
kuona kwamba watu wao wanakuwa na uhuru wa kuiwajibisha serikali na vyombo vya dola au wanawazuia kupata uhuru huo ?
                Je, ni nini kitakachotokea kama Watanzania na Waafika kwa ujumla wanakuwa na uhuru wa  kunufaika kwa mapana na marefu kutokana na ardhi yao na mali asili zao na isiwe ni viongozi na wageni tu ndio wanaonufaika na vitu hivyo ?
                Mathalani, hivi sasa wanaonufaika na ardhi ambayo chini yake kuna madini au vito vya thamani ni viongozi, wanasiasa na wale wanaopewa leseni kuvichimba vitu hivyo. Je, inapojulikana ardhi ya kijiji fulani iko juu ya mgodi wa dhahabu kwanini watu hao wasitajirike kutokana na kuwa wenyeji asili wa ardhi yao wakanufaika tu watu wengine?
                Je, uhuru wa kuzungumza,  kuchanganyika na watu, kuandamana, kufanya mikutano na kuwa na uhuru wa kuabudu na kuwa na mawazo tofatuti na watu wengine ni kitu kinachoheshimiwa na kuvumiliwa au kinashambuliwa na kinapigwa vita kwa kila hali ? Dhahiri au kwa siri ?
                Hivi kweli Waafrika walio wengi wana haki  ya kusafiri na kutembelea nchi nyingine za Kiafrika na ulimwengu. Upo au kuna usanii na porojo kwa kuwa mazingira yameandaliwa kumfanza Mwafrika asiwe na uhuru kama huo?  Na ni wachache wenye uwezo wa kutembea na kuona mikoa mingine ya nchi yao, achilia mbali uhuru wa kuona nchi za nje na huku watu wanataka kukuza utalii wa ndani? Nini kinachofanzwa ili watu wawe na uhuru wa kweli wa kusafiri ikiwa ni kuwepo kwa vyombo vyenye staha na heshima, gharama nafuu na ubora wa kuridhisha?
                Hivi Waafrika ni kati ya watu ambao wanahesabika kuwa na uhuru wa maji na  chakula. Nikiwa na maana ya uhuru huo kuwa ni pamoja na haki ya kupata maji safi na chakula chenye lishe tosha ukiwa mjini au kijijini? Au mahitaji haya ya msingi wanayapata wachache na linachukuliwa kama jambo la kuwaringia na kuwakoga wasiovipata?
                Je, Afrika kuna uhuru wa kusikilizwa na kusikia yote yakuhusuyo na yanayoihusu dunia? Au hali ilivyo ni kuwa sio tu raia bali pia viongozi kuna watu kati yao wanaokaa mkao wa kuwafanza wasikie yale tu wao wanayotaka wayasikie? Hivi vyombo vyetu vya habari, intaneti na mawasiiano mengine yako katika mkao wa kuruhusu uhuru wa mawasiliano wakati wote na kwa watu weote? Na kama uhuru huo haupo au unachezewa ni nini athari kwa nchi yetu na maendeleo yake ?
                Tanzania itafika wapi endapo tutaamua kutumia madini na utajiri wa mali asili ya nchi hii ili watoto wetu wawe na uhuru wa kusoma. Uhuru hapa ikiwa na maana kwamba mtoto anayetaka kusoma na kujiendeleza asinyimwe au asizuiwe kufanya hivyo kwa kuwa tu mzazi wake au jamaa zake hawana uwezo wa kumlipia ada na gharama nyingine za masomo?
                Je, itakuwaje kama Watanzania watachagua uhuru wa afya na tiba bora na wakachagua kuishi na sio kufa ? Ni nini serikali yao iwayo itatakiwa kulifanza na kuhakikisha kwamba uhuru huu unapatikana bila mizungu wala mikwara?
                Je, mikoa yetu inaweza kuwa huru toka serikali kuu na hususan katika masuala ya mipango, mikakati na utekelezaji wake huria bila kuingiliwa na serikali kuu ili kuharakisha kasi ya maendeleo ya mikoa yote nchini ? Kuna wanaoamini wakuu wa mikoa wanastahili kuchaguliwa na sio kuteuliwa, je, hili litaongeza uhuru wa mikoa kwa kiasi gani?
                Tumeona katika nchi kama Cuba, Cape Verde na Malaysia kwamba nyumba sio jambo la anasa. Na kwamba nyumba ni hitaji la msingi kwa binadamu wote. Wapo wanaoamini watu wakiwa na nyumba wanakuwa huru na tayari zaidi kutafuta maendeleo makubwa kuliko ikiwa kinyume cha hivyo. Huwezi ukawa na taifa la wajenga nyumba na waendaao saiti mwaka rudi kila mwaka na nchi ikaendelea!
                Je katika mambo kama vile ujenzi na uendeshaji viwanda, uendelezaji vijiji, mapainduzi ya kilimo, ajira ugenini, ushiriki wenye mafanikio katika michezo ndani na nje ya nchi, maendeleo ya riadha, maendeleo katika tafiti na ufumbuzi, maendeleo na ustawi wa mikoa, uendeshaji mashirika ya umma, yaliyo hai na vitu kama hivyo, je, kukiwa na ushindani na uhuru zaidi wa kuyaendesha Tanzania itapiga hatua mbele au itarudi nyuma ?
                Ni dhahiri kutokana na hayo hapo juu kuwa kuna aina nyingi za uhuru. Na ule wa kwanza, yaani, uhuru wa bendera hauwezi ukawa ni alfa na omega wa aina hizo za uhuru. Aidha, bila kupata uhuru wa aina hizo nyingine ule uhuru w mwanzo wenyewe hauwezi kukamilika.
                Kama hili lasadifu ni muhimu kwamba wakati huu tunapoangalia upya katiba yetu ya zamani kwa madhumuni ya kuwa na katiba mpya ni muhimu sana kuvinjari aina zote za uhuru zinazostahili kuwepo ili tuweze kuwa na mwananchi kamili na sio mwananchi nusunusu.
                Endapo, wabia wote wa nchi wataridhia njia iliyo bora zaidi ni kujaribu kuona tunakuwa na demokrasia pana na yenye kina kirefu kama njia ya kwanza yakuhakikisha kuwa aina nyingine za uhuru kwa njia moja au nyingine kila siku zinapatikana kwa watu wa sehemu na tasnia mbalimbali nchini.
                Matatizo mengi yanayotokea nchini mwetu hivi leo yanatokana na kuwa na demokrasia nusunusu, demokrasia ambayo wakati mwingine inaona kulia,  lakini haioni kushoto; wakati mwingine inasikiliza juu, ikaacha kusikiliza chini; na wakati mwingine inayojali ya mbele, pasina kujali ya nyuma. Hii ni demokraia rojorojo na ambayo ina hatari ya kuvuruga na kusambaratisha zaidi kuliko ya kujenga umoja na kuwa chachu ya kufanikisha maendeleo ya kweli ya kiuchumi na kijamii katika nchi zetu.
                                Nina hakika Tanzania ina kila sababu ya kuwa nyota, lulu na nuru ya Afrika endapo tu dhamira ya kujenga demokrasia ya kweli itakuwepo. Tukitangulia maslahi ya umma kwanza na kuzika ubinafsi, uchama, rushwa za kijinga na upendeleo vitu vilivyoanza kuchipua. Maana sisi tuna mfano wa kuiga na kuigwa. Nyerere. Raia wengine tunaweza tusiwe sawa na Nyerere, lakini kiongozi wetu kuanzia sasa tufanye juu chini awe ni mfano wa Nyerere. Tumtafute. Tumuenzi ili tunusuru nchi yetu, mtu kama huyo !

No comments:

Post a Comment