MZAZI anayetambua kwamba mwanaye ana tabia mbaya, akamuachia
vivyo hivyo bila kumkanya, huwa hajitendei haki wala hamtendei mwanawe haki.
Umekuwa
ni wimbo wa kurudiwa rudiwa kuwa Watanzania hawakopesheki. Ukiwakopa kulipa ni
kazi. Lakini kwa wanaomuelewa binadamu wanafahamu fika kwamba tabia yoyote
hujengwa na malezi na mazingira yaliyopo.
Na
inaeleweka pia kuwa asilimia kubwa ya wanadamu hawana tabia mbaya na ni idadi
ndogo tu ambayo haiaminiki na
hailekezeki.
Nitakuwa
mchache wa shukrani bila kusifu kazi nzuri iliyofanzwa na taasisi za fedha hapa
nchini. Lakini kutokana na ukweli kuwa bado tuna kazi ngumu ya kupigana na
umaskini, ninaamini hata wao wanajua zipo changamoto za zamani na mpya ambazo
twapasa kuzikabili ili nafuu katika umaskini ipatikane nchini.
Nina
wasiwasi pia kwamba baadhi ya taasisi husika zisipojiangalia upya zitajikuta
zinachangia badala ya kupunguza umaskini. Na hili linatokea kutokanana kanuni
na taratibu zilizopo na maombwe katika
masuala mbali mbali ya
kiudhibiti na kiufuatiliaji.
Katika
kutoa mchango wangu kuimarisha sekta hii muhimu nitabainisha mambo kadhaa
ambayo yanastahili kuzingatiwa na taasisi za kifedha na mikopo nchini ili ziwe
na mavuno bora na makubwa zaidi.
Kwanza,
taasisi zikopeshe biashara au mradi na sio mtu. Hali ilivyo hivi sasa ni kwamba
Ali au Agnes ndiye anayekopeshwa. Na taasisi nyingi humuangalia na kumtathmini
Ali au Agnes na sio biashara au mradi husika. Ali au Agnes huwa hafundishwi
wala kufahamishwa juu ya tofauti yake yeye kama mtu na biashara au mradi wake
kama mtu kisheria. Hii ni kasoro inayochangia si haba kushindwa kwa watu
wengi kurudisha fedha wanazozikopa.
Wafanyakazi
na wadhamini wafanze kazi kiurasimu na kiufundi zaidi. Pale wafanyakazi na
wadhamini wanapokuwa na roho ya huruma na kutaka kusaidia mtu badala ya
kumuwezesha mtu kiuchumi/kimkopo ndipo penye kiungo dhaifu kuliko vyote katika
mlolongo mzima wa mikopo na ulipwaji wake. Ni muhimu tukajifunza kwamba nia,
dhamira na uwezo wa mtu kujiondoa toka kwenye umaskini kwa juhudi na maarifa
yake mwenyewe ni jambo kubwa kama ulivyo msaada wa fedha kumuwezesha kufanya
hilo. Lakini yule anayeona ni rahisi kukopa na asifanye la maana na kisha
kuirusha taasisi husika hachangii vita vyetu dhidi ya umaskini bali anaongeza
umaskini wetu. Na watu wa namna hiyo kila kona ni watu wa kupigwa vita na
kutangazwa kama maadui wa maendeleo.
Pasiwe
na mikopo isiyo na akiba. Baadhi ya
taasisi husika kwa kudhania kwamba zinawasaidia maskini, zimeamua kutoa mikopo
bila sharti la mpewa mkopo kuwa na akiba katika akaunti yake. Ninaamini hili ni
kosa na lina hatari kubwa zaidi ya kuchangia umaskini kuzidi badala ya kupungua
kwa wale wanaokopeshwa.
Akiba
na uwekaji na utunzaji wake ni sehemu muhimu na isiyoonekana katika mfumo
wowote wa kibenki na kifedha. Usipokuwepo chochote kinaweza kutokea ndani au
nje ya uwezo wa wahusika na kuleta hasara na majuto makubwa zaidi. Ninaamini,
wakati umefika wa Benki Kuu kuhakikisha kuwa taasisi zote za fedha ndogo kwa
kubwa zinazotoa mikopo sio tu hazitoi mikopo kwa mtu asiyekuwa na akiba hai bali pia na
taasisi zenyewe zinakuwa na akiba kiasi fulani katika benki za biashara na
benki kuu.
Uwekezaji
unaonufaisha wanachama wa taasisi za Kifedha.
Wakati umefika sasa ili kupunguza gharama na riba kwa wajasiriamali,
taasisi za fedha kuangalia uwezekano wa kuwekeza katika miradi sahihi
inayochangia kumuendeleza mwananchi na kupunguza umaskini kiujumla nchini. Ubia
ukianzishwa na mabenki makubwa, mifuko ya hifadhi, bima,makampuni na watu binafsi ndani na nje ya nchi wenye uwezo
na wanaotaka kutoa mchango wao katika vita dhidi ya umaskini kuna mengi
yanaweza kufanyika tena kibiashara na taasisi husika na hivyo mwisho wa siku
gharama na kiasi cha riba kinacholipwa (na wale ambao kwao riba si haramu)
isiwe kikwazo bali kichocheo cha kukopa na kujiendeleza.
Kuwashirikisha
wanafamilia kiuwazi na kimkakati zaidi. Hali ilivyo hivi sasa ni kwamba baba au
mama na jamaa wa familia husika wanahusishwa kama vile ni amana ambayo itadaiwa
pindi mkopaji anaposhindwa kulipa deni lake.
Ninaamini
njia nzuri zaidi ni kumshirikisha baba au mama kama sehemu ya mkopo ili kuondoa
hatari za baba au mama wanaokopa bila mume au mke kuwa na habari ya hili au
lile. Aidha, kwa wale ambao mikopo yao
inatolewa bila mtu kuwa na akiba kwa upande wangu ninahofu kuwa utaratibu wao
unaziongezea familia umaskini zaidi badala ya kuupunguza.
Uchunguzi
wangu binafsi umebaini kwamba kuna tabia ambazo pia zinawakera wakopaji ambazo
ingelifaa zikomeshwe ili kujenga mahusiano bora zaidi kati ya taasisi husika na
wakopaji wake. Ya kwanza, ni ile ya taasisi kutuma 'jeshi zima' kukabili
mkopaji na familia yake pale panapotokea tatizo. Hili linaonesha kuwa
mawasiliano kati ya wadhamini wa mkopaji na taasisi bado ni duni na yanastahili
kuimarishwa toka siku ya awali. Hii ina maana kwamba mkopaji anaweza akapewa
fedha na kuzitumia bila wadhamini kujua kinachoendelea. Na anakuja kushtuliwa
pale tu ambapo mkopaji kaingia kwenye matatizo.
Laiti wadhamini wangelitambua toka awali wangeliweza kuweka
njia zao wenye za kufuatilia au kujiandaa kwa lolote litakalotokea kuliko
kushtuliwa na makomandoo wa mikopo mitaani.
Jambo
lingine ni tabia ya baadhi ya taasisi kuwafungia wakopaji wake ndani (kifungo
cha muda) eti kwa kuwa huo ni utaratibu wa kuwalazimisha kumlipia mwanachama
mwenzao aliyekwama kurejesha marejesho. Katika sheria za asili (natural
justice) hili ni kosa, maana kama ilivyokwisemwa na wahenga kila mtu atabeba
msalaba wake mwenyewe!
Badala
ya majeshi ya kudai mikopo kuwa ndiyo kitu kinachoonekana mara kwa mara
mitaani, ninapendekeza kuwe na majeshi ya kuwasomesha na kuendeleza biashara za
wakopaji.
Endapo
patakuwa na vijana mahiri katika menejimenti, oganaizesheni, usimamizi, udhibiti na uongozi wa masuala ya biashara na taasisi
hizi zikaja pamoja na kuwa na vitabu vya menejimenti na uongozi kwa Kiswahili
nina hakika kasoro zinazotia hofu na uoga mabenki na taasisi za fedha nchini
kumkopesha Mtanzania baada ya muda sio mrefu zitakuwa ni historia.
Katika
miaka ya 60 Japani baada ya vita vikuu vya pili vya dunia ilianza kuzaliwa
upya. Mkunga aliyetegemewa katika mazazi hayo hakuwa mwingine ila benki
zilizoona mbali na mbele za Kijapani. Marehemu Matsushita (National na
Panasonic), Akio Morita (Sony) achilia mbali wakina Toyoda na wengineo
walibebwa si haba kutoka utoto wa ujasiriamali hadi kufikia makampuni makubwa
tunayoyaona duniani leo. Siri ya mafanikio yao ilikuwa ni kwamba benki zilikuwa
zikiwafuata wao kule waliko na wala sio wao kuzifata benki.
Benki
zilikuwa kwa Wajapani wakati huo kama baadhi yake zilivyo leo ni wabia wa
wafanyabiashara, wenye viwanda na wajasiriamali. Wakati mwingine huyu akimbeba
yule, na yule naye kwa wakati wake akimbeba huyu.
Tanzania
sio masikini tu kwa sababu inashindwa kuchimbua utajiri ulio katika ardhi yake,
lakini kubwa zaidi ni kuwa umaskini wetu unatokana pia na mabilioni ya fedha kufungiwa ndani
badala ya kuwa mitaani kuendesha injini ya uchumi wa taifa letu. Wakati umefika
wa taasisi za fedha na mikopo kwanza kutoa elimu na mafunzo yanayohitajika,
kisha wakawa wabia na wajasiriamali na makampuni madogo na kisha wakawa
wateketezi muhimu katika sera zinazochangia kukuza na kupanua uchumi badala ya
kulea na kudekeza uchumi unaochangia kuwa na matajiri wachache lakini maskini
wengi.
Nionavyo
mimi, muamko mpya wa serikali katika kuwatumikia Watanzania kwa njia bora zaidi
hususan katika sekta za fedha na kodi kunaashiria kuwa serikali itakuwa mbele
kuwasaidia wale wote watakaotaka kuwasaidia makini wa Tanzania.
Baada ya kumalizia tu makala haya, nilitazama mdahalo wa
Barrack Obama (Democrats) dhidi ya Mitt Ronney (Republicans).
Kinachodhihirika hapa ni kwamba
changamoto za kiuchumi, kibiashara na kimaendeleo ni sehemu ya maisha. Tunastahili kujipanga, kujifunza na
kujiendeleza kila siku ili kufanya vizuri katika masomo hayo ya maisha. Elimu,
mafunzo, utafiti na ushauri viwe ni vitu vya mazoea na kawaida na sio vitu vya
kukurupuka kukurupuka tu. Asiyejiendeleza hawezi kujiendeleza, wasiojiendeleza hawawezi kuendelea.
No comments:
Post a Comment