Tuesday, November 8, 2011

Ndoa isiyo na tija

Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Hili sio la kutamba, lataka funga mkaja,
Na wengine hulichamba, wasiache kubwabwaja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.


Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Wanandoa hujisomba, wakuja na wasokuja,
Utadhani ni mtumba, hujui aliyeufuja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.

Ndoa ni kitu cha namba, kukua si rejareja,
Yataka mengi kuumba, na sio kwishia moja,
Yataka kujenga nyumba, na pengine kwenda hija,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.

Ndoa sio kama gamba, kuvua halina haja,
Utaonwa ni mshamba, ukabakia mseja,
Ndoa kuvuta kamba, lenu wote kuwa moja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.

Ndoa tamu ya kulamba, ikiwa rojo vioja,
Yataka hali kuvimba, ovyo vitu kutofuja,
Yataka kuvuta kamba, mbele mkajikongoja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.

Akiba anayekomba, upesi kumvua koja,
Na mtaji anayefuja, ni kumshusha daraja,
Maisha yataka gomba, haikubali harija,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.

Ni ndoa yenye ugumba, ndoa isiyo na tija,
Huhasiri na unyumba, pasiwepo na umoja,
Japo mwafunga vilemba, nje watu hawana haja,
Ndoa isiyo na tija, ni ndoa yenye ugumba.

No comments:

Post a Comment