ZIPO habari kwamba serikali ya Uingereza iko mbioni kuandaa utaratibu ambao nchi zinazokataa 'ushoga' , kwa maana ya mwanamme kujigeuza mwanamke na kuwa na haki ya kuolewa na kuwekwa ndani kama mke, zitakuwa zikinyimwa fedha za jamala ambazo kwa Waafrika walio wengi sio msaada ila ni sawa na kurudisha kile ambacho Waingereza na ndugu zao walikwiba, wanakwiba na wanaendelea kukwiba toka kwa Watanzania na Waafrika wengine kupitia ukoloni, ukoloni mambo leo na unyonyaji mkuu wa kibiashara na kiuchumi kimataifa.
Mama wa demokrasia duniani, Uingereza, anataka kwa mabavu kupandikiza ushoga katika nchi za Kiafrika ikiwemo Tanzania kwa kuwazaini Waafrika kwa pipi na shanga kama ilivyokuwa zamani wakati makampuni yake hayachoti tu dhahabu na madini yetu mengine bali pia hata fedha zetu kidogo zilizo katika hazina yetu.
Uingereza ndio nchi iliyoitawala Tanganyika tokea ilipomshinda Mjerumani ikisaidiwa na rafiki zake mwaka 1918-1961 bila kufikia hata nusu ya mafaniko yaliyofanywa na Mjerumani katika miaka yake 30 hivi ya kuitawala Tanganyika. Lakini ndiyo iliyofanikisha kujenga unyonyaji wa hali ya juu wa nchi hii, hadi hii leo ikiwmo kasumba ya viongozi na matajiri wetu kuwapeleka watoto wao kwenda kusomeshwa Uingereza.
Hili hata hivi linatufungua macho Watanzania kwa kutambua kwamba serikali ya Uingereza na Jumuiya ya Madola ni kama vile zinaamini kwamba zimeziweka mfukoni nchi maskini za Kiafrika na kwamba zinaweza kutumia udikteta kufosi kwenye makoo yao chochote kile wanachokitaka wao kwa kuwa ni matajiri na watu wa nchi zetu kwa kuwa maskini wakakubali kirahisi tu.
Hili huwa linawezekana kwa sababu Uingereza na Marekani huwa linawatumia watu waliosoma au kufanya kazi kwao kuja 'kuunyakua' uongozi wa nchi sio kwa sababu nyingine ila kuendeleza maslahi ya Uingereza na Marekani katika nchi husika. Katika wimbi la demokrasia katika nchi zetu hivi sasa tuwe macho sana na viongozi wa kupandikizwa kwa sababu ya nguvu ya fedha. Watu hao kwa kawaida hutumwa na mabepari wa dunia ambao ni kama asilimia 1 tu ya watu duniani kuja kukwiba utajiri wenu kwa kuunda genge la asilimia 0.005 ya mabepari na wanasiasa matapeli ndani ya nchi husika.
Kwa wasiojua dunia ya ubepari tuliyoikaribisha Tanzania ni mfumo ambao unaendeshwa na asilimia 1 tu ya matajiri duniani lakini ulio na sauti na nguvu sio tu juu ya serikali zao bali pia serikali za nchi zinazoendelea ambazo huzitegemea nchi zao. Asilimia hii moja ndiyo inayoipa nguvu asilimia nyingine kama 15-20 za mabepari wa kati wanaokuja kuwekeza katika nchi zetu na kuwanu nua viongozi na matajiri wachache nchini (labda asilimia 2-3), ili kudhulumu asilimia 97-98 ya raia wenzao kwa heri na shari.
Katika hili, mimi sina tatizo hata kidogo kuona wanawake, wazee, vijana, wafanyakazi, wakulima na makundi mengine katika jamii yakifanya uamuzi ya kuandamana na kuwapasha Waingereza na Wamarekani na wenzao kama wao kwamba hatutaki na hatukubali ushoga katika urithi, desturi, utamdauni na mila zetu za Kiafrika hapa Tanzania na kwingineko Afrika.
Ushoga kwa wale wanaoamini katika Quran Tukufu na Biblia ndiyo mambo yaliyosambaratisha nchi za Sodom na Gomorrah. Wakati kuna dalili za Marekani na nchi za Ulaya kuwa katika masahibu ya kila aina, zipo hisia kwamba Waingereza wanachotaka kukifanya ni sawa na mtu anayezama kutaka kufa na wale wanaoweza kuwasaidia na wanaotaka kumuokoa.
Ni kichekesho kwa Uingereza kuwa na msimamo kama huu katika karne ya 22, kama vile bado tupo kwenye karne za 19 au 20.
Inaonekana kama vile Uingereza na nchi nyingine tajiri bado zinaamini kwamba nchi za Kiafrika ni nchi zinazoongozwa na watu ambao uroho na tamaa yao ya misaada vinaweza kuwafanya wakubali lolote lile hata likiwa baya kwa mila, desturi, imani, utamaduni na utu wa watu wao.
Hivi leo uchumi wa Ulaya na Marekani upo kwenye misukosuko sio kwa sababu nyingine bali kwa sababu ya uchumi kukosa haya na aibu au kile kinachoitwa, 'economics without ethics', uchumi bila maadili. Na misaada toka nchi hizo nazo sasa inataka kugeuzwa kuwa ni 'aid without ethics' au misaada bila maadili. Vitu hivi tusivikubali. Na huu ni wakati wa kuwashauri Wazungu kuanza kitu kitakachoitwa uchumi na misaada yenye maadili kama masomo katika shule zao za viongozi na hasa wale wa kimataifa. (Ethiconomics na aideconomics) ili watuelewe na kutufahamu zaidi. Umaskini hauimanishi maskini kukubali kuuza roho, utu na imani yake kwa ajili ya kupewa misaada.
Lakini ni ajabu pia kwa sababu hivi sasa nchi za BRIC-Brazili, Russia, India, Uchina na bila kusahau nchi za Kiarabu, zile zilizokuwa katika ile iliyokuwa ikiitwa Urussi ya zamani, Malaysia, Indonesia, Korea Kusini, Vietnam, Japani na zile za Scandinavia nazo zinatuhitaji zaidi kuliko wao wanavyotuhitaji.
Ili kuwafunza jamaa hawa ningelishauri nchi za Kiafrika kama zilikuwa zikiwapa fursa 8 kati ya 10 Waingereza na wamarekani nchini mwao, sasa zigeuze kibao na kuyapa mataifa haya mapya na yanayokuwa kwa kasi zaidi asilimia 80 ya biashara, uwekezaji na ushirikiano kati yao na kuwabakizia wakongwe Uingereza na Marekani asilimia 20 tu, ili vitisho vyao viwe kazi bure huko tunakokwenda.
Mambo yetu Waafrika kwa kiasi kikubwa yameharibika kutokana na ukaribu na kukubali bila kujiuliza tamaduni za nje, hususan, za Kiingereza na Kimarekani. Ni dhahiri kwamba tungelikuwa tunaujali utamaduni wetu wenyewe na tukashirikiana zaidi na zaidi na nchi tofauti na hizi mbili, hivi leo labda hadithi ya Afrika isngelikuwa hii iliyopo hivi sasa.
Ni nchi za Magharibi na hususan Uingereza, Ujerumani, Ufaransa, Italia na Marekani ndizo zilizochangia na zinazoendelea kuchangia kudhoofisha utu, utamaduni, imani na udugu wetu kwa sababu wanazozijua vizuri kuliko sisi wenyewe. Kutokana na umaskini wetu tumeendelea kuwaganda huku wanatunyonga taratibu.
Huu ni wakati muafaka kwa viongozi wa dini na wafuasi wao nao kuja juu kiddedea na kuwaonyesha mabwana na mabibi zetu wa zamani kwamba Tanzania ya leo sio ya jana na sio nchi ya kuichezea tena!
Viongozi wa dini watumie fursa hii kuzungumza moja kwa moja na walipa kodi wa Uingereza wakiwemo Wakiristo, Waislamu na Wayahudi kuwaomba washinikize serikali ya Uingereza kuachana na wazo la kuinyima Tanzania msaada kwa sababu Tanzania haitakubali ushoga achilia mbali watu wa jinsia moja kufunga na kufungishwa ndoa.
Wakati huohuo, vyama vya siasa nchini hapa na vile vya Uingereza vianzishe vuguvugu la kudai demokrasia katika utoaji misaada na kuheshimiwa kwa haki za nchi maskini katika kulinda utu wa watu wake na mila na utamaduni wao.
Enzi za Uingereza na Marekani kutoa masharti ya kisenge na kiudhalimu kwa Waafrika ninaamini zimepita. Hivi sasa Afrika ina nafasi ya kuchagua na kukataa masharti ya kijinga na yanyochimbua mizizi na kuusambaratisha mashina yake ya utu na utamaduni wake bila sababu ya msingi. Kufuatia ujibari, jeuri na kiburi cha Marekani na Wayahudi, ingekuwa jambo zuri kama nchi za BRIC na marafiki wengine tajiri wa Afrika, zingeingilia kati na kuliziba pengo la bajeti ya UNESCO, kama Marekani itajitoa kuifadhili UNESCO eti kwa sababu Palestina imekubalika kama mwananchi kamili.
Kama mataifa haya makubwa yanaamini kweli katika demokrasia hayawezi kuwalazimisha viongozi wetu kufanya maamuzi kwa niaba yetu. Maana kufanya hivyo ni kuwafunza udikteta viongozi wetu.
Isitoshe baadhi yetu katiba zetu tayari hazikubali ushoga. Je, kwa masharti hayo ya Waingereza hawaoni moja kwa moja kwamba sio tu wanataka kuingilia sheria na katiba yetu, bali pia wanaonyesha dharau kwa serikali na watu wetu ya hali ya juu kabisa.
Wanachostahili kufanya mabwana hawa ni kuwezesha nchi zetu kuwapa fursa wananchi wao kupiga kura ya kukubali au kupinga kuingizwa au kulazimishwa kuufanya halali ushoga nchini mwao.
Kwa jinsi serikali yetu inavyojikuta mchafukoge katika masuala kama ya mkorogo katika suala la huduama za umeme, maji, afya na tiba, ustawi wa jamii na usafi; migodi na madini; ufisadi, EPA na wenzake; mawakala wanavyotumbua na kadhalika na tunavyoambiwa kuwa wanaCCM wenyewe hawaoni mtu wa kupambana na ufisadi ndani ya chama hicho hatujui ni kwa kiasi gani tunaweza kuwa na viongozi watakaoendelea kuonyesha ubabe na ufidhuli kwa wale wanaotutaka tuwe mashoga na wasenge katika dunia hii ieleekeayo kwenye maangamizi ya Sodom na Gomorrah.
Sunday, November 6, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment