NCHI zilizo katika muungano wa Ulaya (EC)zimeifanya kazi ya kujenga umoja kati ya nchi hizo kuwa kitu rahisi kwa
kukubali kuachia baadhi ya madaraka ya kitaifa kwa Umoja huo wa Ulaya.Hii ina maana kwamba nchi hizo kwa pamoja zilikaa na kuangalia mambo mbalimbali na
kisha kukubaliana kuwa kuna mambo haya na yale ambayo yatafanikiwa zaidi endapo yatasimamiwa na Umoja wa Ulaya na sio na nchi moja moja kama
ilivyokuwa huko nyuma.
Hivyo serikali zikaamua kuanzisha taasisi ambazo zilipewa sehemu hiyo ya mamlaka ili zifanye kazi zilizokuwa zikifanywa na nchi moja
moja kwa ufanifu na ufanisi zaidi.Hivi leo huko Ulaya baadhi ya maamuzi na mipango muhimu yanayohusu masuala ya uchumi, siasa, jamii, teknolojia, michezo na
utamduni hayafanywi tena na serikali za kitaifa bali na vyombo mahsusi katika Umoja huo.Hili limechangia kuondoa ukiritimba na ulevi wa madaraka kwa baadhi ya
viongozi Ulaya ambao ulichangia huko nyuma si haba kufanya maamuzi ambayo badala ya kusaidia nchi na bara hili yalikuwa yakiwarudisha watu wake nyuma au
kuwaingiza kwenye migogoro isiyokwisha.
Hili ndilo linalotakiwa litokee pia hapa Afrika Mashariki. Ili kuung'oa mzizi wa fitina unaochangia ulevi wa madaraka na
tabia za kidikteta kwa baadhi ya viongozi na vyama kufikia kiwango cha kudhulumu haki na uhuru wa wananchi kuchagua viongozi wanaowataka lazima pawe na
vyombo vilivyo juu ya vyombo vya kitaifa na pale chombo cha kitaifa kinaposhindwa kuchukua hatua husika kinachukuliwa hatua zinazoamuliwa kijumuiya.Sio siri
Tume ya Uchaguzi ni chombo kimoja tu katika vyombo vingi vinavyohitajika ili malengo yetu ya umoja yaweze kufanikiwa. Mambo mengine ni pamoja na soko moja
la Afrika Mashariki; Shirika moja la Reli la Afrika Mashariki; Shirika moja la Mabasi la Afrika Mashariki; Shirika Moja la Meli la Afrika Mashariki; Paspoti moja ya Afrika
Mashariki; Baraza moja la Mitihani; Shirika moja la Ndege la Afrika Mashariki pamoja na vyuo vikuu, shule, mahospitali, vyama vya kisiasa na kadhalika ambayo
kutokuwepo kwake kumechangia sio haba matatizo yanayozikabili nchi zetu katika maeneo hayo yote kwa makali na maumivu makubwa zaidi kuliko ambavyo
ingelikuwa kama vyombo hivyo vingelikuwa ni vya pamoja.Mfumo wa kisiasa tuliourithi umejenga tabia na mazoea ya viongozi wetu kutaka kuwa na mamlaka
makubwa na yanayoelekea mara kwa mara kupora haki na uhuru wa wananchi kwa njia moja au nyingine.
Na ni kazi kubwa kweli kuwanyang'anya viongozi hao
madaraka na mamlaka fulani kwa sababu baadhi ya wale wanaowazunguka tayari wanafaidika na mfumo huo uliopo. Mfumo unaowapa viongozi nguvu za kupita
kiasi ambazo fumba na kufumbua zinaweza kutumika kulidhuru taifa na watu wake badala ya kulisaidia.Hata hivyo, nadharia za uongozi na menejimenti katika
dunia ya leo zinasema kwamba ikiwa unataka kujenga kitu kikubwa zaidi ni muhimu kwa vile vidogo kuachia ngazi ili maslahi na matakwa ya walio wengi au kwa
kile kilicho kikubwa zaidi kuangaliwa mara moja ili faida au manufaa makubwa zaidi yaweze kupatikana kwa taasisi, nchi na watu wake.WanaAfrika Mashariki ni
muhimu tukubali kwamba ili tufanikiwa katika azma yetu ya umoja wote, viongozi na wananchi tunalazimika kuachia mengi tuliyoyazoea ili ndoto hiyo iwe kweli
mapema kuliko tunavyofikiria.
Tusipofanya hivyo, basi tutazunguka papa hapa na mwishowe tutaisihia katika kutafutana uchawi na yale yaliyoikumba Afrika
Mashariki ya kwanza, Mola apishie mbali, kuikumba pia Afrika Mashariki mpya!Mathalani, ikiwa katika nchi kiongozi na wafanyakazi wa Tume ya uchaguzi
wanachaguliwa na kiongozi aliyeko madarakani haiwezekani kamwe kwa kiongozi wa tume kukaida amri au matakwa ya yule aliyemweka hapo wakati mwingine
kwa upendeleo au kumuokoa mtu aaliyekuwa akizama kimaisha.
Bado katika nchi zetu nyingi kazi na nafasi za kazi hazipewi watu kutokana na ubingwa, uwezo au
utaalamu wao bali kwa sababu za kisiasa na nyinginezo ambazo hatuna muda wa kuzizungumzia hapa. Hili ni lazima libadilike. Na kubadilika kwake ni muhimu
kutenga siasa na nyanja zingine za kimaisha kwa maana kwamba wale wanaochaguliwa kama wabunge, mawaziri na viongozi wa nchi wasijiingize tena katika
masuala ya biashara binafsi na vitu kama hivyo bali watumie muda wao kuondoa umasikini katika nchi zao na nchi zao ziwe tayari kuwapa maisha mazuri
wanapostaafu na sio kumtegemea Mo Ibrahim tu!Hili lifanyike ili kuondoa vishwawishi vya viongozi wasio watu wa dhambi kwa kawaida kutojiingiza katika ufisadi,
wizi wa mali ya umma na vitu kama hivyo.Kisha rasilimali za taifa zitumike katika kulea kizazi cha WanaAfrika Mashariki wanaozawadiwa kwa utaalamu na vipaji
vyao na ambao hawako tayari kuacha fani zao ili waende kwenye siasa.
Hivi sasa hilo linatokea maana wataalamu na watumishiwa umma hawawezi kuwa na
maisha mazuri mpaka wamejiingiza katika siasa.Kutokana na hili upo umuhimu wa kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi ya Afrika Mashariki ambayo itakuwa juu ya
Tume zote huru za Kitaifa na itakayokuwa na uwezo wa kukemea viongozi walioko madarakani ikiwa watajaribu kuwapora wapiga kura uhuru na haki zao za
kikatiba.Zipo faida mbalimbali zitakazopatikana kwa kuwepo kwa Tume Huru ya Uchaguzi hapa Afrika Mashariki. Kwanza, ni jambo muhimu katika kuhakikisha
amani, umoja na mshikamano wetu kama Wanaafrika Mashariki unakuwa juu ya matakwa na ajenda binafsi za viongozi wetu na vyama vyao vya kisiasa.
Hii ina maana, viongozi wa nchi zetu sasa watakuwa wanaogopa kufanya jambo lolote litakalowafichua kuwa ni wakiukaji haki za kibinadamu za nyinginezo katika katiba
za nchi zao na mamlaka za Afrika Mashariki.Ni dhahiri pia kuwa kazi ya kukuza na kuimarisha demokrasia Afrika Mashariki itategemea kwa kiasi kikubwa jinsi gani
ambavyo tunajipanga ili kuwe na vyombo huru nje ya serikali zetu vinavyochangia kuwa na visheni na misheni ya kuipeleka sehemu hii ya dunia kwenye viwango
vya juu vya kimaendeleo na kistaarabu.
TUme huru ni chombo mojawapo kitakachosaidia sana kujenga demokrasia ya kweli hapa Afrika Mashariki.Tume ni
chombo cha kupigania haki za raia. Hii ina maana kuwepo kwake kutasaida sana katika kutenganisha maslahi ya serikali na uongozi na yale ya raia. Tume hiyo
itakuwa ni changamoto kwa serikali zote kuwa na tume huru na inayokubalika na vyama na raia wote.Kazi nyingine kubwa ya T
ume huru ya uchaguzi itakuwa ni kupanga ratiba za uchaguzi kwa nchi zote wanachama na wakati huo huo kusimamia na kudhibiti kazi hiyo iendane na viwango vyote vinavyokubalika
kimataifa.Tume itawajibika pia kuhamasisha na kuoanisha elimu ya uraia kwa nchi zote za Afrika Mashariki na hivyo kuondoa utapeli unaofanyika hivi sasa ambapo nyingi ya fedha zinazotolewa kwa ajili ya kazi hiyo huwa zinaishia mfukoni mwa watu na sio katika kuendesha shughuli hiyo ya kuwaelimisha wananchi juu ya haki zao za kidemokrasia na hasa zile za uhuru, manufaa na haki ya kuchagua mtu au chama wakitakacho.
Tume hii pia itakuwa na kazi ya kuzishauri tume na nchi husika juu ya mambo mbalimbali yatakayochangia kuwa na demokrasia pana na ya kina zaidi katika nchi zetu zote za Afrika Mashariki. Ikiwezekana tume itakuwa na Chuo cha Taaluma za Siasa, Uchaguzi na Mabadiliko ya Kijamii kwa ajili ya wanafunzi toka nchi zote za Afrika Mashariki. Kwa namna hii wafanyakazi wote wa tume zote Afrika Mashariki watapikwa nakuiva ipasavyo ili wawe bora zaidi katika kazi zao na kujenga demokrasia Afrika Mashariki.Sambamba na hili Tume
itakuwa na kazi ya Kuratibu ujio na uwepo wa waangalizi wa kimataifa katika chaguzi na warsha au semina mbalimbali za masuala ya elimu ya uraia na uchaguzi huru na wa haki.Tume itatakiwa pia kuendesha tafiti ambazo zitatusaidia kuona mbali na mbele na kisha kuchukua harua za hadhari kushughulikia masuala yanayoweza kuleta kukosa ukweli, uaminifu na haki katika chaguzi na hivyo kuziingiza nchi katika matatizo ambayo yangeliweza kuepushwa kwa kuzingatia yale tunayojifunza katika tafiti hizo.
Monday, May 23, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment