Saturday, May 7, 2011

Waislamu wanahitaji kuwezeshwa kiuongozi na kiundeshaji taasisi zao

MAAZIMIO kadhaa ya kidini yameandaliwa na kutangazwa hususani Waraka wa Wakatoliki na Mwongozo wa Waislamu katika siku za hivi karibuni. Je, tumejiuliza asili yake ni nini? Maana viongozi wa dini hawawezi hivi hivi tu, kutokana na dhamana, heshima na uzito wao katika jamii kukurupuka tu na kufanya mambo kama haya.

Tujiulize hivi halipo 'ombwe' la utendaji wa kiuongozi, kisiasa na kiserikali ambalo imelazimika lijazwe ? Na wanaolijaza ni viongozi wa dini kwa heri au kwa shari? Kiuongozi ombwe hilo ni ile hali ya kuwa na aina ya uongozi ambao hauna mawasiliano ya kitarafu na wale wanaowaongoza na hivyo kushindwa kujua malengo, matamanio na matarajio yao.

Ombwe hilo pia linachangiwa pia na kiongozi kutojua wanasiasa wenzake na watendaji wa serikali wanachokifanya au wanachoshindwa kukifanya. Kisha kuwawajabisha pale inapostahili. Inadaiwa katika serikali na vyama watu hudhihirisha au kuficha Uislamu au Ukiristo wao kutokana na maslahi na anayegawa maslahi hayo, unafiki mtupu. Kiserikali ombwe hilo linasababishwa na makundi fulani ya watu kuwa huru zaidi kuliko makundi mengine na hivyo badala ya kujenga umoja hujenga mgawanyiko katika makundi.
Tunahitaji kukomaa kisiasa kwa kuacha kushawishika kwa yale moyo unayoyatamani na badala yake tushawishike na kufanya maamuzi kwa kutumia akili zetu, Kipaji pekee ndicho kinachomtofautisha wanadamu na wanyama. Tukikomaa kisiasa kwa kila tamko na kila kitendo, tutakachokifanya kwanza ni kutafakari, kisha kuchunguza chanzo au asili yake, halafu kuangalia athari zake na hatimaye kuangalia jinsi ya kuepusha mabaya.

Katika makala hii hoja yangu ni kuwa tafrani ya dini na serikali iliyopo leo inasababishwa na dini moja kuamini kuwa haisaidiwi na haipewi fursa sawa ya kuchanua na kukua kama dini zingine kwa sababu zisizojulikana—na amani na umoja vitakuwa mashakani hali hii isiporekebishwa. Pamoja na hoja hiyo kuu zipo hoja kadhaa ambazo zipo hapa chini ambazo nazo kwa kiasi fulani zimetufikisha hapa tulipo: Utendaji mbovu wa serikali katika elimu na afya. Ni dhahiri kwamba hivi sasa ni shule, vyuo na hospitali za kidini zinazoendeshwa na kufanya vizuri wakati zile za serikali ni hoi.

Ukichangia na 'MOU' ya Serikali na taasisi za dini za Kikiristo huu umekuwa ni mwiba wa samaki mkubwa kumezwa na Waislamu. Kujirahisisha, kujidhalilisha kwa wafadhili. Haiyamkiniki kwa serikali ya nchi huru na yenye katiba na misimamo yake mingine achilia mbali msingi wa uongozi wa Mwalimu Nyerere, kukubali nchi za nje kutuamulia mambo ambayo yanaweza kutugawa. Uongozi dhaifu kwa Waislamu. Kutokana na wanasiasa na serikali kuingilia mambo ya Waislamu sasa nchi inavuna matunda yake. Inaaminika na wengi, kama Waislamu wangelipata viongozi bora (kielimu na kiutendaji na sio ombaomba na kuinyenyekea serikali) na mifumo huru ya kisasa ya uendeshaji wa dini yao, maendeleo yao yangelikuwa ya uhakika zaidi kuliko ilivyo sasa, na hivyo amani na umoja watu ‘ungegarantiwa’.

Uchumi huria na utandawazi. Miaka sio mingi iliyopita serikali ilitamalaki katika kila shughuli kuanzia elimu, afya hadi viwanda. Hivi leo soko huria na utandawazi kutokana na sera na mwelekeo wa serikali unaoelekea kuwaogopa au kuwapendelea watu wa dini moja zaidi kuliko dini nyingine. Hii ni pamoja na misaada kwa Waislamu kubatizwa misaada ya kigaidi wakati ile kwa wenzao inayotishia umoja na amani yetu imeendelea kuja na kukubalika. Vyanzo na ukubwa wa mitaji tofauti. Wakati baadhi ya dini nchini hazina mtaji wowote wa maana nyingine zina mitaji ndani na nje ya nchi ambayo sasa inawasaidia kununua viwanja, mashamba, majengo na kadhalika na kuanzisha miradi ambayo inawafanya wawe matajiri na wenye uwezo zaidi kisiasa na kijamii. Wakati wale wasiokuwa na mitaji wanaendelea kuwa maskini.

Mipango na Mikakati. Utafiti mdogo nilioufanya umeonyesha kwamba ndugu zetu wa Kiislamu ni dhaifu katika mipango na udhibiti wa shughuli zao. Hii ni tofauti kabisa na Wakatoliki ambao kila kinachoanzishwa kina mpango, mfumo na muungo wa 'oganaizesheni' yake. Kanuni za udhibiti wake na aina ya uongozi unaostahili kuendesha chombo husika. Katika miaka hii ni muhimu kwa taasisi za kiislamu kuwa na 'Rolling Strategic Planning' yake pamoja na matamko muafaka ya 'visheni' na 'misheni' zao. Usimamizi wa fedha.

Utafiti wangu umeonyesha pia kwamba taasisi nyingi za Kiislamu zina usimamizi duni wa mambo ya fedha. Kiongozi anaweza atoke anakotoka na kuchukua fedha yoyote bila kuwajibika kwa mtu yeyote. Fedha ni damu ya taasisi kama isiposimamiwa vizuri huleta madhara zaidi kuliko faida. Umaskini wa fedha na elimu. Waislamu wengi ni maskini kifedha na kielimu. Wanahitaji kuwezeshwa kwa njia moja au nyingine kwa faida yetu sote. Ushahidi wa hili upo katika uhalifu, magereza na mateja barabarani. Muundo na mfumo wa taasisi.

Zipo kanuni na miongozo mbalimbali kuhusu taasisi mbalimbali iwe ya elimu au ya afya au ya fedha na kadhalika. Muundo au mifumo ya lazima inayohitajika kuwepo ili mambo yaende vizuri. Kwa wenzetu kuna upungufu mkubwa na aghalabu taratibu na kanuni za menejimenti ya kisayansi havipo kabisa. Elimu na Uongozi. Wakati makanisani kuna watu ambao ni madaktari, maprofesa na mabingwa wa mambo mbalimbali hivi sivyo ilivyo kwa wenzetu. Inaelekea kama yoyote yule mwenye elimu hatakiwi kwenye safu za uongozi wa juu wa taasisi kiritimbifu inayosimamia mambo ya Waislamu kwa hivi leo. Kutokuwepo Umoja katika wingi.

Yapo madhehebu mbalimbali ya Kiislamu lakini inavyoelekea serikali hutambua mwakilishi mmoja, tofauti ilivyo kwa Wakiritsto ambavyo kila dhehebu lina uwakilishi wake. Hili lazima lishughulikiwe mara moja ili kuwapa Waislamu nafasi ya kujenga umoja wa madhehebu yao. Aidha kwa kuwa Uislamu hauna ubaguzi wa rangi wala kabila hatutarajii kwamba lazima kiongozi wao awe tu Mmatumbi hata kama mtu huyo hana elimu tosha ya dini na dunia. Kwani Wahindi au Waarabu bora zaidi hawawezi kuwa viongozi ?

Misaada toka nje. Wapo wanoamini kuwa misaada toka nje inatakiwa iwe na faida sawa kwa watu wa imani zote. Ikiwa inaonekana watu wa imani moja wananufaika zaidi na misaada sio ya ndani tu bali hata ya nje huwezi ukajenga umoja wa kitaifa. Mwamba ngozi kuvutia kwake. Katika jamii yoyote kila kundi hupenda kuvutia ngozi (manufaa) upande wao. Kazi kubwa ya serikali ni kuhakikisha kila upande una fursa sawa katika vuta hiyo. Serikali inapoonekana kulalia upande mmoja, ndipo matatizo yanapoanza. Mipaka kati ya serikali na taasisi za kidini.

Lazima pawe na mipaka kati ya uongozi wa serikali na wa dini. Na hili linaweza likafanyika vizuri zaidi kwa kuwa na Katiba mpya badala ya hii ya viraka tunayotumia sasa. Maana tunapozungumzia katiba mpya sio suala la kisiasa tu bali ni makubaliano rasmi kati ya viongozi na wananchi kuhusu serikali itegemee nini kutoka kwa wananchi, na wananchi wategemee nini kutoka kwa serikali katika kila jambo. Mawasiliano. Ni muhimu kwa viongozi na serikali kuwa na mawasiliano ya kudumu na viongozi wa makundi makubwa ya kijamii kiasi cha kuwa wakati wote 'wanaanalaizi' ni nini matarajio na kero za makundi hayo na viongozi wake.

Hili litatuwezesha kuepusha kuzuka kwa mitazamo na misimamo tofauti ambayo haichangii bali inajenga nyufa katika jamii yetu. Athari za haya ni nini ?Vipengee vyote nilivyoonesha hapo juu vinahitaji kuangaliwa upya kwa makini na kushughulikiwa kwa namna ambayo athari mbaya zinadhibitiwa. Athari hizo ni pamoja na chuki, wivu, ugomvi usiokwisha, kutishiwa kwa amani na umoja wetu, watu kutoaminiana na wanasiasa na viongozi wa dini 'waovu' kuitumia fursa hiyo kupanda mbegu za 'Kirwanda enzi zile' nchini mwetu.

Watanzania ni jamii ya aina yake ulimwenguni hapa. Karibu kila familia yetu ina Mkiristo na Mwislamu ndani. Baba wa Taifa aliweka misingi madhubuti ya umoja wa Kitaifa iliyojengwa juu ya haki, usawa na heshima kwa wote. Kiongozi wa aina yoyote anapopinda masuala haya ya haki, usawa na heshima ndiye atakayekuwa chanzo cha kuvunjika amani na umoja wetu. Na kiongozi yoyote wa serikali au kisiasa anayeshindwa kuwaambia viongozi wa dini: ' Ya Kaizari mpeni Kaizari, na ya Mungu mwachieni Mungu, ' ni tatizo.

Mwisho, ikumbukwe kwamba taasisi ni kama mwanadamu. Ni kiumbe kinachozaliwa, kukua, kubadilika na kuwa bora zaidi kupambana na mazingira yake kwa jinsi muda unavyokwenda. Kwa hiyo sio sahihi basi kusema kwamba taasisi tulizo nazo sasa zimetosha. Eti kukiwa na taasisi nyingi tutatjivuruga wenyewe. La hasha. Kwa mujibu kwa nadharia za kuzaliwa, kukua, kufa na vingine kuchukua mahala pake kushindwa au kufa kwa taasisi moja au nyingine sio kitu kibaya. Maana ni ushahidi wa kutosha kwamba taasisi hiyo muda wake ulikwisha na haikuwa inahitajika tena na binadamu.

Kuna taasisi tulizonazo leo ambazo lazima zitakufa na ni dhahiri kuna taasisi nyingi nyinginezo zinazoweza kuzuka sasa na zikaishi miaka mingi baada ya sisi kusahahulikwa kwamba tuliishi hapa duniani.

Waislamu wameponzwa na wanaendelea kuponzwa na ukiritimba wa BAKWATA na kwamba taasisi zinazoweza kuiga mifano ya kina Ismailia na Jamatini zao za kuzuia watu wao kushuka chini ya mstari wa umaskini, mabohora na hata Answari Sunna na Wahabi zinahitajika kuliko zilivyowahi kuhitajika huko nyuma ili kuwasaidia Waislamu kushiriki kikamilifu na kwa mapana na marefu katika vita dhidi ya umaskini, ujinga na maradhi. Taasisi zinazoshindwa kuwafaa wengi kwa walio wachache kuzila na kuziua kwa manufaa yao binafsi sio taasisi Waislamu wanazostahili kuwa nao, maana taasisi zao zilistahili kuwa bora kabisa kuliko taasisi za dini nyingine hapa nchini.

Tuwakumbuke na kuwaenzi Waislamu wa miaka ya uhuru wa kisiasa ambao hawakusita kutumia mali na nafsi zao kupigania uhuru. Ili kuanzia leo tujenge uongozi wa kiislamu unaodhamiria kutumia mali na nafsi zao kuwakomboa Waislamu nchini na Afrika kwa ujumla.

No comments:

Post a Comment