KWANZA tutofauatishe kati ya Tovuti na Wavuti. Tovuti ni mtandao wa kompyuta kadhaa duniani zinazowezesha watu kuwasiliana kielektroniki. Wakati ambapo Wavuti ni kurasa za mtu binafsi au taasisi au serikali kwenye mtandao huo.
Afrika kwa ujumla wake iko nyuma sana katika kuwakilishwa kwake kwenye tovuti. Maudhui nyingi zilizopo leo katika mtandao ni za Ulaya, Marekani, India, China na kwingineko na sio Afrika. Aidha Tanzania ina uwakilishi sawa na hamna katika lugha yake ya Kiswahili. Maudhui za nje zilizopo katika Kiswahili ni nyingi kuliko maudhui za Kiswahili kutoka Tanzania.
Hivi sasa Tanzania ina wavuti moja ya serikali ambayo imejumuisha wizara zote humo ndani yake. Tovuti hii kwa wengi inaonekana kutokuwa na tofauti na ubao wa matangazo. Kwa kiasi kikubwa wavuti hiyo hairuhusu mawasiliano tasihili kati ya wahusika wizarani na wananchi. Bado kwa walio wengi wakiwa na shida serikali inawabidi kuswaga mguu na kwenda huko na kupewa mihadi inayochukua muda kutimizwa hadi matatizo yao yashughulikiwe au yatupwe kwenye kaburi la sahau.
Tofauti na nchi kama Rwanda, Mauritius na Ghana viongozi wetu hawaonekani kwenda na wakati wala kulichangamkia suala la Teknohama kwa kuzingatia kwamba kuna faida nyingi za kiuchumi, kijamii, kiutamaduni na kiteknolojia zinazoweza kupatikana kutokana na kuwa na mtazamo na msukumo wa kimaendeleo zaidi.
Pengine ni kwa sababu hii ndio maana nchi hizo ambazo zilikuwa nyuma ya Tanzania katika suala la Teknohama kwenye miaka ya 80 wakati sisi tunatawakali katika kuondoa kodi k atika uingizaji wa kompyuta leo zinatuonesha indiketa. Na kama tusipobadilika hatutaona hata moshi wa motokaa yao ya maendeleo ya Kiteknohama.
Swali hapa ni, je, serikali inaweza kulibadili hili na kuwa na mfumo wa wavuti unaoonekana kuwa na maana na faida kwa Watanzania na wasio Watanzania ?
Tatizo la kuwa na wavuti moja kwa wizara zote za serikali ni kuwepo kwa mlundikano wa maudhui zisizooana na zinazomkanganyisha na kumpotezea mtafutaji jambo na msomaji na hivyo kuongeza gharama kwa upande wake. Faida ya kuwa na wavuti kwa kila wizara ni kuwa unarahisisha utambulisho wa wizara, visheni na misheni yake na kazi zake. Vievile unarahisisha upatikanaji wa habari zinazohusu wizara na mawasiliano na utoaji huduma kwa wananchi na wote wanaohitaji huduma za wizara hiyo. Hali kadhalika, wavuti inaweza ikaonesha umuhimu au kutokuwepo na umuhimu wa kuwa na wizara fulani. Kwa kawaida, wizara ambayo hakuna mtu anayewasiliana nayo itagundulika kuwa ama inachapa kazi vizuri sana na hakuna aliye na malalamiko nayo au wizara hiyo ni boya ambalo linahitajika tu wakati wa dharura-pengine kisiasa.
Kwanini ni muhimu kuwa na Wavuti?
Zipo faida mbalimbali za kuwa na wavuti ambazo viongozi wetu wakizifahamau basi watachangamkia mara moja tenda ya kuhakikisha kuwa kila wizara inawakilishwa vilivyo katika tovuti. Faida hizo ni pamoja na:
. Kujulisha dunia kuwa upo. Katika dunia ya leo sio rahisi kujulikana kama upo kama huna uwakilishi katika mtandao. Bahati na manufaa mbalimbali zimeziendea taasisi na watu ambao wameonekana kuwepo mtandaoni. Wakati kuna taasisi na watu wengi tu ambao wamekosa mambo mbalimbali kutokana na kutokuwepo katika tovuti.
Aidha, yeyote aliye na tovuti ana fursa ya kujitangaza kwa haraka na kwa mapana zaidi kuliko yule asiye na wavuti.
. Mawasiliano. Wavuti nyingi hivi leo zinatoa fursa ya mawasiliano ya papo kwa hapo. Mathalani, BBC wanaweza wakawa hewani na wakati huo huo wanawasiliana na wasikilizaji wao kupitia wavuti yao.
. Shule au Chuo. Wavuti inaweza kuwa na huduma ya elimu au shule au chuo ambacho hutoa elimu au mafunzo mtandaoni. Yapo mambo mbalimbali yanayoibebesha serikali gharama kubwa leo lakini laiti yangeliweka mtandaoni serikali ingelihitaji watu wachache tu kuieneza elimu hiyo hadi vijijini.
. Chombo cha Habari. Wavuti ikitumika ipasavyo ni chombo cha habari cha uhakika, ndani na nje ya nchi. Kwa kutumia chombo hiki serikali inaweza kuepusha umbeya na uzushi ambao sikuhizi huanzia kwanza kwenye mtandao.
. Chemchemi ya fikra na mawazo huru. Wavuti huvuta na kukusanya mawazo ya kila aina -mazuri kwa mabaya na kuwapa viongozi mbalimbali fursa ya kujua mtazamo na msimamo wa wananchi na hivyo kuwaepusha kufanya maamuzi yatakayoharibu na badala yake kuwapa fursa ya kufanya maamuzi yatakayojenga nchi siku zote.
. Ukaguzi na uwajibikaji. Endapo serikali haina lolote la kuficha wavuti inaweza ikatumika kuwasilisha bajeti ya mapato na matumizi ya kila wizara siku zote katika mwaka mzima na hivyo watu kufuatilia bajeti hizo na kuzikosoa kabla mambo hayajaharibika.
. Mijadala. Hivi leo dunaini mijadala mingi ya kijamii, kiuchumi, kiutamaduni na kisiasa inafanyika katika tovuti kuliko katika sehemu nyingine zozote za mawasiliano ya umma. Watumiaji wengi wa tovuti ni watu waliosoma na wanaojua kile wanachokizungumza kuliko mbumbumbu.
. Kuongeza wingi wa taarifa na makala za lugha yako. Endapo wizara zote zitakuwemo katika tovuti na kisha machapisho yote ya Kiswahili toka enzi za Waarabu, Wajerumani na Waingereza na awamu zote za serikali baada ya uhuru kuwepo humo basi Tanzania itakuwa imechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza wingi wa maudhui za Kiswahili katika mtandano na hivyo kurahisisha mambo mengi yanayohitajika na Watanzania wa rika na elimu mbalimbai kupatikana humo.
. Kurahisisha kazi. Wavuti pia hutumika kurahisisha kazi. Badala ya mtu kufuata na kujaza fomu toka wizarani mtu anaweza kujaza fomu hiyo kwenye mtandao na kusubiri majibu toka kwenye mtandano ili kufuatilia kinachotakiwa hapo baadaaye. Hili litapunguza urasimu na msongamano katika wizara na hivyo kuwapa watumishi wa wizara nafasi ya kushughulikia masuala mengine muhimu zaidi kitaifa. Hii ina maana kwamba wavuti ni chombo cha huduma kinachoaminika na kufanya kazi haraka zaidi kuliko vyombo vingi vinginevyo.
. Biashara. Kwa zile wizara zinazochangia uzalishaji mali nchini kuna fursa pia kwa wavuti kutumika kibiashara. Biashara kubwa ya nchi za nje inaweza ikafanyika katika tovuti na pakiwa na udhibiti wa kutosha pasiwe na nyufa zinazoruhusu rushwa na utapeli kama ilivyo leo.
. Kwenda sambamba na teknolojia. Kwa kuwa na wavuti jambo hili peke yake linasaidia kuwaamsha watendaji wa wizara na hivyo kutokuwa mbumbumbu na kubaki nyuma kiteknolojia. Ni kitu kinachowapa changamoto pia ya watumishi hao kutaka kujua zaidi na kujiendleleza katika masuala ya Teknohama. Hili linawasaidia pia kubadilika na kwenda na utandawazi kiasi ambacho ni rahisi kwao kuajiriwa na nchi au makamapuni ya nchi za nje kwa faida yao na faida ya nchi.
. Kutoa fursa za ajira kwa vijana. Ni dhahiri pia kwamba pale kila wizara itakapokuwa na wavuti yake basi nafasi kadhaa za ajira zitakuwa zimeundwa kwa ajili ya vijana wa Kitanzania na hivyo kuongeza fursa ya wao kujiboresha na kuweza kushindania nafasi za ajira katika soko la dunia. Kwa hali ilivyo sasa ni kwamba vijana wakikosa changamoto na shughuli zinazowaingizia kipato wanaweza kugeuza ustadi na ubingwa wao wa Teknohama kufanya mambo ya kipuuzi yasiyo na maana kwa nchi na watu wetu.
. Tathmini. Wavuti pia ni njia ya mtu au taasisi kujitathmini na kutathminiwa na wengine kama mtu huyo anafanya au taasisi hiyo inafanya jambo la maana lenye faida kwa walaji au watumiaji wa huduma au bidhaa zake. Usipokuwa na wavuti mtu au taasisi yenyewe na watu wengine wote wanabaki katika giza kuhusu suala hili.
Hivi sasa Tanzania ina Sera ya Teknohama, ina taasisi kadhaa za kuanza utekelezaji kamilifu wa sera hizo na ina vijana wenye hamasa na tashwishi kubwa ya kufanya Teknohama kuwa kitega uchumi muhimu kitaifa. Kinachokosekana ni utashi wa kisiasa. Pamoja na mambo mengine ili tuondokane na kulemaa huku kiteknolojia ni muhimu kwa viiongozi wetu kuamka na kuanza kwa mapana na marefu kuitangazia dunia nia na azma ya Tanzania kuwa nchi inayokubali, kukumbatia na kutaka kujiendeleza zaidi kwa kutumia Teknohama. Nina hakika vyombo vyote vya habari viko tayari kuisaidia serikali na wananchi katika hili. Kinachongojewa ni kwa serikali kuonesha ari na nia hiyo ya kutambua kuwa Teknohama ni kitega uchumi muhimu katika maendeleo ya Tanzania.
Saturday, May 7, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment