TUKIO la wanafunzi wa Shule ya Sekondari Kibasila ni kumbukumbu inayosikitisha, kwani inahusu tabia iliyojijenga miongoni mwa watumishi mbalimbali wa umma. Tabia hiyo ni ile ya kufumbia macho na masikio matatizo ya wadogo na wanyonge hadi matatizo hayo yazae maafa. Ni mbegu inayopendwa na uongozi na mfumo wa serikali ambayo imebobea katika kupanga, lakini haifuatilii kwa makini na karibu utekelezaji wa mambo mbalimbali.
Ni uongozi ulio mbali na maisha, hali halisi na matatizo ya mwananchi wa kawaida. Ni uongozi unaoweza kukaa madarakani miaka mia moja na usilete mabadiliko yoyote. Ni uongozi uliopo madarakani kwa sababu ya udhaifu wa kielimu, kifedha, kikatiba na kimamlaka au kiuwezo wa kisiasa ya wananchi wengine? walio wengi ambao wangeliweza kuwa viongozi bora zaidi.
Ni zao la kuwa na wananchi walio wengi ambao ni mbumbumbu wa demokrasia na dhana ya kubadili serikali inayoshindwa kutimiza ahadi zake kwa wananchi.
Ingawa insha hii itawazungumzia polisi, lakini wao ni mfano hai tu na iko mingine pengine mibaya zaidi...
Mathalani je, ni wizara gani inayoruhusu mashimo wazi barabarani na inayochangia watu kuumia na hususan kuvunjika miguu kila siku mijini ? Hawalioni hili. Nani awawajibishe?
Ni nani anayethubutu kutobadili nguzo za umeme zinazokaribia kuanguka au kutodhibiti waya za umeme zinazopita chini badala ya juu ?
Ni nani anayeruhusu petroli stesheni kwenye makazi ya watu wakati hathubutu kuwapigia faya simu bali anawabipu tu?
Ni wahandisi gani na wizara gani inayoruhusu ghorofa zinazojengwa kwa 'udongo'.... yaani kwa maana zege ambalo halijafikia kiwango kinachotakiwa na hakuna anayewawajibisha ?
Iweje tuna shule zisizo na vifaa wala mbinu za kukabiliana na janga la moto au kwa kuwa?hakuna mtoto wa mkubwa anayesoma huko?
?
Inakuwaje wakubwa wana mashangingi yanayogharimu Sh 200 milioni, lakini kuna hospitali zisizo na gari la kubeba wagonjwa (ambulance)?
Inakuwaje tunakuwa na magari ya faya yasiyo na maji?wala njia za uhakika za kuwasiliana nayo?
Vipi wananchi wanakunywa maji yasiyotiwa dawa na hakuna anayewajibika? Ni nani anayedhibiti kiwango kinachotakiwa? Nani anayedhibiti usalama wake na nani anafuatilia?
Tumejipanga vipi kuona kwamba hakuna silaha ikiwemo mabomu yasiyo mahala pake au tunasiasaisha mpaka hili? Nani anayekula au kusalimika kwa maneno matamu?
Ni nani anayewajibika na watoto wetu wakienda au kutoka shuleni? Kuwalinda dhibi ya udhalilishaji na ukora wa makonda na wapiga debe kulikuwa nguvu ya soda? Na wazazi wenyewe mbona hawana umoja kukataa kunyanyaswa kwa watoto nchini hapa?
Kwa kifupi utaona maswali haya yanaelekeza kidole karibu kila idara na wizara. Uwajibikaji wetu ni usanii na wimbo huo umekwishawachosha wengi.? Tusipobadilika kuanzia sasa tuachane na jina Tanzania na kujiita Nigeria maana ndiko tunakoelekea!
Katika nadharia ya uongozi au menejimenti wote tunafahamu kwamba kuna kazi kadhaa zinazopaswa kutekelezwa. Kazi hizo pamoja na kuwepo kwa mipango, mikakati?na utekelezaji wenyewe ni kazi za oganaizesheni, uratibu, usimamizi au uongozi?na udhibiti au ufuatiliaji wa mambo na kuchukua hatua za haraka kurekebisha mambo pale yanapoonekana hayaendi kama yalivyopangwa.
Serikali yetu na watumishi wake wanasifika kama magwiji wa mipango. Lakini utekelezaji aghalabu huwa tofauti na mipango kwa walio wengi. Aidha suala la oganaizesheni yaani kuhakikisha kuwepo kwa mifumo na taratibu zinazofanya kazi,iwe ni kwa watu au vifaa bado ni duni.? Suala la uongozi na usimamizi kwa maana ya watu wanaohakikisha mambo yanafanyika kama yalivyopangwa lina kasoro kubwa.? Udhibiti na ufuatiliaji mambo hufanyika mambo pale tu yanapoharibika na sio wakati wote. Na matokeo yake ndiyo hapa tulipofikishwa leo. Lithibitishe hili kwa yaliyotokea BoT.
Wote ni kama tunaamka asubuhi na kwenda makazini mwetu kama maroboti kila asubuhi bila kuwa na azma hata moja ya kuhakikisha nchi angalau inashinda na kuyaacha nyuma matatizo ya msingi.
?
Kwanini serikali yetu iitwe gari ambalo betri imekwisha na haliendi bila kusukumwa ? Na ni vipi tunakuwa na betri mpya ili ukiwasha stata tu gari linaondoka?
Kwanini serikali yetu iponzwe na watumishi wake na kuonekana ni serikali inayolala na huamka tu jambo likishatokea? Kwanini tusiwe na watu wanaoweza kutuepusha na mabalaa kama wanavyofanya wao wenyewe majumbani kwao, ili kuwalinda wake, watoto na mifugo yao? Au ukishakuwa kiongozi siku hizi haustahili tena kujali ya wengine? Huu ndio uongozi kweli? Je, kwa namna hii tutafika ?
Katika suala la oganaizesheni ni kwa kiasi gani tunafahamu yote yanayopaswa kufanyika ili kazi au mradi fulani ufanikiwe? Tunagawaje kazi na majukumu ? Nani au idara gani au wizara gani anahusika na nini ?
Tathmini yake inafanyikaje? Na OPRAS iliyobuniwa na kuvalishwa vichwani mwetu na wataalamu wa rasilimali watu toka nje inafaa katika mazingira yetu ya Tanzania au nayo ni sawa na kutaka abiria kwenye gari lenye abiria wengi waliosimama kuliko waliokaa na kufunga mikanda? Je, kuna uratibu na nani anafanya uratibu huo? Je, kuna taarifa za utendaji na zinawafikia wanaostahili kuzipata ili kufanya maamuzi ya kuhakikisha mambo yote yanakwenda sawasawa wakati wote? Je, tunapitia mara kwa mara muundo, mfumo na taratibu, rasilimali watu na nyinginezo na kuona kinachohitajika kubadilika ili utendaji usiyumbe?
Je, hili lingefanyika kwenye ile njia panda ya Chang'ombe na Mandela viongozi pengine hata wa juu wa serikali wasingelikuwa wanafahamu mahala pale pana matatizo gani kiasi cha kuitwa 'Machinjioni'? Je, wote tulikuwa vipofu kutokuona kwamba pale hakuna taa za barabarani na usalama wa barabarani hawapataki kwa sababu wanazojua wao wenyewe?
Tatizo kama nilivyokwishawahi kusema hapo awali halistahili kabisa kuacha kuendelea kuwa tatizo. Lakini kwa Tanzania tatizo huendelea kuwa tatizo mwaka nenda, mwaka rudi. Na watumishi?wanaohusika hustuka tu pale tatizo kubwa linapotokea au watu wanapoamua kulala majiani na magari ya wakubwa yakashidwa kupita.
Kiongozi ni mtatua au mtafuta ufumbuzi wa matatizo. Yule anayeshindwa kupata ufumbuzi wa matatizo hata yale ya kawaida ana walakini. Hana sifa ya uongozi. Hafai kuwa kiongozi.
Maana akiwepo au asipokuwepo hali itakuwa ileile.
?
Huwa ninajiuliza hivi kweli watoto wa vigogo na vizito nao wangelikuwa katika walalamikaji hali ingefikia hivi?
Hivi unaojali tu wake na watoto wao kweli unaweza kuitwa uongozi wa watu ?
?
Ninasikia baadhi ya wakubwa wakilalama viongozi wenzao wawe na huruma. Huruma itatoka wapi bwana wee wakati mmekwishajenga tabia ya mkubwa kutojali kabisa ya mdogo?
Hili huanzia tunapowapa watu hawa ukubwa. Baadhi yao, iwe mawaziri, wakuu wa mikoa, makatibu wakuu na kadhalika hupewa maofisi wakubwa wajifiche huko wasikutane tena na watu; hupewa magari ya kifahari kuwabeba wao, wake zao na watoto wao, katika maofisi yao wengine wana vyoo na hata lifti zao tu binafsi na huko nchi za nje tunaambiwa hoteli wanazofikia hazifanani na padiemu zao. Mtu wa namna hii kweli utamtegemea aelewe ugumu wa maisha kwa Mtanzania wa kawaida ?
Sifa moja ya uongozi ni kiongozi kujishusha na kuwa sawa na anaowaongoza. Kisha akajifunza maisha na matatizo yao. Aidha akajua ni nini matamanio au matarajio yao. Na baada ya hayo akasuka mipango na mikakati inayowawezesha wote kwa pamoja kufikia malengo ya taasisi au eneo na wakati huo kutimiza ndoto za washikadau wote.
Nimalizie kwa kubainisha kuwa mimi ni kati ya wale wasioamini kwamba kiongozi atakayeitoa nchi kwenye ujinga, maradhi na umaskini anaweza akatoka katika kizazi hiki kinachojenga makasri ndani na nje ya nchi. Kwa upande wangu ninaamini kwamba kiongozi atakayeitoaTanzania katika aibu ya kuwa nchi maskini wakati ina kila sababu ya kuwa nchi tajiri, atakuwa yule atakayeshuka chini na kwenda kuishi na watu vijijini, ili aonje adha ya maisha ya Watanzania walio wengi, ajifunze na akamate matarajio na matamanio yao na kisha arudi Ikulu kuipanga nchi upya.
Hawa sio kati ya wale viongozi wanaokataa hata tu kwenda kuishi Dodoma wakati sio kijiji bali ni mji. Wala sio wale wanaotaka kuishi kama matajiri wa Ulaya katika nchi ya maskini wakubwa duniani. Kiongozi huyo ni mtu atakayekubali kuwa maskini ili awatajirishe kwanza wale anaowaongoza. Na huyu sidhani ni mtu nitakayekaa na kumuona?wakati wa uhai wangu maana viongozi waliopo hawajui kwamba muda nao ni rasilimali adimu. Na tukiyangoja maendeleo kwa muda mrefu wote tutakuwa tumekwishakufa.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment